STATE
HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar
05.04.2018
RAIS wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, amesema kuwa kuna kila sababu ya kumuenzi
Marehemu Mzee Abeid Amani Karume kwa kuikomboa Zanzibar na kuwaachia
Wazanzibari Serikali yenye mfumo madhubuti unaozingatia Utawala wa Sheria.
Dk. Shein aliyasema hayo, leo
katika hotuba yake ya ufunguzi wa Kongamano la Kumbukumbu ya Rais wa Kwanza wa
Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Marehemu Mzee Abeid Amani Karume,
lililoandaliwa na Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, huko katika ukumbi wa
Chuo hicho Bububu, Wilaya ya Magharibi “A”, Unguja.
Katika hotuba yake hiyo,
Rais Dk. Shein alisema kuwa bado wananchi wa Zanzibar na Tanzania nzima kwa
jumla wanathamini sana hekima, busara na misingi imara ya maendeleo
aliyowaachia Mzee Karume.
Alisisitiza kuwa Zanzibar
itabaki kuwa na Serikali madhubuti ya kidemokrasia yenye utawala wa sheria kama
ilivyoasisiwa na Mzee Karume ambaye alikuwa kiongozi mstahamilivu na ambaye
alifuata falsafa ya kuwa ustahamilivu na uvumilivu sio udhaifu bali ni sifa ya
uongozi
Alieleza kuwa mchango Mzee
Karume kwa maendeleo ya Zanzibar na Tanzania kwa jumla ni mkubwa sana na hapana
atakayethubutu kulikanusha jambo hilo yakiwemo Mapinduzi matukufu ya Januari
12, 1964 ambayo kila mmoja anafaidika.
Rais Dk. Shein alisema
kuwa miongoni mwa mambo muhimu aliyoyasisitiza Mzee Karume ni kwua Zanzibar
lazima iwe na wataalamu wazalendo wenye uwezo na ujuzi wa kutosha na wenye
kujiamini katika kupanga na kusimamia mipango ya maendeleo.
Dk. Shein aliongeza kuwa
Mzee Karume alichukia sana ubaguzi wa kidini na kusisitiza kuwa katika kumuenzi
kiongozi huyu ni vyema wananchi wakaendelea kuepuka ubaguzi wa kidini na badala
yake waendeleze upendo miongoni mwao pamoja na kuheshimiana.
Katika suala zima la
uwajibikaji na ufuatiliaji wa kazi, Dk. Shein alisema kuwa Mzee Karume
aliongoza kwa kuonesha njia na kuzikagua kazi zinazifanywa na kutoa maelekezo
ili kuongeza ufanisi kwani pia, alikuwa kiongozi wa mfano aliezingatia maadili
ya uongozi hasa katika suala la uadilifu, busara na uwajibika.
Aidha, Rais Dk. Shein
alieleza kuwa katika kutekeleza wajibu wake Mzee Karume aliongoza kwa ushauri
na ridhaa ya Baraza la Mapinduzi, jambo ambalo linaendelea kutekelezwa hadi
hivi leo ikiwa ni pamoja na kutungwa kwa Dikrii ambazo ziliendeleza utawala wa
sheria, Demokrasia, Usawa, Umoja na Maridhiano.
Alisisitiza kuwa Marehemu
Mzee Karume alionesha ushujaa katika kupinga dhuluma za aina zote walizofanyiwa
wanyonge wa Unguja na Pemba na watawala wa Kisultani na Wakoloni kwa muda wa
miaka mingi ambapo wananchi wa Zanzibar walinyimwa haki zao za maisha katika
kuendelesha maisha yao.
Dk. Shein alieleza kuwa
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kipindi cha Awamu ya Kwanza
iliyoongozwa na Mzee Karume akiwa ni Rais wa Kwanza wa Jamhuri ya Watu wa
Zanzibar pamoja na mambo mengineyo ilifanikiwa kutekeleza mambo kadhaa yaliyoelezwa
katika Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya ASP.
Miongoni mwa hayo ni
pamoja na kutangazwa kutaifishwa kwa skuli zote zilizokuwa zikiendeshwa kwa
misingi ya ubaguzi na kutangaza elimu bure mnamo Septemba 23, 1964, kutangaza
matibabu bure, kutangaza kutaifisha ardhi, kuondosha utaratibu wa kuwadhulumu
wanyonge kwa kuweka vitu vyao rahani (poni).
Jengine ni kujenga nyumba
za kisasa Unguja na Pemba mjini na vijijini, kuwajengea makaazi bora wazee na
wengine ambao hawakuweza kukaa kwenye nyumba za wazee walipatiwa posho la kila
mwezi, kuanzishwa Wizara za Serikali na kuwaeleza wananchi hali halisi ya fedha
za Serikali ilivyo kila mwaka.
Sambamba na hayo, Rais Dk.
Shein alitoa pongezi kwa Uongozi wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere kwa
kumualika pamoja na maandalizi mazuri ya Kongamano hilo lenye mada isemayo
“Mchango wa Maremu Mzee Abeid Karume katika Maendeleo ya Zanzibar”
Dk. Shein pia alitoa
zawadi kwa washindi wa Insha bora zilizoeleza juu ya Kumbukumbu ya Marehemu
Mzee Karume.
Mapema Waziri wa Nchi
Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais Mohammed
Aboud Mohammed alitoa pongezi kwa Chuo
hicho kuandaa Kongamanon hilo litakalokuwa endelevu huku akitumia fursa hiyo
kueleza kuwa juhudi za Mzee Karume yeye na wenzake zimepelekea kuwepo kwa amani
na utulivu mkubwa hapa nchini.
Waziri Aboud alitumia
fursa hiyo kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe
Magufuli pamoja na Rais Dk. Shein kwa jinsi wanavyokwenda sambamba na yale yote
yaliyoanzishwa na waasisi wa Taifa hili.
Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo
Cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere Profesa Mark Mwandosiya alieleza azma ya Chuo
hicho kuandaa kongamano hilo huko akitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa jinsi
alivyoiletea maendeleo makubwa Zanzibar kutokana na sifa zake mbali mbali za
uongozi ikiwemo uvumilivu, usikivu, ustahamilivu, usimamizi, utawala bora na
matumizi mazuri ya lugha aliyonayo Dk. Shein.
Nae Mkuu wa Chuo hicho Profesa
Shadrack Mwakalila alieleza maendeleo makubwa yaliopatikana katika chuo hicho
mara baada ya kuundwa Kampasi ya Chuo hicho hapa Zanzibar na kuanzisha masomo
ya Cheti, Shahada na Stashahada.
Profesa Mwakalila alieleza
kuwa Kongamano hilo litakuwa endelevu kwa lengo la kumuenzi Marehemu Mzee
Karume na kueleza mashirikiano makubwa yaliopo kati ya Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar na Chuo hicho huku akitumia fursa hiyo kueleza changamoto za Kampasi
ya Chuo hicho hapa Zanzibar.
Mada mbili Kuu
zimewasilishwa katika Kongamano hilo ikiwa nipamoja na mada ya ‘Fikra za Abeid
Karume katika Kujenga Umoja na Mshikamano wa Kijamii Zanzibar” iliyotolewa na
Dk. Muhammed Seif Khatib na mada ya “Fikra za Abeid Amani Karume na Mapinduzi
ya Uchumi Zanzibar”,aliyotolewa na Balozi Amina Salum Ali.
Viongozi mbali mbali wa
vyama vya siasa na Serikali walihudhuria katika Kongamano hilo.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment