RAIS wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameipongeza Kampuni
ya Kimataifa ya Mitandao ya Kisasa ya Mawasiliano ya ZTE ya China kwa kuunga mkono azma ya Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar katika kutekeleza Mradi wa Serikali Mtandao
(e-Government) ili kwenda sambamba na mabadiliko ya dunia na kuimarisha ufanisi
wa utendaji Serikalini.
Dk. Shein aliyasema
hayo leo Ikulu mjini Zanzibar wakati alipokuwa na mazungumzo na Ujumbe wa
Kampuni ya Kimataifa ya Mitandao ya Kisasa ya Mawasiliano ya ZTE kutoka nchini
China ukiongozwa na Makamo Mkuu wa Rais wa Kampuni hiyo Zhao Peng.
Katika maelezo yake,
Rais Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo na ujumbe wake kuwa Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar imeridhishwa na hatua za utekelezaji wa awamu ya kwanza
ya Mradi huo wa Serikali Mtandao
(e-Goverment) na kueleza mipango inayoendelea katika kuanza awamu ya pili ya
Mradi huo.
Alieleza kuwa tayari
mchakato wa kuanza kwa awamu ya pili ya Mradi huo unaendelea kukamilishwa ambapo utahusisha uanzishwaji wa Mfumo wa
Huduma za Afya kwa njia ya Kielektroniki (e-Health) pamoja na Uanzishwaji wa Mfumo wa Kodi
(e-Tax).
Aidha, Rais Dk. Shein
alieleza kuwa hatua hiyo itaimarisha ufanisi wa utendaji Serikali, utoaji wa
huduma na upatikanaji wa taarifa za umma na kuimarisha matumizi ya (TEHAMA) kwa
ujumla hali ambayo itaifanya Zanzibar nayo kuingia katika mabadiliko ya
kiteknolojia kwa mafanikio makubwa.
Sambamba na hayo, Rais
Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo haja ya kuwepo utaratimu na mfumo maalum wa
kupata mafunzo kwa watendaji kutoka katika sekta hizo husika ili irahisishe
utendaji wa shughuli hizo zitakapoanza.
Alieleza kuwa kwa vile
teknolojia hiyo ni mpya na muhimu hapa nchini, hivyo suala la kupatiwa mafunzo
kwa watendaji husika linapaswa kupewa kipaumbele huku akiipongeza Kampuni hiyo
kwa mafanikio iliyoyapata na kuzivutia nchi nyingi duniani.
Nae Makamo Mkuu
wa Rais wa Kampuni ya Kimataifa ya
Mitandao ya Kisasa ya Mawasiliano ya ZTE kutoka nchini China Zhao Peng alimpongeza Rais Dk. Shein kwa
ushirikiano mzuri uliopata kampuni hiyo katika kutekeleza majukumu yake kwenye
awamu ya kwanza ya Mradi huo.
Alieleza kuwa
makubaliano ya utekelezaji wa Mradi huo kwa awamu ya Pili ambapo Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar kwa kushirikiana na Serikali ya Watu wa China chini ya Kampuni
ya ZTE zimekubaliana kutoa fursa nzuri kwa Zanzibar kutumia mfumo wa Teknolojia
ya kisasa (TEHAMA).
Kiongozi huyo alieleza
matarajio yake kuwa Zanzibar itakuwa ni miongoni mwa nchi katika ukanda wa
Afrika Mashariki na Kati itakayokuwa na mafanikio makubwa katika mfumo wa
Teknolojia ya Kisasa (TEHAMA).
Aidha, kiongozi huyo
aliunga mkono wazo la Rais Dk. Shein la kutoa mafunzo kwa watendaji husika
katika mradi huo na kueleza kuwa Kampuni yake imelichukua na italifanyia kazi
ili kuona utekelezaji wake.
Mradi wa awamu ya pili
wa Serikali Mtandao (e-Government) utahusika na ujenzi wa mfumo wa miundombinu
ya mawasiliano “Access Network” ambao unakusudia kuleta ufanisi katika matumizi
ya (TEHAMA) ambapo utapeleka huduma za mawasiliano katika majengo ya serikali
pamoja na hospitali zilizoteuliwa na taasisi husika.
Pia, utahusika na
mfumo wa huduma za afya kwa njia ya kielektroniki (e-Health) kwa lengo la kuimarisha utoaji wa huduma za afya
hapa Zanzibar na kukabiliana na matatizo mbali mbali ambayo yamekuwa
yakijitokeza katika utoaji wa huduma hizo pamoja na kupata vifaa kadhaa vitakavyosaidia
kuimarisha utoaji wa huduma hizo.
Mradi huu unategemewa
kuanzisha mfumo wa utunzaji wa taarifa za afya katika Hospitali zote kuu
zilizopo Zanzibar ili kutunza kumbukumbu katika hospitali hizo.
Serikali ya Mapinduzi
ya Zanzibar kupitia Mradi wa Serikali Mtandao (e-Government) imeona kuna haja
kubwa ya kuwa na mradi utakaosimamia ukusanyaji wa Kodi za Zanzibar kwa mfumo
wa teknolojia ya Habari na mawasiliano (e-Tax) ambapo lengo kuu la mradi huo ni
kuiwezesha Serikali kukusanya kodi kwa kiwango kikubwa kwa njia salama na kwa
ufanisi zaidi.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment