Habari za Punde

Kampeni ya ‘tokomeza malaria’ Zanzibar yazinduliwa kwa ugawaji vyandarua

 Waziri wa Afya Zanzibar akizungumza na waandishi wa habari mbalimbali kuhusiana na uzinduzi wa ugawaji wa vyandarua,katika mazungumzo yaliofanyika  ukumbi wa Wizara ya Afya Mnazimmoja Mjini Zanzibar.
 Waandishi wa habari mbalimbali waliohudh,uria katika mkutano wa uzinduzi wa ugawaji wa vyandarua katika mazungumzo yaliofanyika  ukumbi wa Wizara ya Afya Mnazimmoja Mjini Zanzibar.
 Naibu Meneja Mradi wakumaliza malaria Zanzibar,Faiza Bwanakheri Abbas akizungumza katika mkutano wa uzinduzi wa ugawaji wa vyandarua mazungumzo yaliofanyika  ukumbi wa Wizara ya Afya Mnazimmoja Mjini Zanzibar.
 Mwandishi wa habari wa Gazeti la Nipashe Rahma Suleiman akiuliza masuala katika mkutano huo.

Mkurugenzi wa Vector Work Waziri Nyoni akijibu masuala alioulizwa na waandishi wa habari katika mkutano huo (Picha na Abdalla Omar Habari – Maelezo).



Na Salum Vuai, MAELEZO
KIASI cha vyandarua 195,000 vilivyotiwa dawa ya kuulia mbu waenezao malaria, vinatarajiwa kugawiwa kwa nyumba 38,884 Unguja na Pemba.
Akizindua kampeni ya kupambana na malaria leo Aprili 4, 2018 katika uwanja wa Kisonge, Waziri wa Afya Hamad Rashid Mohammed, amesema hatua vyandarua hivyo vitaelekezwa zaidi katika maeneo yanayoonekana kuwa sugu wa maradhi ya malaria.
Hatua hiyo ni katika mkakati endelevu wa kutokomeza malaria moja kwa moja, ambapo ugawaji wa vyandarua hivyo umelenga zaidi kuwafikia akinamama wajawazito na watoto walio chini ya umri wa miaka mitano.
Waziri Hamad amesema dawa iliyotiwa katika vyandarua hivyo ina uwezo wa kudumu kwa miaka mitatu na hivyo kusaidia maambukizi mapya ya malaria nchini.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa ugawaji wa vyandarua hivyo, Waziri Hamad amesema kuwa malaria bado yapo na juhudi za makusudi zinahitajika ili kuweza kuyatokomeza.

Amesema kuwa, wagonjwa 4,139 walithibitishwa kuugua malaria katika hospitali za Zanzibar mwaka 2017, ikilinganishwa na wagonjwa 3,424 mwaka 2016 ambapo wagonjwa wanne walifariki dunia mwaka jana kutokana na maradhi hayo.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, kiasi cha shilingi bilioni moja nukta tatu zitatumika katika kipindi cha mwaka 2018 kwa ajili ya kupambana na ugonjwa huo visiwani Zanzibar.

Amesema jukumu la kumalizia maradhi hayo nchini halipasi kuachiwa Wizara ya Afya pekee, bali kila mwananchi ana wajibu wa kutoa ushirikiano hasa katika kuweka mazingira safi ili kuzuia mbu wa malaria kuzaliana.
“Inasikitisha kwamba pamoja na juhudi za serikali katika kuilinda afya za wananchi wake, watu wengi bado hawataki kubadilika kwani hata kusafisha mazingira ya majumbani mwao wanaona ni kazi ya serikali. Hii ni hatari,” alieleza.
Aliwaomba wananchi kushirikiana kwa pamoja katika kufukia madimbwi yanayotuwama maji kwa muda mrefu kwenye maeneo yao badala ya kujipweteka wakitegemea nguvu za serikali.
Aidha aliwataka wananchi watakaonufaika na vyandarua hivo kuvitumia katika njia bora na salama ili viweze kudumu kwa muda mrefu kama ilivokusudiwa.

Halikadhalika aliwataka kuachana na kasumba zinazoenezwa na watu wasiokuwa na nia njema, kwamba vyandarua hivyo pamoja na dawa za malaria zinazopigwa majumbani vinapunguza nguvu za kiume na pia husababisha ugumba kwa wanawake, akisema huo ni uzushi.

Naibu Meneja mradi wa malaria Zanzibar Faiza Bwanakheri Abbas alisema mpango wa kumaliza malaria hautaweza kufanikiwa iwapo jamii haitajenga utaratibu wa kuweka usafi katika maeneo yote yanayowazunguka.

Alisema kitengo chake kimejiwekea utaratibu maalumu wa kupitia maeneo yote hatarishi na kuwataka wananchi wajitokeze kusafisha mazingira yao.

Kiasi cha shilingi bilioni 1.3 zinatarajiwa kutumiwa katika kipindi cha mwaka 2018 kwa ajili ya kupambana na ugonjwa huo visiwani Zanzibar ukiwa msaada kutoka Shirika la Misaada ya Kimataifa la Marekani (USAID) na Mfuko wa Fedha wa Dunia (Global Fund).

IMETOLEWA NA HABARI MAELEZO-ZANZIBAR

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.