Habari za Punde

Maadhimisho ya siku ya kifua kikuu duniani

 Waziri wa Afya Hamad Rashid Mohammed kushoto akiwa katika maandamano ikiwa ni shamrashamra za kilele cha maadhimisho ya siku ya kifua kikuu kilichofanyika Ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilishi.Kulia kwake ni Mkuu wa Mkoa Mjini Magharibi Ayoub Mohamed Mahmoud.
 Baadhi ya Wananchi waliohudhuria maandamano hayo ya kilele cha maadhimisho ya siku ya Kifua kikuu Duniani.
 Meneja kitengo shirikishi Ukimwi,Kifua kikuu na Ukoma Farhat Khalid akitoa salamu za utangulizi katika maadhimisho hayo ukumbi wa Zamani wa Baraza la Wawakilishi mjini Zanzibar
 Mwakilishi wa Shirika la Afya Duniani WHO Dkt. Andemichel Ghirmay akitoa salamu za Shirika hilo kwa wananchi wa Zanzibar katika kilele cha maadhimisho ya siku ya kifua kikuu kilichofanyika Ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilishi.
 Waziri wa Afya Hamad Rashid Mohammed akitoa hutuba yake ya kilele cha maadhimisho ya siku ya kifua kikuu kilichofanyika Ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilishi.Kulia kwake ni Naibu wake Harusi Said Suleiman na kushoto ni Mwakilishi wa Shirika la Afya Duniani WHO Dkt. Andemichel Ghirmay
  Baadhi ya Washiriki wa kilele cha maadhimisho ya siku ya kifua kikuu kilichofanyika Ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilishi.
  Baadhi ya Washiriki wa kilele cha maadhimisho ya siku ya kifua kikuu kilichofanyika Ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilishi.
Mkuu wa Wilaya ya Mjini Marina Joel Thomas akitoa neno la shukran katika kilele cha maadhimisho ya siku ya kifua kikuu kilichofanyika Ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilishi mjini Zanzibar Picha na Abdallah Omar-Maelezo Zanzibar .

Na Faki Mjaka-Maelezo Zanzibar 
Serikali imeonya kuwanyang’anya Leseni na kuzifunga biashara za Wafanyabishara watakaobainika kuuza Dawa za Serikali katika maduka yao.
Hatua hiyo ni moja kati ya juhudi za kusimamia upatikanaji wa huduma za afya kwa kiwango kinachostahiki.
Waziri wa Afya Hamad Rashid Mohammed ametoa onyo hilo katika kilele cha maadhimisho ya siku ya kifua kikuu kilichofanyika Ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilishi.
Amesema Serikali licha ya kutumia zaidi ya Shilingi Bilioni kumi za kitanzania kwa ajili ya kununulia Dawa lakini imegundulika kuwa wapo Wafanyabiashara huziuza Dawa hizo katika maduka yao.
Ametaja baadhi ya Dawa zilizobainika kuuzwa kuwa ni pamoja na Dawa za Malaria na Dawa za Uzazi wa mpango ambazo serikali huzitoa bure kwa wananchi.
Amesema pesa hizo za kununuliwa Dawa hutolewa na Serikali kupitia Kodi za Wananchi na kwamba yeyote anayenda kinyume kwa kuwazidishia mzigo wa matibabu wananchi na Serikali kwa ujumla hatovumiliwa.
“Lazima tuchunge rasilimali zetu na tujali wananchi wetu..Kwa mfanyabiashara anayetaka kununua Dawa akaagize kokote lakini sio kuchukua Dawa zetu ambazo tunatoa bure kwa wananchi wetu mkawauzia hizo hizo, hatukubali tutafunga leseni na biashara hata kama ni Kidonge kimoja” alionya Waziri Hamad.
Amerejea kauli yake alioitoa siku za karibuni ya kuwataka watendaji wa Wizara ya afya ambao bado wanajimilikisha Mali za Serikali kinyume na sheria wazirudishe kabla ya mwezi mmoja kuisha.
Akizungumza kuhusu Kifua kikuu Waziri Hamad amesema Serikali imedhamiria kupambana ipasavyo na ugonjwa huo ambapo kwa mujibu wa taarifa aliyoitoa Waziri huyo Dkt. Shein ambaye ni Rais wa Zanzibar atakuwa ni mpambanaji namba moja wa ugonjwa huo.
Waziri huyo amefahamisha kuwa Zanzibar imefanikiwa kwa kiasi kikubwa katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Malaria na kwamba ipo haja kuelekeza nguvu katika magonjwa mingine ikiwemo Kifua kikuu.
Amesema ni jambo linalowezekana pale ambapo kila mmoja kwa nafasi yake kuanzia Viongozi wa familia hadi ngazi ya taifa kuwa tayari katika mapambano ya Kifua Kikuu.
“Kila kiongozi akiwajibika ipasavyo hakuna uwezekano wa Kifua kikuu kushambulia Wananchi wetu kama ilivyo sasa” alinasihi Hamad
Amesema ni vyema ukawekwa utaratibu maalum ya kuwatunza Viongozi wa Shehia ambao katika Shehia zao hakuna Wagonjwa wa Kifua kikuu kutokana na kazi nzuri wanayoifanya.
Hatua hiyo itachochea ari kwa Viongozi wengine kuzidisha mapambano kukabiliana na ugonjwa huo ambao bado unaendelea kusumbua wananchi Unguja na Pemba.
Awali Mwakilishi wa Shirika la Afya Duniani WHO Dkt. Andemichel Ghirmay ameiomba Wizara kuongeza juhudi za kutoa elimu kwa wananchi ikiwemo kutambua dalili za ugonjwa huo na namna ya kujikinga.
Amesema WHO inajivunia kufanya kazi na Serikali ya Mapinduzi kutokana na mashirikiano wanayotoa kwa shirika hilo.
Kwa upande wake meneja Meneja kitengo shirikishi Ukimwi,Kifua kikuu na Ukoma Farhat Khalid wakati akitoa salamu za utangulizi alihamasisha upatikanaji wa rasilimali kwa ajili ya vitendea kazi.
Aidha aliomba Serikali na Wananchi lwa ujumla kuufanya ugonjwa wa Kifua Kikuu kuwa ajenda ya kudumu katika Vikao vyao.
Kwa mujibu wa takwimu za Wizara ya Afya jumla ya Wagonjwa 948 wamegunduliwa kuwa na ugonjwa wa Kifua kikuu mwaka 2017 ambapo wagonjwa tisa wamegundulika kuwa na Kifua kikuu sugu.
Kila ifikapo Machi 24 ya kila mwaka ni siku ya maadhimisho ya Kifua Kikuu ulimwenguni ambapo hutumika kuikumbusha na kuishajihisha jamii kuwa Kifua kikuu bado ni janga kubwa katika jamii.
Maadhimisho ya mwaka huu yameambatana na ujumbe usemao “tunahitaji viongozi mahiri wa kuongoza mapambano ya kumaliza kifua kikuu”

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.