Habari za Punde

Kutokuwepo huduma rafiki kwenye vyombo vya sheria kunakwamisha wanawake kupeleka malalamikko wanapodhalilishwa


NA/ ZUHURA JUMA, PEMBA

KUKOSEKANA kwa huduma rafiki na ufaragha kwa baadhi ya vyombo vya sheria, kunakwamisha juhudi za wanawake kupeleka malalamiko yao wakati wanapodhalilishwa kutokana na kuona aibu.

Hali hiyo inapelekea kuongezeka kwa vitendo vya ukatili kwa wanawake na watoto, kwani wao ndio wanaoathirika zaidi, ingawa wanasuasua kuvifikia Vyombo vya sheria kuripoti pale wanapodhalilishwa, kutokana kutokuwepo kwa huduma rafiki katika vituo hivyo.

Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi, kwa nyakati tofauti  wanajamii wa shehia sita zilizofikiwa wa Mradi wa kukuza Usawa wa Kijisia na kuwawezesha Wanawake (GEWE), walisema   ni vyema kwa Serikali  kuweka wahudumu wanawake katika sehemu za kupeleka malalamiko ya akinamama, ili kuweza kuelezea kwa uwazi yanayowakumba.

“Sehemu nyingi ukienda unawakuta wanaume tena kwenye matatizo kama haya ya udhalilishaji, sisi kama wanawake tunahitaji sehemu iliyofaragha tena kuwe na wanawake wenzetu, maana tunaona aibu”, anashauri.

Sharifa Said Hamad (45) mkaazi wa shehia ya Kangagani, alisema kuwa  ili wanawake waweze kuripoti baada ya kudhalilishwa, zinahitajika huduma rafiki katika Vyombo vya sheria, kwani wanapomkuta mwanaume huona aibu na kushindwa kupeleka malalamiko yake.

“Kwa kweli mtu anaona aibu, huku ameshadhalilishwa, halafu anakwenda kwenye vyombo husika anawakuta wanaume, hii inavunja moyo”, alisema mama huyo.

Nae, Mama mwenye umri wa miaka (30) mkaazi wa Shengejuu ambaye mtoto wake (16) alibakwa mwaka jana, alieleza kuwa, mwanamke anapodhalilishwa, wanaume wengine wote huwaona maadui, ambapo anapokimbilia katika vyombo vya sheria na kumkuta tena mwanamme, huona aibu zaidi kuelezea alivyodhalilishwa.

 “Kesi ya mtoto wangu sijui imefikia wapi, kwani tokea siku hiyo mimi sijaenda tena, anakwenda mume wangu tu, na huyo mtuhumiwa juzi amebaka mtoto mwengine maeneo ya hapa hapa mtaani, kwa kweli inaumiza”, alihadithia.

Nao, waratibu wa Shehia sita za GEWE, ambazo ni Shengejuu, Mchangamdogo, Kinyikani, Kiungoni, Kangagani na Mjini Ole walieleza kuwa, kuna baaadhi ya wanawake bado ni wagumu kuripoti kwa kile wanachodai kuona aibu, ingawa baada ya elimu, wamekuwa wakiripoti angalau kwa waratibu.

Jumla ya kesi 20 wameripoti wanawake wenyewe katika shehia hizo kuanzia mwaka 2015, hadi Oktoba mwaka jana kati ya kesi 51 za udhalilishaji walizopokea waratibu wa wanawake na watoto.

Mussa Suleiman Said, mkaazi wa Kinyikani, alisema kuwa ni vyema katika maeneo ya kupeleka malalamiko ya wanawake, kuwepo na wanawake wa kupokea malalamiko hayo, ili wasione aibu zaidi ya kile walichodhalilishwa.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kaskazini Pemba, Haji Khamis Haji, alisema  baadhi ya wanawake wamekuwa wagumu kuripoti, jambo ambalo limesababisha kwa Wilaya ya Wete Dawati la kijinsia Mkoa huo kupokea kesi 78 walizoripoti wanawake kati ya kesi 209 za udhalilishaji zilizofikishwa hapo kuanzia mwaka 2015 hadi Oktoba mwaka jana.

Mratibu wa kituo cha Mkono kwa Mkono Wilaya ya Wete, Asma Mohamed Fasihi, alisema wanawake wamekuwa wakipoteza ushahidi kwa kushindwa kufika kwenye vyombo vya sheria kuripoti, ambapo alipokea kesi moja (1) iliyofikishwa na mwanamke wenyewe mwaka 2015 hadi mwaka jana kati ya kesi 165 za udhalilishaji zilizofikishwa kituoni hapo.

Ofisa Ustawi wa Jamii Wilaya ya Wete, Haroub Suleiman Hemed , alisema   kwa upande wake wanawake huripoti kwa kiwango kikubwa kesi za madai kuliko jinai na kuwataka  wawe mstari wa mbele kutetea haki zao kwa kufika katika vyombo vya sheria.

Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, sura ya tatu kifungu cha 12 (3) kinaeleza ‘haki za raia, wajibu wa maslahi ya kila mtu yatalindwa na kuamuliwa na mahakama pamoja na vyombo vyengine vilivyomo ndani ya nchi… ’ ingawa wanawake wamekuwa wakijisahau kuripoti kesi za udhalilishaji na kujiona hawawezi.

Mkataba wa haki za kimataifa wa kupunguza aina zote za ubaguzi dhidi ya wanawake wa mwaka 1979, Ibara ya 2, inalazimisha nchi wanachama kuchukua hatua madhubuti zinazofaa zikiwemo za kisheria kupinga udhalilishaji dhidi ya wanawake.

Mratibu wa TAMWA, Mzuri Issa Ali, alisema   udhalilishaji kwa wanawake na watoto bado upo Zanzibar, hivyo wanajamii wawe tayari kudhibiti vitendo hivyo kwa kwenda kuripoti na kuzisimamia ipasavyo kesi za matendo hayo.

Hata hivyo pamoja na elimu inayotolewa kwa wanajamii katika kutokomeza vitendo vya ukatili  kwa wanawake na watoto, ingawa bado vinaongezeka kutokana na baadhi ya wanawake kuona aibu kwenda kuripoti

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.