Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, Azungumza na Mabalozi na Wenyeviti wa Wilaya ya Kati Unguja leo.


MAKAMO Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza kuwa CCM inaendelea kutekeleza Ilani yake ya Uchaguzi ya mwaka 2015-2020 na kuwahakikishia wananchi kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itajenga barabara ya kisasa katika eneo la Mwanakwerekwe na daraja la kisasa katika eneo la Kibondemzungu.

Dk. Shein ambaye pia, ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi aliyasema hayo huko katika ukumbi wa Dk. Ali Mohamed Shein ulioko katika Kampasi ya Chuo Kikuu Cha Taifa Zanzbar (SUZA), Tunguu, Wilaya ya Kati, Mkoa wa Kusini Unguja wakati alipokuwa akizungumza na Mabalozi wa Wilaya ya Kati.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein aliwaeleza viongozi hao kuwa tayari Serikali imeshatenga fedha kwa ajili ya ujenzi huo katika maeneo hayo ambayo yamekuwa hayapitiki wakati wa mvua kubwa na kuleta usumbufu kwa wananchi hasa wa Mkoa wa Kusini na wale wa Wilaya ya Magharibi.

Dk. Shein alisema kuwa ujezi huo unatarajiwa kuanza mwishoni mwa mwaka huu na fedha zake tayari zimeshatengwa katika Bajeti ijayo ya mwaka 2018/2019 ili ujenzi uweze kuanza kwa haraka na kupelekea barabara hizo ziweze kupitika wakati wote.

Aliongeza kuwa tayari wataalamu wako katika mchakato wa kuangalia namna ya ujenzi utakavyotekelezwa katika maeneo yote hayo mawili ambayo yamekuwa yakileta usumbufu mkubwa kwa wananchi wkati wa kipindicha mvua hasa za masika “Serikali imeamua kujenga na pesa zipo”alisisitiza Dk. Shein.  

Aidha, Makamo Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar aliwataka Mabalozi wa Wilaya ya Kati kuyaeleza mafanikio makubwa yaliofikiwa ambayo yametekelezwa na Serikali yao chini ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Dk. Shein aliendelea kusisitiza kuwa kuanzia Bajeti ijayo ya mwaka 2018/2019 hatakiwa mzazi kuchangia ada ya mwanawe kwa skuli ya Sekondari na Msingi na Serikali imeamua kwa makusudi kutekeleza azma ya Marehemu Mzee Abeid Karume ya elimu bure.

Rais Dk. Shein aliwaeleza viongozi hao kuwa kwa upande wa sekta ya afya pia, juhudi za makusudi zimechukuliwa katika kuhakikisha huma za afya nazo zinatolewa kwa misingi hiyo hiyo huku akiwaleza kuwa maelezo kamili yatasomwa katika Bajeti za Wizara katika Baraza la Wawakilishi linalotarajiwa kuanza wiki ijayo.

Akiwaeleza wajibu wao kwa mujibu wa Katiba ya CCM, Dk. Shein aliwaeleza viongozi hao kuendelea kusimamia amani na kuongeza kasi katika suala hilo kwani CCM ndio inayosimamia amani, utulivu na mshikamano.

Alisisitiza kuwa Sera ya CCM ni amani, utulivu na msikamano hivyo CCM ni lazima ishinde ili kuendeleza amani, utulivu na mshikamano huo sambamba na kuendelea kuyaenzi na kuyatunza Mapinduzi ya Januari 12, 1964 na Muungano wake wa Tanganyika na Zanzibar.

Alisema kuwa ndani ya CCM kuna kundi moja tu, na kuwataka Mabalozi kuendelea kuwafahamisha wana CCM na kuwataka kutoruhusu wale wanaoingia ndani ya chama chao hicho kwa kutaka uongozi na baadae kutowatendea majukumu yao wananchi waliowachagua.

Pia, aliwataka viongozi wa CCM kufanya wajibu wao kwa kila aliyepewa nafasi ya kuongoza na kuwataka kufanya kazi zao kwa ufanisi mkubwa na kusisitiza kuwa Malazolizi ni vyema wakafanya kazi walizokabidhiwa na chama ikiwa ni pamoja na kutafuta ushindi wa CCM na si ushindi wa mtu mmoja mmoja.

Aliwataka kuwatafuta viongozi watakaowasaidia na kuiendeleza CCM na si wale ambao mara tu baada ya kupata uongozi wanawakimbia wananchi waliowachagua jambo ambalo alisema si sahihi hasa kwa wale viongozi wa ngazi za Ubunge na Wawakilishi ambao Mabalozi hao wanawajua.

Aidha, alisema kuwa CCM ni chama kinachopendwa katika maeneo yote duniani na kimekuwa na Mashina yake ndani na nje ya Tanzania

Alisisitiza kuwa ushindi wa CCM mwaka 2020 hauepukiki na lazima CCM ishinde kwani ni maelekezo ya chama hicho kuwa ushindi ni jambo la lazima, ushindi ambao utaletwa bila ya nguvu wala ubabe.



Sambamba na hayo, Dk. Shein alieleza kuwa uchumi wa Zanzibar umeimarika kwa kiasi kikubwa na umekuwa kutoka asilimia 6.8 kutoka mwaka 2016 hadi kufikia asilimia 7.5 mwaka 2017 pamoja na kuongezeka kwa pato la mtu binafsi kutoka TZS 1,800,000 hadi TZS 2,000,000.

Nae Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Dk. Abdalla Juma Mabodi alieleza haja kwa viongozi hao kuwa karibu na wananchi pamoja na kuwepo kwa mikutano ya viongozi na wananchi ifanyike mara kwa mara pamoja na kufanya ziara za mara kwa mara ili kupata kujua matatizo yanayowakabili.

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kusini Unguja Ramadhan Abdalla Ali (Kichupa),alitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa juhudi zake za kuendeleza na kuimarisha miradi mbali mbali ya maendeleo katika Mkoa huo ikiwa ni pamoja na barabara mpya ya Cheju- UngujaUkuu aliyoizindua katika shamrashamra za miaka 54 ya Mapinduzi.

Nao Mabalozi wa Wilaya ya Kati katika risala yao iliyosomwa na Balozi Mkombe Vuai Khamis, walitoa shukurani za dhati kwa  Rais Dk. Shein kwa kuendelea kukutana nao awamu kwa awamu hatua ambayo inadhihirisha wazi mashirikiano yaliopo kati ya viongozi wa Chama na Serikali.

Walieleza kuwa vikao vyake hivyo anavyokutana na Mabalozi ambavyo Dk. Shein alivianza tokea mwaka 2014 vimeweza kufanikisha kwa kiasi kikubwa uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 pamoja na ule wa marejeo wa tarehe 20 Machi 2016 ambapo CCM ilipata ushindi mkubwa na Wilaya yao pia, kupata ushindi kwenye nafasi zote.

Walimpongeza Rais Dk. Shein kwa utekelezaji wake wa Ilani ya Uchaguzi pamoja na uongozi wake imara, ujasiri usiyoyumba na kuweza kushuhudia maendeleo makubwa yaliopatikana katika Nyanja mbalimbali za kiuchumi, kisiasa na kijamii zikiwemo elimu, afya, umeme, maji safi na salama, miundombinu ya barabara, pencheni ya wazee kuanzia miaka 70 na nyenginezo.

 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.