MWAKILISHI wa jimbo la
Tunguu Simai Mohammed Said, akizungumza na wanafunzi wa skuli ya msingi Unguja
Ukuu, wakati wa zoezi la kupima afya ya kinywa na meno lililoendeshwa na
jumuiya ya HIPZ kwa kushirikiana na Wizara ya Afya Zanzibar skulini hapo leo
Machi 7, 2018. (Picha na Haroub Hussein).
DAKTARI
Feroz Jafferji ambaye ni mratibu wa jumuiya ya HIPZ, akimchunguza kinywa
mwanafunzi wa skuli ya Unguja Ukuu Mkoa wa Kusini Unguja ili kujua iwapo ana
ubovu wa meno, wakati jumuiya hiyo ilipotoa mafunzo ya kupiga mswaki vizuri.
(Picha na Haroub Hussein-Zanzibar).
Dk
Najat Abdalla akimuangalia mwanafunzi Hafidh Ali wakati wataalamu wa afya ya
kinywa na meno kutoka jumuiya ya HIPZ walipofika skuli ya msingi Unguja Ukuu
kutoa mafunzo juu ya namna bora ya kupiga mswaki. (Picha na Haroub Hussein).
DAKTARI Anna Dilan Yildiz akionesha namna ya kupiga mswaki vizuri kwa wanafunzi
wa shule ya msingi Unguja Ukuu katika jimbo la Tunguu Zanzibar ikiwa ni
maandalizi ya kuadhimisha ‘Siku ya Afya ya Meno’ duniani ifikapo Machi 20,
2018. Kushoto ni Mwakilishi wa jimbo la Tunguu Simai Mohammed Said. (Picha na
Haroub Hussein-Zanzibar).
MACHI
7, 2018
KUELEKEA
maadhimisho ya ‘Siku ya Afya ya Meno’ duniani, Jumuiya ya HIPZ leo Machi 7,
2018 ilikuwa katika skuli ya msingi
Unguja Ukuu kutoa mafunzo kwa wanafunzi juu ya namna bora ya kupiga mswaki.
Jumuiya
hiyo, kwa kushirikiana na madaktari wa Wizara ya Afya, pia iliwafanyia
uchunguzi wanafunzi wa skuli hiyo ili kubaini watoto wenye matatizo ya meno na
kuwapatia tiba.
Akizungumza
katika zoezi hilo, daktari dhamana kanda ya Unguja Muhidin Abdalla Mohammed,
alisema kutokana na umuhimu wa afya ya meno, wizara imaeamua kuufanya mwezi
Machi kuwa wa kampeni ya usafi wa kinywa na meno.
Alisema,
kampeni hiyo ni miongoni mwa maandalizi kuelekea ‘Siku ya Afya ya Meno’
kimataifa ambayo huadhimishwa tarehe 20 Machi ya kila mwaka, ambayo inafanywa
ili kukuza uelewa wa watu katika afya ya meno ambayo alisema bado jamii
haijaipa kipaumbele.
Dk.
Abdalla alisema tayari zoezi kama hilo limefanyika jana (Machi 6) katika skuli
ya Kivunge Mkoa wa Kaskazini Unguja, na kesho Machi 8 wamepanga kufika skuli ya
Jambiani Mkoa wa Kusini Unguja, na wiki ijayo watakuwa skuli za Mwanakwerekwe,
Mjini Magharibi.
“Afya
ya meno ni muhimu lakini bado jamii haina mwamko wa kuyashughulikia wa uzito
unaostahili kama wanavyofanya kwenye mambo mengine kiafya. Aidha ni vyema iwe
tunawachunguza watoto mapema pamoja na kuwafunza namna bora ya kupiga mswaki
ili kuepusha uharibifu,” alifahamisha Dk. Abdalla.
Alieleza
kuwa hapa Zanzibar, tatizo la meno ni kubwa kwani yanawapata wananchi wengi kwa
nama tafauti, ama kuugua meno kwa kutoboka au kuumwa ufizi, lakini akasema
yanaweza kuepukwa kama jamii itafuata maelekezo ya kitaalamu katika kuyatunza.
Daktari
huyo aliwataka wananchi waache kutumia dawa za kienyeji katika kutibu maradhi
ya meno, ambazo alisema vipimo vyake si vya uhakika, bali wakiona dalili za na
matatizo ya meno wafike hospitali mapema na kupata ushauri na tiba za
kitaalamu.
Aliishukuru
jamii kwa kuwapa ushirikiano na kujitokeza kwa wingi katika kampeni hiyo,
ambayo alisema ni muhimu katika
kuyapatia ufumbuzi matatizo ya meno.
Mapema,
Mwakilishi wa jimbo la Tunguu Simai Mohammed Said, aliwashukuru wataalamu hao
kwa kutoa elimu hiyo kwani usafi wa kinywa ni muhimu kwa kujenga heshima ya mtu
na mapenzi mbele ya watu anaoishi pamoja nao.
Alieleza
kufarijika kwa juhudi za walimu wa skuli hiyo katika kutoa elimu ya usafi kwa
wananfunzi, mbali ya fursa kama hizo za huduma za kiafya zinazowafikia mara kwa
mara.
Mwakilishi
huyo aliwaahidi madaktari hao kwamba uongozi mzima wa jimbo utaendelea kutoa
ushirikiano kwa taasisi za kiserikali na binafsi, kila zinapohitaji kuwapeleka
wananchi huduma mbalimbali za kijamii.
Zoezi
hilo litaendelea hadi Machi 20, mwaka huu, ambapo itakuwa kilele cha
maadhimisho ya ‘Siku ya Afya ya Meno’ duniani, huku likijumuisha madaktari
wengine wa kujitolea kutoka nchini Ujerumani na Umoja wa Falme za Kiarabu.
No comments:
Post a Comment