Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti ya Baraza la Wawakilishi Mhe. Mohammed Said Mohammed Dimwa akisoma Majumlisho ya Mjadala wa Bajeti ya Serikali Kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019.
UTANGULIZI
Mheshimiwa
Spika, naomba nitangulize shukurani za
awali kwa Mola wetu Allah (S.W) kwa kutuwezesha kuidiriki siku ya leo katika hali
ya uzima na afya. Aidha, nimshukuru tena Mwenyezi mungu kwa kutujaalia neema ya
pekee ya kuwa miongoni mwa waliokamilisha mfungo wa Mwezi mtukufu wa Ramadhan, tunamuomba
atulipe malipo ya funga zetu, na pia atuwafikishe tuione Ramadhani ya mwakani tukiwa
wazima wa afya Amiin.
Mheshimiwa Spika, napenda pia kukushukuru wewe binafsi na wasaidizi wako Mheshimiwa Mgeni
Hassan Juma Naibu Spika wa Baraza la Wawakilishi, pamoja na Wenyeviti wa Baraza
Mheshimiwa Mwanaasha Khamis Juma na Mheshimiwa Shehe Hamad Mattar kwa namna
mnavyotuongoza katika kutekeleza majukumu ya chombo hichi kwa maslahi ya
wananchi.
Mheshimiwa
Spika, Itakumbukwa kwamba tokea tarehe 9/05/2018 Baraza la
Wawakilishi limekuwa katika mjadala wa Bajeti ya mwaka 2018/2019 ambapo bajeti
za Wizara zote 14 zimejadiliwa na kupitishwa, Mheshimiwa Spika, kwa
dhati kabisa napenda kuchukuwa fursa hii, kuwapongeza Wajumbe wote wa Baraza lako
kwa kukamilisha kazi hiyo kwa umakini na ufanisi mkubwa, kutokana na namna walivyozichambua na
kuzijadili bajeti za Wizara na kutoa maoni yao ambayo bila shaka yalilenga
kuzifanya bajeti hizo ziwe bora zaidi na zenye kuleta tija inayostahiki kwa maslahi
ya wanachi na taifa kwa ujumla, ili dhamira na malengo ya nchi yetu yaweze
kufikiwa kwa ufanisi mkubwa.
Mheshimiwa
Spika, Kanuni ya 100(2) ya Kanuni za Baraza la Wawakilishi
inaelekeza kwamba, Serikali kwa kushirikiana na Kamati ya Bajeti itafanya
majumuisho kuhusiana na hoja mbali mbali zitakazojitokeza wakati wa mjadala wa
Makadirio ya bajeti za Wizara zote. Mhesh
imiwa Spika, naomba kuliarifu Baraza lako kwamba Kamati ya Bajeti
imetimiza masharti ya Kanuni hiyo, kwa kufanya kikao cha majumuisho kwa muda wa siku mbili
tarehe 18/06/2018 na 19 /06/2018, na kufanikiwa kupitia hoja mbali mbali za
kibajeti zilizoibuliwa na Wajumbe wakati wakichangia bajeti za Wizara pamoja na
maoni ya Kamati za kisekta yaliyowasilishwa Barazani kupitia hutuba za Kamati
zao.
Mheshimiwa
Spika, napenda kuchukua fursa hii kuwashukuru sana Wajumbe
wa Kamati ya Bajeti kwa ushirikiano wao waliouonesha katika kutekeleza majukumu
ya Kamati. Aidha, napenda kuwapongeza kwa kazi kubwa waliyoifanya ya kuchukua
hoja mbali mbali za Wajumbe zilizotokana na mijadala ya bajeti, ambazo ndio msingi
wa Hotuba hii. Mheshimiwa Spika, ili kuzipa nguvu shukurani zangu naomba
kuwatambua kwa kuwataja kwa majina kama ifuatavyo;-
1. Mhe. Mohamed Said Mohamed Mwenyekiti
2. Mhe. Bahati Khamis Kombo Makamo
Mwenyekiti
3. Mhe. Simai Mohammed Said Mjumbe
4. Mhe. Zulfa Mmaka Omar Mjumbe
5. Mhe. Shehe Hamad Mattar Mjumbe
6. Mhe. Abdalla Ali Kombo Mjumbe
7. Mhe. Asha Abdalla Mussa Mjumbe
Mheshimiwa
Spika, pia napenda kuwatambuwa na kuwashukuru Makatibu wa
Kamati ya Bajeti ambao wamekuwa na msaada mkubwa kwa Kamati yangu, ambao ni
1. Ndg. Abdalla Ali Shauri
2. Ndg. Asha Said Mohamed
3. Ndg. Kassim Tafana Kassim
Mheshimiwa
Spika, Kamati ilifanya majumuisho ya Mjadala wa Bajeti ya
mwaka 2018/2019 kwa kushirikiana na Serikali, kwa kushauriana kuhusu hoja mbali
mbali za kibajeti zilizojitokeza wakati wa mijadala ili kuangalia maeneo ambayo
yanaweza kufanyiwa marekebisho au kuwekewa mazingatio maalum katika utekelezaji
wake, kwa lengo la kuongeza ufanisi wa Bajeti. Hivyo nitaiwasilisha taarifa hii ambayo ni matokeo ya mashauriano hayo baina ya Kamati
ya bajeti na Serikali kwa Baraza lako tukufu.
Mheshimiwa
Spika, Katika kukamilisha kazi ya majumuisho ya mijadala
ya Bajeti, Kamati ilikaa na Mawaziri wa Wizara zote zilizohusika na hoja ambao
pia waliambatana na watendaji wakuu wa taasisi zao, ili kuweza kusaidia
ufafanuzi wa hoja zilizoibuliwa. Aidha, kwa kuzingatia nafasi ya Wizara ya
Fedha katika mchakato mzima wa Bajeti, kikao hicho pia kilimjumuisha Waziri wa
Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Khalid Salum Mohammed, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo
Ndg. Khamis Mussa Omar pamoja na baadhi ya Watendaji wakuu wa Wizara hiyo. Kamati
inapenda kuwashukuru Mawaziri pamoja na watendaji wao wote kwa ushirikiano
mkubwa walioipatia Kamati katika kukamilisha zoezi hilo.
Mheshimiwa
Spika, Kwa kuzingatia umuhimu wa Kamati za Kisekta katika kazi
ya majumuisho ya mijadala ya bajeti, Kamati pia iliwaalika Wenyeviti wa Kamati
za Kudumu kwa lengo la kushauriana nao juu ya hoja na changamoto za kibajeti hususan
katika sekta wanazozisimamia. Kamati ya Bajeti inawashukuru sana
Wenyeviti wa Kamati kwa ushrikiano wao walioipatia Kamati kwa kutoa maoni ambayo
yamesaidia sana katika kufanikisha majukumu ya Kamati kwa ufanisi mkubwa.
Mheshimwa
Spika,
Hoja zilizojitokeza wakati wa mjadala ni
nyingi na kimsingi Kamati inazitambua zote kuwa ni muhimu. Hata hivyo, naomba
ieleweke kwamba Hotuba hii imejumuisha baadhi tu ya hoja hizo kwa kuzingatia
uhusianao wake na vifungu vya bajeti, ufafanuzi wa hoja hizo uliotolewa na
Serikali wakati wa mjadala pamoja na matokeo ya mashauriano baina ya Kamati na
Serikali kuhusu hoja hizo wakati wa kikao cha majumuisho.
MAENEO
YALIYOCHANGIWA NA WAJUMBE WENGI
Mheshimiwa
Spika, maneo ambayo yalichangiwa na Wajumbe wengi ni kama
ifuatavyo;
- Uimarishaji
wa Maslahi ya Walimu pamoja na ajira za walimu wakujitolea
- Changamoto katika Utekelezaji wa Mfumo wa Ugatuzi
- Changamoto
za Miundombinu ya Barabara
- Tatizo la
kuongezeka kwa vitendo vya Udhalilishaji wa kijinsia
- Kusuasua kwa utekelezaji wa baadhi ya miradi mikubwa ya
Maendeleo
- Umuhimu
wa kutumia mifumo ya kisasa katika kukusanya mapato
- Nidhamu
katika Matumizi ya Fedha za Serikali
- Changamoto
za kuchelewa kwa ripoti za mwaka za ukaguzi za Afisi ya Mdhibiti na Mkaguzi
Mkuu wa Hesabu za Serikali.
- Changamoto
katika Utaratibu uliopo wa kukabiliana na maafa
- Changamoto za
Huduma katika sekta ya afya
- Changamoto
za upatikanaji wa huduma ya maji
- Changamoto
za Uendeshaji wa Meli ya M.V Mapinduzi II
- Changamoto
za Biashara baina ya Zanzibar na Tanzania Bara
UFAFANUZI
WA HOJA ZILIZOTOKANA NA MAJADILIONO YA MAJUMUISHO BAINA YA SERIKALI NA KAMATI
YA BAJETI
Mheshimiwa Spika, Baada
ya maelezo hayo ya Jumla sasa naomba niingie kwenye hoja 31 kutoka katika
mafungu na Wizara tofauti ambazo zilijadiliwa
na hatimae kutolewa ushauri na Kamati kwa lengo la kuhakikisha tunapata
bajeti iliyo bora zaidi.
Mheshimiwa Spika, Naomba niwasilishe ufafanuzi wa Hoja hizo kwa njia ya Bango Kitita
ambalo limegawika Sehemu Tatu; sehemu ya kwanza inahusu Hoja za Kisekta, Sehemu
ya Pili inahusu, majibu ya Serikali na sehemu ya Tatu ni Maoni ya Kamati ya Bajeti.
Mheshiwa Spika, baada ya maelezo hayo sasa naomba niwasilishe Hoja hizo
kwa mpangilio wa Wizara kama ifuatavyo:
HOJA ZILIZOTOKANA
NA MJADALA WA BAJETI KWA MWAKA 2018/2019
|
||
HOJA
|
MAJIBU YA WIZARA
|
MAONI YA KAMATI
|
1. TUME YA UCHAGUZI: Wajumbe
walipendekeza Bajeti ya Tume ya Uchaguzi iongezwe kutokana na unyeti wa
majukumu yake, ambapo kwa mwaka wa fedha 2017/2018 ilipangiwa Tsh
bilioni1,695,500,000 na mwaka wa fedha 2018/2019 imepangiwa Tsh. bilioni
1,774,100,000. Aidha, Majengo ya Tume
ya Uchaguzi yako katika hali mbaya ikiwemo jengo la ghorofa la Wilaya ya Kaskazini “A”
ambalo miundombinu yake haiwawezeshi watu wenye ulemavu kulitumia kwa wepesi. Kwa Afisi za Wilaya ya
Kaskazini “B” kuna changamoto ya ufinyu wa ofisi kiasi cha kushindwa
kuhudumia watu watatu kwa wakati mmoja.
|
Wizara
imeiarifu Kamati kuwa bajeti iliyopangwa ya Tsh. bilioni 1,774,100,000
inatosheleza katika kutekeleza majukumu ya kuhudumia Ofisi na pia wamekiri
kuwa wamepata ongezeko la asilimia 5 ya
fedha za bajeti ya 2018/2019, kulinganisha na Bajeti ya 2017/2017 na hivyo
hakuna changamoto ya fedha. Aidha, kuhusiana na majengo ya Tume kuwa hali
mbaya, Wizara imeeleza kamati kuwa imeshaomba maeneo kwa ajili ya ujenzi wa
ofisi mpya za Tume katika Wilaya ya Kaskazini A, Wilaya ya Kaskazini B,
Wilaya ya Magharib A na Wilaya ya Magharibi B.
|
Kamati
ilikubaliana na kiwango ambacho Wizara wameridhia kupatiwa kwa kuwa wamekiri
fedha inayotolewa inatosheleza katika kutekeleza majukumu yao.
|
2.
MFUKO WA MAENDELEO YA JIMBO CDF: Wajumbe
wengi walichagia kuhusiana na Fedha chache zinazotolewa kwa ajili ya Mfuko wa
Maendeleo ya Jimbo (CDF) ambapo kwa
sasa zinatolewa jumla ya Tsh milioni 20 na imependekezwa ziongezwe Tsh
milioni tano (5).
|
Serikali
imekiri kuwa fedha zinazotolewa kwa ajili ya Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo
(CDF) katika majimbo ni chache na imeahidi kulifanyia kazi suala hili
kuhakikisha kuwa zinaongezeka kwa mujibu wa uchumi utakavyoimarika katika
bajeti zijazo.
|
Wajumbe
wamesisitiza juu ya kuongezwa kwa fedha za Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo (CDF)
kwa kuwa majimboni kuna shughuli nyingi ambazo zinatakiwa kutekelezwa na pia
kufanyiwa uchambuzi wa kina kuhusiana na fedha hizo zilivyotumika majimboni.
|
|
||
1.
IDARA YA URATIBU NA USHIRIKIANO WA KIMATAIFA NA URATIBU WA WAZANZIBARI
WANAOISHI NJE YA NCHI
Kumekuwepo
na changamoto ya baadhi ya wataalamu wa sekta mbali mbali kushindwa kushiriki
katika mikutano ya mashirikiano ya kikanda tokea hatua za awali kutokana na
ufinyu wa fedha, licha ya baadhi
Mawaziri kushiriki katika mikutano hiyo na kupelekea kushindwa kuiwakilisha Zanzibar
ipasavyo. Kwa msingi huo, Wajumbe wamependekeza Idara hii kwa bajeti ya mwaka
2018/2019 itengewe fedha za kutosha na pia zipatikane kwa wakati ili utekelezaji
wa miradi ya maendeleo inayohusu Zanzibar ipate uwakilishi wa wataalamu
tokea hatua za awali. Kwa mwaka wa
fedha 2018/2019 Idara hii imepangiwa bajeti ya Tsh 537,965,000
|
Kamati
iliarifiwa kuwa, Bajeti iliyotengewa kwa Idara hii inatosheleza kwa mujibu wa
watendaji wanaotarajiwa kusafiri kwa kuzingatia kuwa Idara hii kazi yake ni
kuratibu tu. Aidha, fedha iliyotengwa ni kwa ajili ya safari za watendaji
kama ilivyo kwa Wizara nyengine ambazo nazo kila moja ina bajeti yake kwa
shughuli za kuhudhuria mikutano ya kikanda.
|
Kamati
imeridhika na ufafanuzi wa Wizara, na kwakuwa Wizara imekiri kuwa Bajeti hiyo
inatolesheleza, Kamati imeridhia fungu hilo kubakia kama lilivyo.
|
3.
OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA,
SERIKALI ZA MITAA NA IDARA MAALUM ZA SMZ
|
||
1.
Kuhusiana na mradi wa CCTV Camera ambao kwa mwaka wa fedha 2018/2019
umetengewa Tsh bil. 20. Wajumbe walishauri kati ya fedha hizo zipunguzwe bil.
5 na zielekezwe kwenye kuimarisha barabara za ndani, mbazo bado zinauhitaji
mkubwa wa fedha ukilinganisha na uwezo halisi wa kifedha uliopo hivi sasa.
Aidha, kwa kipindi cha miaka mitatu
Wizara imepokea shilingi bilioni
4,600,000,000/- tu kwa ajili
ya uendelezaji wa barabara za ndani (Feeder road).
|
Kamati
imearifiwa kuwa, Mradi huu ni wa miaka mitano na Serikali inalazimika kulipa
kwa mujibu wa mkataba wa mradi huo. Kwa hivyo inashauriwa fedha hizo
zisipunguzwe.
Fedha
kwa ajili ya barabara za ndani zinatokana na Mfuko wa Barabara. Ambapo katika
mgao wa mfuko huo asilimia 15 zinapelekwa Halmashauri kwa ajili ya kuendeleza
bararabara za nadani. Aidha, Serikali kupitia Wizara ya Fedha na Mipango,
Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa, Serikali za Mtaa na Idara Maalum za SMZ,
pamoja na Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji zitakaa pamoja
kuangalia namna ya kuongeza asilimia ya mgao wa mapato ya Mfuko wa Barabara
kwa ajili ya kuimarisha barabara za ndani.
|
Kamati
imeridhika na Maelezo ya Wizara na imekubali fedha za Mradi wa CCTV zibakie
kama zilivyo. Aidha, Kamati imeunga mkono wazo la kuongeza mgao wa fedha za
mfuko wa Barabara kwa ajili ya kuimarisha barabara za ndani. Hivyo, Kamati ya
Bajeti inaitaka Kamati husika ya Sekta kulifuatilia suala hilo.
|
2.Wajumbe
wengi hawakuridhishwa na ufanisi wa ukusanyaji wa mapato katika masoko
ikiwemo mapato ya maegesho (parking), kulinganisha na huduma zinazopatikana
pamoja na mazingira ya masoko hayo.
|
Kamati
imearifiwa kuwa mfumo wa ukusanyaji wa Mapato unatarajiwa kuwa kwa njia ya
kielektroniki baada ya kipindi cha miezi miwili hadi mitatu. Aidha, Wizara
imekiri kwamba miundombinu katika masoko hairidhishi. Hivyo, Wizara imeahidi
kuwa itafanya maboresho baada ya kumalizika kwa kipindi cha mvua.
|
Kamati
imependekeza wananchi wapatiwe elimu
kuhusu maeneo yanayoruhusiwa na ambayo hayaruhusiwi kwa ajili ya
maegesho “parking”. Kamati pia
imeshauri kuanzishwa maeneo ya maegesho ya ghorofa ambayo yanakwenda sambamba
na ukuaji wa mji. Pia Kamati imependekeza utakapoanza mfumo wa elektroniki
kuwepo na utaratibu wa ukaguzi wa malipo ya maegesho ili kudhibiti uvujaji wa
mapato.
|
|
||
1. Katika bajeti ya
mwaka 2018/19 Mahakama imepangiwa matumizi ya uendeshaji wa ofisi shilingi
bilioni 1,515,100,000/= na Tsh bilioni
1,113,800,000 za ruzuku. Wajumbe walishauri kuongezwa kwa fedha hizo kwa kuwa
mara nyingi Mahkama imekuwa ikishindwa kuwawezesha mashahidi kuhudhuria
mahkamani na kusababisha kusuasua kwa kesi.
|
Wizara
imekiri kuwa bajeti iliyotengwa kwa mahkama kuu haitoshelezi katika
kutekeleza majukumu yake. Fedha za matumizi mengineyo (Other charges) za kila
mwezi hazitoshelezi kutokana na gharama kubwa za uendeshaji wa mahkama. Hata
hivyo, bajeti hiyo ni kwa mujibu wa ukomo “ceiling” waliyowekewa. Hivyo,
Mahkama inafanya kazi kwa mujibu wa vipaumbele vyake kulingana na fedha
walizoidhinishiwa.
|
Kutokana
na changamoto zilizopo katika Mahkama, Kamati inapendekeza Ofisi ya Rais,
Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala Bora kukaa pamoja na Wizara ya
Fedha na Mipango na kuangalia namna ya kutatua changamoto zilizopo katika
Mahkama ili kuleta utendaji ulio na ufanisi.
|
2. Kamati ya Sheria,
Utawala Bora na Idara Maalum imeshauri Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu
Uchumi (ZAECA) kupitia bajeti ya mwaka 2018/2019, ipatiwe vyombo vya usafiri
hususani Afisi za Pemba ambazo zinatumia gari moja tu kwa Mkoa wa Kusini na
Mkoa wa Kaskazini, jambo ambalo kwa kiasi kikubwa limekua likiathiri utendaji
wao na kukosa ufanisi katika maeneo yao ya kazi.
|
Wizara
imekiri ni kweli wana tatizo la usafiri ambalo linapunguza ufanisi wa
shughuli za ZAECA Pemba. ZAECA wameshindwa kuweka mpango wa ununuzi wa gari
kutokana na ukomo wa bajeti “ceiling” walio wekewa. Kwakuwa taratatibu
zinaruhusu, Wizara ya Fedha imewashauri ZAECA, ikiwa suala la gari ndio
kipaumbele chao waombe kibali kwa Katibu Mkuu Kiongozi kwa ajili ya kununua
gari kwa kuhaulisha fedha ndani ya vifungu vya bajeti yao.
|
Kamati
inapendekeza ZAECA wauchukue ushauri wa kuhaulisha vifungu vya bajeti ili
waweze kununua gari. Pia Kamati imependekeza Wizara ya Fedha iangalie
uwezekanao wa kuwapatia ZAECA gari miongoni mwa gari zilizo rejeshwa na
Taasisi nyengine.
|
3. Kamati ya PAC haikuridhishwa na
kuchelewa kwa ripoti za Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za
Serikali (CAG) ambazo zipo nyuma sana, wakati tupo katika bajeti ya mwaka
2018/2019 ndio kwanza Ofisi hii imekamilisha ukaguzi wa mwaka wa fedha
2015/2016. Aidha, Kamati ilionesha kutoridhishwa na kutoletwa Barazani Ripoti
za Ukaguzi wa Miradi na Programu za Maendeleo ambazo zingeliwasaidia Wajumbe
wa Baraza kupima ufanisi wa utekelezaji wa miradi hiyo.
|
Kamati
imearifiwa kuwa, kwa mujibu wa taratibu za ukaguzi ripoti hizo hazijachelewa
kama inavyoelezwa kwakuwa ni lazima kwanza yafanyike matumizi kabla ya
kufanywa ukaguzi na baada ya miezi mitatu ya matumizi ndio ukaguzi unapaswa
kufanyika. Aidha, Serikali imekiri ni kweli kuna mashirika hayajawasilisha
ripoti zao Barazani na kuahidi italifanyia kazi suala hilo ili Mashirika hayo
yawasilishe ripoti zao kwa mujubu wa Sheria.
|
Kamati
imeitaka Serikali ilifanyie kazi suala la ucheleweshwaji wa ripoti za CAG kwa
kuyaainisha mashirika yote yanayopaswa kuleta
ripoti zake Baraza la Wawakilishi na kuhakikisha ripoti hizo
zinawasilishwa kama ulivyo utaratibu.
Aidha,
imependekezwa pia kuwe na uwazi zaidi katika ripoti za Mdhibiti na
Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali
“CAG” ili jamii ifahamu
kinachoendelea.
|
|
||
1. Kwa mwaka wa fedha
2017/2018 Wizara ilipangiwa kukusanya jumla ya TSh. 4,344,000,000/= ambazo
zitaingia katika Mfuko Mkuu wa Serikali. Pia ilipangiwa kukusanya Sh.
3,113,600,000/= ambazo zitatumika na taasisi husika. Katika utekelezaji
halisi, Wizara ilikusanya Sh. 2,924,572,780/= sawa na asilimia 61 zilizoingia
katika Mfuko Mkuu wa Serikali. Lakini kwa upande wa makusanyo yanayobakia
katika Taasisi, Wizara ilifanikiwa kukusanya Sh. 3,515,703,680/= sawa na
asilimia 113 ya malengo kama ilivyoelezwa katika utekelezaji. Wajumbe
walihoji juu ya makusanyo yanayobakizwa kwa taasisi kuvuka malengo na
kuzorota kwa makusanyo yanayopelekwa
katika mfuko mkuu wa Serikali.
|
Wizara
imekiri ni kweli haikuvuka malengo ya makusanyo yanayoingia katika Mfuko Mkuu
wa Serikali, kutokana na kuwekewa malengo
makubwa ya makusanyo kwa bajeti ya mwaka 2017/2018 kulingana na uwezo wao wa
kukusanya. Aidha, Kutokana na historia yao ya nyuma ya ukusanyaji mapato,
shabaha waliyowekewa mwaka huu pia ni kubwa sana. Hivyo, kiuhalisia kiwango
hicho walichokusanya sio kidogo kulinganisha na uwezo wa Wizara.
|
Kamati
imeridhika na majibu ya Wizara. Aidha, Kamati inapendekeza Wajumbe
wapatiwe mafunzo kuhusu masuala ya
bajeti ili dhana ya kubakiza mapato (retention) kwa tasisi zinazokusanya mapato
ieleweke.
|
2.
Kamati ya Maendeleo, Wanawake, Habari na Utalii, haikuridhiswa na uendeshaji
wa ZBC 2 kupitia mkataba uliofungwa baina ya Shirika la Utangazaji la ZBC na Kampuni ya Azam Media LTD kwa ajili ya uendeshaji wa channel hiyo, kutokana na kutoonekana mapato yanayotokana na
matangazo ya ZBC 2 kupitia mkataba
huo.
|
Wizara
imekiri ni kweli hakukuwa na mapato yaliyopatikana kupitia Mkataba huo,
ingawaje Mkataba huo ulikuwa umejikita zaidi katika suala la mashirikiano,
kwa kuandaa na kurusha vipindi vya pamoja na kugawana mapato. Aidha, Wizara
imeiarifu Kamati kuwa mkataba wa awali umemalizika tokea tarehe 15/03/2018,
na kwa sasa wapo kwenye utaratibu wa kujadiliana kuhusu mkataba mpya. Wizara imeomba ipewe
muda ili kuhakikisha kasoro zilizojitokeza awali hazijirejei tena katika
mkataba mpya wanaojiandaa kuingia.
|
Kamati imeishauri ZBC
na Serikali kwa ujumla kuwa makini katika kusimamia mikataba ili kuhakikisha
ufanisi wa mikataba hususan katika masuala ya mapato.Aidha, Kamati imeagiza
kupatiwa kivuli cha Mkataba huo wa makubaliano baina ya ZBC na Azam Media LTD
ili ijiridhishe.
|
3. Wajumbe
wengi walichangia kuhusu umuhimu wa kuitangaza zaidi Zanzibar Kiutalii hasa
ikizingatiwa kwamba ni moja kati ya maeneo ya vipaumbele vya nchi kwa mwaka
wa fedha 2018/2019 Programu ya Utangazaji na Uhamasishaji wa Utalii
imetengewa Tsh milioni 533,145,000 tu. Aidha, Wajumbe walichangia kuhusu
kuimarisha maeneo ya kihistoria na vivutio vya ndani ambavyo iwapo
vitaimarishwa mapato ya sekta hii yataongezeka mara dufu.
|
Wizara
imekiri, ni kweli bajeti iliyotengwa kwa ajili ya kuutangaza Utalii ni ndogo,
hata hivyo, kutokana na ukomo wa bajeti “ceiling” na uwezo wa Serikali
kiwango hicho kinatosha kutekeleza majukumu waliyojiwekea. Aidha, Wizara
imesisitiza kulingana na fedha wanayopatiwa utendaji wao ni mkubwa hasa
ikizingatiwa kiwango cha watalii wanaoingia nchini kinaridhisha kulinganisha
na bajeti wanayotengewa kwa ajili ya kuutangaza Utalii.
|
Kamati imeridhika na
majibu ya Wizara na kuipongeza kutokana na kazi kubwa wanayoifanya. Hata
hivyo Kamati, imeisisitiza Wizara kuitangaza zaidi Zanzibar kupitia balozi
zilizopo nje ya nchi pamoja na kuweka taarifa muhimu zinazohusiana na Zanzibar
ambazo zinakosekana katika balozi . Kamati pia imeshauri Wizara ifanye
utafiti katika visiwa vilivyopo Zanzibar ili zijulikane rasilimali zilizopo
ambazo zinaweza kusaidia na kuwa na mchango mkubwa katika kuwavutia watalii.
|
6. WIZARA YA KAZI, UWEZESHAJI,
WAZEE, WANAWAKE NA WATOTO
|
||
1.
Wajumbe wengi walijenga hofu na kuomba ufafanuzi kuhusu fedha za Programu ya
Kukuza Maendeleo ya Wanawake na Kupinga Udhalilishaji ambayo kwa mwaka wa fedha
2018/2019 imetengewa Tsh bilion 1.7 kwakuwa inaonekana fedha hizo zimeongezeka
maradufu ukilinganisha na bajeti ya mwaka 2017/18, licha ya ukweli kwamba
vitendo vya udhalilishaji bado vinaendelea kuongezeka.
|
Kamati
imearifiwa kuwa sababu ya Bajeti ya
Fungu la Programu ya Kukuza Maendeleo ya Wanawake na Kupinga Udhalilishaji
kuwa kubwa ni kutokana na mikakati
iliyowekwa ya kupambana na vitendo vya
udhalilishaji, ikiwa ni pamoja na
kulipia malipo ya waratibu wa
vitendo vya udhalilishaji. Aidha, fungu hili linaonekana kubwa kutokana na
kuunganishwa Programu ndogo mbili, yaani Programu ya Uratibu wa Masuala ya
Usawa wa Kijinsia na Uendelezaji wa Wanawake na Programu ya Mapambano dhidi
ya Udhalilishaji wa Wanawake na Watoto. Kuhusu hoja ya kuongezeka kwa vitendo
vya udhalilishaji, Wizara imeeleza kuwa vitendo vya udhalilishaji
havijaongezeka isipokuwa kwa sasa wananchi wamehamasika kuripoti matukio ya
vitendo hivyo katika Mamlaka husika.
|
Kamati
imependekeza kwa bajeti ya mwaka 2019/2020 Wizara itoe ufafanuzi zaidi kwa
programu ambazo zimefanyiwa mabadiliko makubwa ya fedha kupitia kitabu cha
Hotuba cha Mheshimiwa Waziri ili Wajumbe wajuwe matumizi halisi ya fedha hizo
badala ya kuzichanganya.
|
2.
Wajumbe walihoji kuhusu kutofautiana kwa malengo ya utoaji wa Mikopo kwa
mwaka 2018/2019 baina ya Kitabu cha Hutuba ya Mhe. Waziri na Kitabu kikubwa
cha Bajeti ambacho Wajumbe wanaidhinisha. Katika Kitabu cha Hotuba ya
Mheshimiwa Waziri imeelezwa kuwa Wizara inatarajia kutoa Mikopo 600 lakini
kwenye Kitabu kikubwa Wizara inaonekana kupanga kutoa Mikopo 500. Aidha
kwenye utekelezaji wa mwaka 2017/2018 pia kunatofauti ya Idadi ya Mikopo
iliyotolewa baina ya Kitabu cha Hutuba na Kitabu kikubwa. Kwenye Kitabu cha
Hutuba imeripotiwa kuwa Wizara ilitoa jumla ya Mikopo 279 lakini kwenye
Kitabu kikubwa imeripotiwa kuwa Wizara ilito mikopo 300.
|
Wizara
imeeleza kuwa tofauti ya Malengo ya
Idadi ya Mikopo itakayotolewa kwa mwaka 2018/2019 ilitokana na makosa
ya kiuchapaji. Aidha, kuhusu tofauti
ya Idadi ya Mikopo iliyotolewa kwa mwaka 2017/2018 inatokana na kutofikiwa
Utekelazaji wa malengo ya mikopo hiyo.
|
Kamati
imeridhia ufafanuzi uliotolewa na Wizara juu ya utafauti wa taarifa baina ya
vitabu viwili vya bajeti. Aidha, Kamati inasisitiza kuwepo kwa umakini zaidi
wakati wa kuandaa vitabu ili makosa
kama hayo yasijirejee tena.
|
|
||
1.
Kutokana na changamoto nyingi katika sekta ya elimu ikiwemo ukosefu wa vifaa,
ubovu wa madarasa, uhaba wa walimu, uchache wa vitabu vya kusomea na vikalio,
Kamati ya Ustawi Jamii imependekeza fedha za bajeti ya Programu ya Elimu ya
Sekondari TZS bilioni 95.6 zilizotengwa kwa mwaka 2018/2019, zipatikane kwa
wakati ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi. Kwa mwaka wa fedha
2017/2018 Programu hii ilitengewa Tsh 63.5 bilioni, Hadi kufikia machi
2018 jumla ya tsh 27.4 bilioni tu
ndizo zilizopatikana sawa na asilimia 43.
|
Fedha
zilizochelewa kupatikana ni fedha za wahisani
tu, kwa upande wa fedha za SMZ za Maendeleo pamoja na fedha za
matumizi ya kawaida zote zimepatikana kwa wakati na kwa kiwango kizuri .
Aidha, changamoto mbali mbali zinazojitokeza katika sekta ya elimu zinaendelea
kufanyiwa kazi.
|
Kamati
imekubaliana na hoja bila ya marekebisho yoyote.
|
2.
Kamati ya Ustawi wa Jamii imearifu kuwepo kwa madeni ya walimu yanayotokana
na malimbikizo ya stahiki za mishahara kama vile posho za likizo, masawazisho
ya stahiki baada ya kumaliza masomo ya juu (mishahara) na posho za nauli.
Kutokan na changamoto hiyo ambayo ni ya muda mrefu. Kamati imetowa wito kwa
Wizara kuchukua hatua za kusawazisha malimbikizo hayo kwa lengo la kuongeza ufanisi
wa walimu.
|
Wizara
imearifu kwamba madeni yote ya malimbikizo ya walimu pamoja na wastaafu yameshalipwa
hadi kufikia mwaka 2016.
|
Kamati
inashauri Wizara kuendelea kulifuatilia zaidi suala la malipo ya madeni ya
walimu ili kuwaondoshea usumbufu. Kamati inasisitiza suala hilo kwakuwa bado
kuna malamiko kwa baadhi ya walimu kuhusu madeni hayo. Aidha, iweke utaratibu
mzuri ambao hautowapa usumbufu waalimu katika kufuatilia stahiki hizo.
|
3.
Wajumbe wengi wameonesha kutoridhishwa na maendeleo ya Ujenzi wa vituo vya
elimu Amali vya Daya-Mtambwe na Makunduchi. Kwakuwa kuna ongezeko la fedha
kwenye Programu ya Elimu Mbadala na Mafuzno ya Amali, ambapo kwa mwaka 2017/2018 Programu hii ilitengewa
Tsh bilioni 17.1 na kwa mwaka 2018/2019
imetengewa Tsh bilioni 24.5. Wajumbe wameitaka Wizara kuhakikisha changamoto
hii inatatuliwa ndani ya mwaka huu wa fedha, kwa kuhakikisha majengo hayo
yanendelezwa na kufikia hatua inayoridhisha.
|
Wizara
imekiri kuwepo kwa matatizo yanayohusiana na mkandarasi katika mkataba wa mwanzo
ambao umekwisha muda wake na kwasasa wamesaini mkataba mpya kwa ajili ya
utekelezaji kazi. Aidha, Wizara imeahidi kufanya jitihada ili changamoto
zilizojitokeza kwa mkandarasi wa awali zisijitokeze tena.
|
Kamati
imeishauri Wizara kuendelea kusimamia kwa karibu ujenzi wa vituo vya Elimu ya Amali na pia kuanzisha kitengo cha
majenzi katika Wizara ili kitakacho saidia kutatua baadhi ya changamoto za
miradi ya ujenzi.
|
4.Kamati
haikuridhishwa na fedha zilizotengwa katika Programu ya Ubora wa Elimu,
ambapo kwa mwaka wa fedha 2018/2019 imetengewa Tsh bilioni 7.7 tu, licha
kuwa Programu hii inahusisha taasisi
nyingi kama vile Taasisi ya Elimu Zanzibar, Baraza la Mitihani, Mrajis wa
Elimu, Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Elimu, Shirika la Huduma za Maktaba, elimu
mjumuisho, Vituo vya Mafunzo ya Walimu, TEHAMA
na michezo.
|
Wizara
imeiarifu Kamati kuwa bajeti iliyotengwa ambayo ilionekana kuwa ni ndogo ni
fedha za ruzuku kutoka Serikalini lakini pia kuna fedha nyengine za miradi
zinazochangiwa na washirika wa maendeleo.
|
Kamati
imeridhishwa na majibu ya Wizara na kupitisha hoja hii bila ya mabadiliko
yoyote.
|
8.WIZARA YA BIASHARA NA VIWANDA
|
||
1. Kamati ya Fedha, Biashara na Kilimo haikuridhishwa
na bajeti ndogo iliyotengwa kwenye Programu ndogo ya Ukuzaji Viwanda (SR010201),
ambayo kwa mwaka wa fedha 2018/2019
imetengewa jumla ya shilingi 3,665,290,000. Kiwango hicho kinaonekana ni
kikubwa ikilinganishwa na fedha zilizotengwa mwaka 2017/2018 ambazo ni
shilingi 644,987,000. Lakini kiuhalisia
fedha hizo hazitoshelezi hata kuanzisha kiwanda kimoja na kwa msingi
huo imependekezwa programu ndogo hiyo iongezewe fedha zaidi kwa nia ya kuanzisha
viwanda na kuvifanya na kuwa endelevu.
|
Wizara imekiri kuwa fedha zilizotengwa kwa Programu
ndogo ya ukuzaji viwanda (SR010201) ni ndogo na hivyo katika kipindi cha
mwaka wa fedha wa 2018/2019 imejipangia kuimarisha Taasisi ya SMIDA ambayo
imeanza kazi zake rasmi mnamo tarehe 1 Julai 2018. Aidha pia Wizara
itaimarisha maeneo tengefu ya viwanda kwa ajili ya wajasiriamali wadodo
wadogo ambao watazalisha bidhaa zitakazokuwa na viwango stahiki.
|
Wajumbe wameridhika na majibu ya Wizara na hakukuwa na
mabadiliko yeyote. Aidha, Kamati imeshauri Serikali kuwa na mkakati wa
kuendeleza maeneo tengefu yaliyotengwa pamoja na maeneo ya uwekezaji ya Micheweni,
Amani na Fumba.
|
2.
Kamati ya Fedha, Biashara na
Kilimo imeshauri kusitishwa kwa mkataba baina ya Kampuni ya Jabal Kilimanjaro
ya Dubai na Taasisi ya Viwango Zanzibar (ZBS)
inayohusiana na huduma ya ukaguzi wa magari yanayotaka kuingizwa nchini kutoka
Dubai. Mkataba huo unaeleza kuwa asilimia 70 ya mapato ya shughuli hiyo
yanaingia kwa Kampuni hiyo na asilimia 30 tu ndio inarudi kwa Serikali ya
Mapinduzi Zanzibar. Kamati imependekeza kusitishwa kwa Mkataba huo
kwakuwa Kiwango kinachoingia nchini ni
kidogo mno.
|
Wizara imekiri juu ya kuwepo kwa matatizo katika
mkataba uliofungwa baina ya Kampuni ya Jabal Kilimanjaro ya Dubai na Taasisi
ya Viwango Zanzibar (ZBS) na kuomba
kuwa mkataba huo usivunjwe kwasasa, kwa kuwa
unatarajiwa kumaliza muda mnamo 2020 na Wizara imeahidi kurekebisha
kasoro zilizojitokeza pindi watakapofunga mkataba mwengine.
|
Hoja imekubaliwa na wajumbe wa Kamati na pia kuomba
kupatiwa nakala ya mkataba uliofungwa kwa lengo la kujiridhisha. Aidha,
Kamati inasisitiza umuhimu wa kushirikishwa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu katika
kufunga mikataba ili kuepukana na mikataba isiyo na manufaa na Serikali.
|
9.WIZARA YA VIJANA UTAMADUNI
SANAA NA MICHEZO
|
||
1. Kamati ya Maendeleo ya Wanawake,
Habari na Utalii, haikuridhishwa na bajeti inayotengwa katika kuendeleza
michezo hapa nchini. Kwa msingi hu Kamati imeomba Serikali kuongeza bajeti ya
Michezo, ili kuondokana na tabia ya kuomba omba hasa pale timu zetu
zinaposhiriki mashindano ya Kimataifa.Kwa mwaka wa fedha 2018/2019 Programu
Ndogo ya Ukuzaji na uendelezaji wa Michezo imetengewa Tsh 368,400,000/-.
|
Wizara
imeiarifu Kamati kuwa imejipanga vyema kwa bajeti ya Michezo na hivyo kwa
mwaka huu wa fedha timu ya taifa itahudumiwa vizuri na kasoro zilizojitokeza
katika kipindi cha nyuma zitarekebishwa.
|
Kwa
kuwa Idara ya Michezo imetenga bajeti ya milioni 290 kwa ajili ya Timu ya Taifa,
Kamati inasisitiza fedha hizo zitumike kama zilivyokusudiwa kwa ajili ya
kuleta ufanisi katika sekta ya michezo na hivyo Kamati imeridhika na hoja
hiyo.
|
2. Kamati ya Maendeleo ya Wanawake,
Habari na Utalii haikuridhishwa na kiwango cha Bajeti iliyotengwa kwa Idara
ya Maendeleo ya Vijana, kulingana na Idadi ya Mabaraza ya Vijana yaliyopo
nchini, ambapo Kwa mwaka huu wa fedha 2018/2019 Programu ya Maendeleo ya
Viajana imepangiwa Tsh 457,448,000/ pekee.
Kamati imeshauri Bajeti hii iongezwe kwa kiwango kikubwa zaidi katika
miaka ya usoni ili Idara iweze kuendesha Mabaraza mengi zaidi pamoja na
miradi ya maendeleo inayoanzishwa kupitia mabaraza hayo pamoja na kuiwezesha
kutatua changamoto zao ikiwemo kukosa ofisi
na kupata sehemu ya kufanya vikao vyao.
|
Wizara
imeiarifu Kamati kuwa katika mwaka wa fedha wa 2017/2018 fedha walizopatiwa
Baraza la Vijana zimefikia asilimia 70, ambalo miongoni mwa majukumu ya
Baraza la Vijana ni kuratibu shuguli za vijana ikiwa ni pamoja na kutatua matatizo ya
vijana ikiwemo ukosefu wa ajira, hivyo Bajeti hiyo inatosha kwa shughuli
zilizopangwa.
|
Hoja
imekubaliwa na Kamati bila ya marekebisho yoyote.
|
10.WIZARA YA UJENZI MAWASILIANO NA USAFIRISHAJI
|
||
1.
Wajumbe wengi wamehoji kuhusu ubora wa Barabara zinazojengwa kutokana na
kuharibika mara kwa mara hususan kipindi cha mvua, ambapo ukarabati
unaofanywa kila zinapoharibika
unaigharimu Serikali fedha nyingi. Aidha, Wajumbe wamelalamikia
kuchelewa kulipiwa fidia kwa baadhi ya barabara licha ya agizo la Mhe. Rais
la kutaka barabara zote zilipiwe fidia.
|
Wizara
imeieleza Kamati kuwa kuharibika kwa barabara kunatokana na matumizi mabaya
ya barabara hizo ikiwemo kuongezeka kwa magari yenye uzito mkubwa
ukilinganisha na uwezo wa barabara na pia barabara zinazoharibika nyingi zao
zilijengwa zamani. Aidha, Wizara imejipanga kuunda Kamati Maalum ambayo
itajihusisha na usimamizi wa ujenzi wa Barabara.
Kuhusiana
na Fidia Wizara itajitahidi katika kulipa fedha hizo na kumalizia madeni
katika mwaka huu wa fedha.
|
Kamati
inaisisitiza Wizara juu ya kusimamia ujenzi wa barabara bora na imara. Aidha,
Kamati imeshauri Wizara kuwa makini katika kuingia mikataba na kamapuni
zinazojenga barabara hizo kwa kuhakikisha kuwa zinajengwa katika kiwango
stahiki.
|
2. Kamati ya Ardhi na Mawasiliano
imependekeza kuharakikisha kuifanya Karakana ya magari kuwa Mamlaka ili iweze
kuwa na maamuzi na kuimarisha utendji kazi wake, hatua ambayo itaipunguzia
Serikali gharama kutokana na hali iliyopo sasa ambapo magari mengi hupelekwa
Gereji za watu binafsi kutokana na ukosefu wa vifaa vya kutosha katika
karakana ya Serikali.
|
Wizara
kwa hatua ya awali imelekezwa na Serikali kuwa Karakana zote za Mawizara
zitaunganishwa na kuwa chini ya Karakana kuu. Aidha, kwa sasa Serikali
imeagiza kuwa gari zote za Serikali zinatakiwa kufanyiwa matengenezo katika
karakana za Serikali badala ya kupelekwa kwenye karakana za watu binafsi.
|
Kamati
inashauri kuwepo na mkakati mzuri wa kusimamia malipo ya gari za Serikali
zinapopelekwa karakana kwa ajili ya matengenezo ili kudhibiti matmizi mabaya
ya fedha.
|
11. WIZARA YA AFYA
|
||
1. Kamati ya Ustawi wa Jamii
haikuridhishwa na bajeti iliyopangiwa Programu ya Kinga na Elimu ya Afya
ambayo kwa mwaka wa fedha 2018/2019 imetengewa Tsh bilioni 19,669,126,000/-
sawa na asilimia 19.4 ya bajeti ya Wizara. Hivyo, Kamati imependekeza kwa
mwaka ujao wa fedha bajeti ya Programu hii iongezwe ili malengo
yaliyokusudiwa yaweze kutekelezwa kwa ufanisi.
|
Wizara
imeihakikishia Kamati kuwa fedha iliyotengwa kwa Programu ya Kinga na Elimu
ya Afya inatosheleza katika kutekeleza majukumu ya programu hiyo. Aidha,
programu ya Huduma ya Afya ya Msingi ambayo ilikuwa katika programu hiyo
imegatuliwa katika Halmashauri na kwa msingi huo fedha zilizopo zinatosheleza.
|
Kamati
imeridhia na ufafanuzi wa majibu ya Wizara.
|
2. Pamoja na juhudi zilizochukuliwa na
Serikali za kuongeza bajeti ya Wizara ya Afya hasa katika ununuzi wa dawa,
bado kuna changamoto kubwa ya upatikanaji wa dawa katika Hospitali na vituo
vya Afya. Kutokana na changamoto hiyo, Wajumbe wengi wamelihoji juu ya
usimamizi na utaratibu mzima unaotumika katika usambazaji wa dawa kutoka
Bohari kuu kwenda katika vituo vya Afya.
|
Wizara
imeeleza kuwa Utaratibu uliokuwepo sasa ni kwamba dawa zinapelekwa katika
kila kituo cha afya kwa mujibu wa maombi yanayopelekwa Bohari ya madawa kwa
mujibu wa mahitaji yaliyopo. Utaratibu huo unatumika kwa vituo vyote na Hospitali
kubwa kama ya Mnazi mmoja ambayo kwa kawaida huwa wanaagiza dawa mara moja au
zaidi ya mara 15 kwa mwezi. Aidha, kwa sasa bohari wanatumia mfumo wa
M-system ili kufahamu dawa zilizotoka, kiwango chake na hospitali iliyopokea dawa hizo. Lakini pia
kunatumika Mfumo wa Electronic Logistic Management Information System (eLMIS) kuagiza madawa
bohari.
Hivyo,
kuna dawa za kutosha katika Hospitali ya Mnazi Mmoja na japo kuna changamoto
ndogo ndogo, kwa sasa Serikali imefikia zaidi ya asilimia 80 ya upatikanaji
wa dawa katika mahospitali japokuwa kuna changamoto ndogo ndogo zinazoendelea
kufanyiwa kazi.
|
Kamati
imeridhika na majibu ya Wizara na pia inaitaka Kamati husika ya Kisekta
kufuatilia kwa karibu suala hili.
|
3. Kamati ya Ustawi wa Jamii
imeishauri Serikali kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Rufaa
ya Binguni kutokana na ukweli kuwa kwa bajeti iliyotengwa mwaka huu wa fedha
hazitotosha kuanza ujenzi mkubwa wa hospitali hiyo ambayo inatarajiwa kuwa ya
kisasa na yenye vifaa vingi vya gharama kubwa.Mradi huu kwa mwaka wa fedha 2018/2019 umepangiwa bajeti ya Tsh
14,000,000,000/- bilioni.
|
Fedha
zilizotengwa kwa mradi wa ujenzi wa hospitali hii ni Tsh bilioni 4, lakin pia
kumetengwa jumla ya Tsh. bilioni 15 kutoka kwa washirika wa maendeleo,
hivyo ni imani ya wizara kuwa fedha
hizo zitatosha kwa awamu ya mwamzo “phase one” ya mradi huo, Aidha Kamati Maalum
imeundwa ili kuhakiksha mradi huo unakwenda vizuri katika utekelezaji wake.
|
Kamati
imeridhika na ufafanuzi uliotolewa na Wizara na kuagiza Kamati ya kisekta
ifuatilie suala hilo zaidi.
|
12. WIZARA YA ARDHI, NYUMBA, MAJI
NA NISHATI
|
||
1.Wajumbe walihoji juu ya gharama
kubwa wanayoibeba wananchi wakati wa kuunganishiwa huduma za umeme. Pamoja na utaratibu
unaotumika wa kuunganishwa na huduma hiyo kwa mkopo kwa wale wasiokuwa na
uwezo wa kulipia gharama hizo papo kwa papo, ambapo wamelalamikia utaratibu
huo kuwa hauwapi wananchi unafuu katika kupata huduma hiyo.
|
Kamati
imeelezwa kuwa gharama wanazoingia wananchi ni gharama za mwisho za
kuunganishwa (Point of end user) hatua ambayo Shirika limefikisha miundombinu
ya umeme kuelekea eneo ambalo wananchi wanahitaji kutumia huduma hii.
Hivyo,
kwa wananchi ambao wanahitaji huduma kutoka (Point of end user), hulazimika
kuchangia gharama za kuufikisha umeme huo sehemu anayohitaji, lakini kwa
kuzingatia hali za wananchi kunakuwepo na punguzo la gharama hizo. Shirika
pia lina utaratibu wa kuwaunganishia wananchi na huduma ya umeme kwa mkopo
usiokuwa na riba kwa lengo la kuhakikisha wananchi wanapata huduma hiyo.
|
Kamati
imeshauri kuwa mkakati wa kusambaza umeme vijijini usiwe umeelekea eneo moja
tu bali uzingatie mikoa na maeneo yote kwa ufanisi zaidi. Aidha Kamati
ilisisitiza kuwa Shirika liendelee kutoa unafuu wa huduma za umeme hususan
kwa kaya maskini ambazo mara nyingi inakuwa ni vigumu kuunganishwa na huduma
hii.
|
2.Wajumbe wengi walihoji juu ya kadhia
inayowakabili watendaji wa Mamlaka ya ZAWA kulipwa mishahara ya kima cha
chini ambayo ni chini ya Tsh. 300,000 kinyume na agizo la Serikali
lililotokana na ahadi ya Mhe. Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi ambalo lilielekeza kuanza kulipa mishahara ya 300,000 kwa watendaji
wa kima cha chini. Aidha, Wajumbe walihoji juu ya kadhia ya upatikanaji wa
maji licha ya kuwa kumekuwa na miradi mingi ya maji na fedha nyingi
zinatengwa kwa ajili ya kuimarisha huduma hiyo.
|
Mamlaka
imeeleza Kamati kuwa ilishindwa kulipa mshahara wa kima cha chini cha laki
tatu kutokana na kutoongezewa ruzuku yake ya 2.5 bilioni kwa mwaka 2017/2018.
Aidha, pamoja na kuwaandikia Kamisheni ya Utumishi wa Umma mara tatu bado
hawajapatiwa muungozo wa kulipa mishahara hiyo. Kwakuwa kwa mwaka 2018/2019
ruzuku ya Mamlaka imeongezwa wanategemea kuweza kulipa mishahara hiyo, baada
ya kupata Muungozo kutoka Kamisheni ya Utumishi wa Umma pamoja na Idhini ya
Bodi ya Shirika. Kuhusu malimbikizo ya mishahara ya ZAWA kwa mwaka 2017/2018
ZAWA kwa kuwa wanapokea karibia 80 asilimia ya fedha zake kutoka Serikalini, hivyo
kwa sasa hawataoweza kulipa malimbikizo ya wafanyakazi kwa mwaka 2017/2018
Kuhusu changamoto ya maji, Mamlaka imeelezea
kuwa miradi mingi ipo katika hatua nzuri isipokua miundimbinu ya maji mingi
ni chakuvu na hivyo kupelekea upotevu mkubwa wa maji.
|
Kamati
imemuagiza Katibu Mkuu wa Wizara afuatilie suala la mishahra ya kima cha
chini kwa mujibu wa agizo la Serikali katika kamisheni ya Utumishi wa Umma.
Aidha kuhusu changamoto ya maji Kamati imemuagiza Mwenyekiti wa Kamati ya Kisekta
afuatilie miradi ya ZAWA ambayo haijakamilika
|
13. WIZARA YA KILIMO, MALIASILI,
MIFUGO NA UVUVI
|
||
1. Wajumbe
wengi walichangia juu ya kilimo cha mwani ambacho kimeajiri wanachi wengi
katika maeneo ya pwani, licha ya kukabiliwa na changamoto ya bei ambayo
haiendani na uhalisia wa ugumu wa kilimo chenyewe.Wajumbe walihitaji kufahamu
Serikali ina mipango gani ya kuimarishaa zao hilo ili kuwanufaisha wananchi
waliojiajiri kupitia sekta hiyo.
|
Wizara
imeiarifu Kamati kuwa, inashajihisha wakulima wa mwani kujihusisha zaidi na
kilimo cha mwani mnene katika kina mrefu cha bahari ambao una bei kubwa zaidi
badala ya kulima mwani mwembamba ambao una bei ndogo katika soko la dunia.
Aidha, Wizara wanashajihisha wawekezaji kuekeza viwanda vya kusarifu mwani
kwa matumizi mbali mbali na pia inatoa taaluma kwa wananchi kufanya matumizi
tofauti ya bidhaa zinazotokana na mwani ili kuongeza matumizi ya ndani ya
nchi badala ya kusafirisha mali ghafi nje ya nchi.
|
Katika
kuwahamasisha wananchi kusarifu zao la mMwani, Wizara iwawezeshe kwa
kuwapatia taaluma pamoja na vifaa vya kuweza kusarifu. Aidha, Wizara
iwafutoia wakulima wa mwani soko la uhakika ili waweze kuhamasika katika
kukiendeleza kilimo hicho.
|
14.WIZARA YA FEDHA NA MIPANGO
|
||
1. Licha ya kuwepo mahitaji makubwa ya
matengenezo ya barabara, fedha zilizotengwa kwa bajeti ya 2017/2018 kupitia
Mfuko wa Barabara zilitumika kwa kiwango kidogo sana (asilimia 26).
Changamoto kama hiyo pia ilijitokeza katika Utekelezaji wa Programu ya
Kuimarisha mambo ya Kale ambapo marekebisho ya Makumbusho ya Bihole na
Makumbusho ya Dunga hayakufanyika kutokana na kutokamilika kwa utaratibu wa
manunuzi (procurement). Changamoto
hizi za manunuzi hazileti taswira nzuri katika utekelezaji wa bajeti na pia
zinaweza kuathiri mipango ya maendeleo tunayojipangia kwa kuchelewa
kutekeleza kwa wakati miradi inayopangwa.
|
Kuhusu
changamoto iliyojitokeza ya fedha za mfuko wa barabara kutokutumika Serikali
kupitia Wizara ya Fedha na Mipango, Ofisi ya Rais, tawala za Mikoa, Serikali
za Mitaa na Idara Maalum za SMZ na Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na
Usafirishaji watakaa pamoja kuzitatua changamoto zilizojitokeza za Mfuko wa
Barabara kwa lengo la kuongeza ufanisi wa matumizi ya fedha hizo.
|
Kamati
imeridhika na ufafanuzi uliotolewa na Wizara na imeitaka Serikali kuhakikisha
kuwa changamoto hii inapatiwa ufumbuzi.
|
2. Wajumbe walitaka kupatiwa ufafanuzi
juu ya fedha za mauzo ya zao la karafuu kwa mwaka 2017/2018 yaliyofikia jumla
ya Tsh. bilioni 118.7 kwa tani 8,508.45 ambazo kimsingi zimekua hazionekani
katika mzunguko wa fedha katika mabenki hususan kwa upande wa Pemba.
|
Wizara
imeeleza kuwa itaiomba Benki Kuu ya Tanzania (BOT) kufanya utafiti utaolenga
kufaham mzunguko wa fedha za mauzo ya karafuu unavyokwenda
|
Kamati
imeridhia na majibu ya hoja. Aidha, inapendekeza suala la kufanya malipo ya
mauzo ya karafuu kwa njia ya benki yazingatiwe.
|
USHAURI WA JUMLA WA KAMATI
Mheshimiwa
Spika,
Kamati
ya Bajeti inaendelea kutoa wito kwa Afisi ya Baraza na Serikali kwa ujumla
kuzifanyia kazi changamoto za Kamati ya Bajeti ikiwemo changamoto ya kutokuwepo
Sheria ya Bajeti pamoja na Ofisi ya bajeti kwa ajili ya kuisaidia Kamati katika
utekelezaji wa majukumu yake. Mheshimiwa
Spika, uzoefu unaonesha kuwa, katika mabunge mengi Kamati ya Bajeti
inawekewa Sheria ya Bajeti ambayo inatoa Mamlaka kwa Kamati juu ya kuongeza au
kupunguza fedha katika mafungu ya bajeti kutokana na mapendekezo ya Wajumbe na
Kamati za kisekta katika mijadala ya Bajeti. Aidha mabadiliko ya Kanuni yaliyofanyika
hayajajitoshelaza katika kuipa nguvu na kuiwekea utaratibu mzuri wa kazi Kamati
hii katika kushughulikia masuala ya bajeti.
Mheshimiwa Spika,
kupitia marekebisho ya Kanuni za Baraza la Wawakilishi ya mwaka 2016, tumeanzisha
mfumo mpya wa upitishaji wa bajeti pamoja na kuunda Kamati ya Bajeti ambapo kwa
sasa bajeti kuu hupitishwa mwisho baada ya mijadala ya Wizara zote, tofauti na
ilivyokuwa awali. Hata hivyo, mabadiliko hayo hayajasaidia Wajumbe wako pamoja
na Kamati ya Bajeti kuweza kufanya mabadiliko ya vifungu baada ya Kamati ya
Matumizi kuidhinisha. Hivyo kuna kila sababu ya kujifunza zaidi ili dhamira ya
kuanzisha mfumo huu iweze kufikiwa.
Hitimisho
Mheshimiwa
Spika,
Baada ya uwasilishaji wa hoja naomba
nimalizie kwa kukushukuru tena kwa kunipatia nafasi hii ya kuwasilisha
majumuisho ya mjadala wa makadirio ya bajeti ya mwaka 2018/2019. Aidha, napenda
pia kuwashukuru wajumbe wote kwa kunisikiliza kwa utulivu na umakini.
Naomba kuwasilisha.
Ahsante,
Mohamed Said Mohamed,
Mweyekiti,
Kamati ya Bajeti,
Baraza la Wawakilishi,
Zanzibar.
No comments:
Post a Comment