Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein Azungumza na Mkurugenzi Mkuu wa UNIDO Ikulu leo.


Rais  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kushoto)  akisalimiana na  Mkurugenzi  Mkuu wa UNIDO Bw. Li Yong alipofika Ikulu Zanzibar leo kwa mazungumzo pamoja na Ujumbe aliofuatnana nao.09 Machi 2018.
Rais  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein(kulia) akizungumza na  Mkurugenzi  Mkuu wa UNIDO Bw. Li Yong wakati alipofika Ikulu Zanzibar leo akiongozana na  Viongozi mbali mbali wa Shirika hilo
Rais  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein(kulia) akizungumza na  Mkurugenzi  Mkuu wa UNIDO Bw. Li Yong (wa pili kulia)wakati alipofika Ikulu Zanzibar leo akiongozana na  Viongozi mbali mbali wa Shirika hilo ,[Picha na Ikulu.]

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza haja kwa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Maendeleo ya Viwanda (UNIDO) kuiunga mkono Zanzibar katika kutekeleza azma yake ya kuimarisha viwanda vidogo vidogo na vya kati ili kufikia dhima ya uchumi wa viwanda na kukuza soko la ajira nchini.

Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo wakati alipokuwa na mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Maendeleo ya Viwanda (UNIDO) Li Yong Ikulu mjini Zanzibar.

Katika maelezo hayo Rais Dk. Shein alimueleza Mkurugenzi Mkuu huyo mikakati iliyowekwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuhakikisha sekta ya viwanda inaimarika.

Dk. Shein alimueleza Mkurugenzi Yong kuwa Serikali tayari imeandaa mipango na kutekeleza mikakati ya kuimarisha sekta ya viwanda kwa kutambua umuhimu wake katika kuchangia uchumi, kuimarisha sekta nyengine za uzalishaji na biashara, kuimarisha upatikanaji wa bidhaa mbali mbali na kutoa fursa kubwa ya ajira.

Aidha, Rais Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo kuwa Zanzibar inathamini sana ushirikiano na uhusiano mwema na wa muda mrefu kati yake na (UNIDO) na kuahidi kuuendeleza.

Dk. Shein alimueleza Mkurugenzi Mkuu huyo kuwa Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya CCM ya mwaka 2015-2020 imezielekeza Serikali zake mbili kuelekea katika uchumi wa Viwanda, ili iwe ni ukombozi halisi wa kuwapatia fursa zaidi za ajira vijana sambamba na kuimarisha uchumi wa Tanzania.

Alisema kuwa hatua za UNIDO kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta hiyo ya viwanda ina umuhimu mkubwa na itasaidia katika kufikia lengo lililokusudiwa.

Rais Dk. Shein alisema kuwa miongoni mwa juhudi zinazochukuliwa ni pamoja na kuimarisha kilimo kikiwemo kilimo cha mwani ambacho kimekuwa mkombozi mkubwa kwa wananchi lakini bado kumekuwepo baadhi ya changamoto zinazokikabili kilimo hicho, hivyo kuna haja kwa UNIDO kutoa ushirikiano wake katika eneo hilo ili kusaidia kilimo hicho hasa kwa akina mama ambao ndio wengi wanaojishughulisha na kilimo hicho.

Aidha, Rais Dk. Shein alisema kuwa Zanzibar imezungukwa na bahari na pia, ni mwanachama wa Jumuiya ya Nchi zinazopakana na Bahari ya Hindi (IORA), lakini bado haijazitumia vyema rasilimali zinazotokana na bahari kwa kutokuwa na viwanda vinavyotegemea mali ghafi na rasilimali za bahari.

Hata hivyo, Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo hatua na juhudi zinazochukuliwa na Serikali katika kuhakikisha Zanzibar inaanzisha Kampuni yake ya Uvuvi na kueleza haja kwa UNIDO kuunga mkono jitihada hizo.

Rais Dk. Shein alimueleza Mkururugenzi Yong kuwa Zanzibar inawakaribishwa wawekezaji kuja kuwekeza katika sekta ya viwanda, vikiwemo viwanda vya samaki na rasilimali za bahari.

Sambamba na hayo, alieleza kuwa Zanzibar imejaaliwa kuwa na utajiri wa viungo vya chakula na kusisitiza kuwa iwapo vitaongezwa thamani mafanikio makubwa yatapatikana huku akitumia fursa hiyo kueleza hatua zilizofikiwa na Zanzbar katika kuimarisha Mfumo wa Teknolojia ya Kisasa (TEHAMA), hatua ambayo itasaidia katika kuimarisha sekta ya viwanda.

Nae Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Maendeleo ya Viwanda (UNIDO) Li Yong alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa Shirika hilo litaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuhakikisha inafikia malengo iliyojiwekea katika kuimarisha sekta ya viwanda.

Mkurugenzi Li Yong alimueleza Dk. Shein kuwa UNIDO imeamua kwa makusudi kuiunga mkono Tanzania ikiwemo Zanzibar kwa kutambua kuwa tayari kuna mipango na mikakati kabambe imewekwa katika kuimarisha sekta ya viwanda.

Aidha, Mkurugenzi Mkuu huyo alimueleza Rais Dk. Shein kuwa UNIDO itaendeleza uhusiano na ushirikiano wake na Zanzibar na kupongeza mashirikiano mazuri yaliopo kati ya Shirika hilo na Wizara ya Bishara na Viwanda ya Zanzibar.

Katika maelezo yake Mkurugenzi Mkuu huyo alieleza haja ya kuimarisha teknolojia katika kuimarisha sekta ya viwanda, biashara na masoko.

Alieleza kwamba nchi nyingi duniani zimeweza kuwatafutia masoko wajasiriamali wake kwa kuwawekea mkazo katika uendeshaji wa Biashara kwa njia ya mitandao. Kwa hivyo, alisema kuwa itakuwa ni vyema ikiiwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaweka mkazo katika eneo hilo ili kuweza kukabiliana na changamoto ya kuwepo masoko ya uhakikika ya bidhaa mbali mbali zinazotengenezwa nchini.

Mkurugenzi Mkuu huyo alimueleza Rais Dk. Shein mikakati aliyowekwa na UNIDO katika kuhakikisha inaongeza miradi iliyopo sambamba na kuimarisha miradi iliyopo kwa upande wa Tanzania Bara na Zanzibar na kuitaka Zanzibar kujiandaa vyema kuipokea miradi hiyo

Kiongozi huyo wa UNIDO alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa Shirika hilo litahakikisha linatoa kipaumbele chake katika kuiamrisha kilimo cha mwani ili kuhakikisha akina mama wananufaika na kilo hicho huku akiahidi kuvifanyia kazi vipaubele vyote vilivyowekwa na Zanzibar katika kuimarisha sekta ya viwanda ili kwenda sambamba na uchumi wa viwanda
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.