Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, Azungumza na Ujumbe wa (AMT) Kutoka Dubai.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameyakaribisha Makampuni ya Privinvest na Advanced Marine Transport (AMT) kutoka nchini Dubai yanayotengeneza meli za aina mbali mbali kuja kuekeza hapa Zanzibar.

Dk. Shein ameyakaribisha Makampuni hayo wakati alipofanya mazungumzo na Mwakilishi wa Makampuni hayo Jean Boustany Ikulu mjini Zanzibar aliyefuatana na Balozi mdogo wa Tanzania nchini Dubai Ali Jabir Mwadini ambapo Mwakilishi huyo alieleza dhamira ya Makampuni hayo ya kuja kuekeza Zanzibar.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein aliyakaribisha Makampuni hayo na kueleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iko tayari kutoa ushirikiano wake mkubwa na kuweka mazingira mazuri katika kuhakikisha azma ya Makampuni hayo inatimia.

Dk. Shein alieleza kuwa azma ya Makampuni hayo imekuja wakati muwafaka ambapo Zanzibar imo katika mikakati ya kutekeleza uchumi wa bahari ambapo hatua hiyo imeonesha mwanzo mzuri kwa Zanzibar kufikia hatua hiyo.

Aidha, Dk. Shein alimuueleza Mwakilishi huyo kuwa lengo la Makampuni hayo kuja kuekeza Zanzibar itasaidia kuendeleza historia ya Zanzibar ya kuwa eneo na kituo kikuu cha biashara katika ukanda huu wa Afrika Mashariki na Kati ambapo shughuli hizo zilianza tokea miaka ya 1899 hapa Zanzibar.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iko tayari kushirikiana na Makampuni hayo na kueleza hatua itakayofuata kwa viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kukaa pamoja na uongozi wa Makampuni hayo kwa lengo la kuangalia utekelezaji wa azma hiyo.

Dk. Shein alimueleza Mwakilishi huyo kuwa kikao hicho kitasaidia kutoa mwelekeo kwa pande mbili hizo kutokana na fursa zilizopo sambamba na kuangalia ni uwekezaji wa aina gani utaanzishwa na Makampuni hayo ambayo yanauzoefu mkubwa katika utengenezaji wa meli za aina mbali mbali.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alimueleza Mwenyekiti huyo mikakati iliyowekwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuhakikisha inaanzisha Shirika lake la uvuvi hatua ambayo itaimarika zaidi baada ya uwekezaji wa Makampuni hayo hapa nchini pamoja na kuimarisha sekta ya uvuvi na kupanua soko la ajira kwa vijana.

Alieleza kuwa uwamuzi wa Makampuni hayo ni mzuri na umekuja katika wakati muwafaka ambapo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imo katika kutekeleza Sera ya Uchumi wa Viwanda, hivyo hatua hiyo itakuwa chachu katika kufikia malengo yaliyowekwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Pia, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kumueleza Mwenyekiti huyo mikakati ya mashirikiano katika sekta za maendeleo iliyofikiwa katika mazungumzo kati yake na viongozi wa nchi za Falme za Kiarabu aliokutananao katika ziara yake ya hivi karibuni aliyoifanya huko UAE.

Nae Mwenyekiti wa Makampuni ya Privinvest na Advanced Maritime Transport (ATM) Kanda ya Afrika Jean Boustany alimueleza Rais Dk. Shein jinsi Makampuni hayo yalivyovutiwa kuja kuekeza hapa Zanzibar.

Mwenyekiti huyo, alieleza kuwa Makampuni hayo yanaamini kuwa kukamilika kwa lengo lao hilo kutaipaisha Zanzibar kiuchumi sambamba na kukuza sekta za maendeleo zikiwemo uvuvi, viwanda, ajira na nyenginezo.

Juean Boustany alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa Makampuni hayo yako tayari kuja kuekeza Zanzibar na kuahidi kutoa mashirikiano makubwa kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Aliongeza kuwa Makampuni hayo yamevutiwa na mazingira mazuri ya Zanzibar hatua ambayo itakuwa chachu katika kufanikisha azma yao hiyo.

Pamoja na hayo, Mwenyekiti huyo alimueleza Rais Dk. Shein kuwa Makampuni hayo ni miongoni mwa Makampuni yanayoongoza katika utengenezaji wa vyombo vya usafiri wa baharini na uendeshaji wa Bandari na usafirishaji wa mizigo,pia yanatoa huduma kwa majeshi ya wanamaji,ukodishaji wa ndege na meli na utandazaji na uedeshaji wa miundombinu ya mafuta na gesi

Aidha, alieleza kuwa katika Bara la Afrika Makampuni hayo yanafanya shughuli zake Afrika Kusini, Angola, Cameroon, Congo, Equatorial Guinea, Ghana, Nigeria, Madagascar na Msumbiji ambapo shughuli kuu za Makampuni hayo ni kutengeneza meli za aina mbali mbali zikiwemo meli za uvuvi, ulinzi, meli za abiria, bishara na yoti (yatch).

Mwenyekiti huyo amemuhakikishia Dk. Shein kuwa Makampuni hayo yako tayari kuimarisha uhusiano na ushirikiano na Zanzibar na kusisitiza kuwa azma yao hiyo itazidi kujenga na kuuimarisha uchumi wa Zanzibar.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.