WAZIRI
wa Habari, Utalii na Mambo ya Kale Mahmoud Thabit Kombo (Kushoto), akimkabidhi
kiongozi kuu wa blogi ya Zanzibar 24 Suleiman Juma Is-haka nyaraka zenye
taarifa za kihistoria na mambo ya kale kwa ajili ya kuzitangaza ili kuvutia
watalii zaidi hapa nchini. Uongozi wa Zanzibar 24 ulimtembelea Waziri huyo Juni
6, 2018 katika ratiba yake ya maadhimisho ya kutimiza miaka mitatu tangu
kuasisiwa kwa blogi hiyo.
Na
Salum Vuai, WHUMK
KUNA
umuhimu mkubwa wa kuisaidia mitandao ya kijamii zikiwemo televisheni za
kimtandao (Online TV’s) inayochipukia hivi sasa, ili ziweze kutimiza wajibu wa
kuwajuvya wananchi na dunia habari za matukio mbalimbali kwa haraka.
Akizungumza
na uongozi na wafanyakazi wa blogi ya Zanzibar 24 ofisini kwake Kikwajuni mjini
Zanzibar, Waziri wa Habari, Utalii na Mambo ya Kale Mahmoud Thabit Kombo,
amesema mitandao ya kijamii ni tegemeo kubwa sasa kutokana na uwezo wa
kuwafikia wananchi haraka hata katika simu zao za mkononi.
Uongozi
wa Zanzibar 24 ulimtembelea Waziri huyo kwa lengo la kubadilishana mawazo na
kupata ushauri chanya, ikiwa sehemu ya programu zake za kusherehekea miaka
mitatu tangu kuanzishwa kwa blogi hilo.
“Sasa
watu hawana haja ya kusubiri saa mbili usiku kusikiliza taarifa za habari
katika televisheni, kwani kukua kwa teknolojia kumerahisisha mawasiliano na
kila kitu kimo kiganjani,” alieleza.
Alifahamisha
kuwa, katika dunia ya sasa iliyojaa ushindani, haijuzu mwandishi wa habari
kuchelewa kufika kwenye matukio kwa kisingizio cha kutokuwa na usafiri bali
anapaswa kutumia maarifa na kuwa na moyo wa kujituma, vyenginevyo wenzake
watamkimbia na kumuacha nyuma.
Waziri
Kombo alisema, ni juu ya mamlaka,
taasisi za umma na binafsi pamoja na wafanyabiashara, kuitumia mitandao
na blogi za kihabari katika kutangaza shughuli zao endapo zinataka kuifikia
dunia kwa kasi na kutambulika kikamilifu.
Hata
hivyo, aliushauri uongozi wa Zanzibar 24 kuhakikisha wanamaliza mchakato wa
kujisajili rasmi wanaoendelea nao, ili kuhalalisha shughuli zake, ambazo
amesema tayari zimekubalika licha ya changamoto kadhaa zinazohitaji kufanyiwa
kazi.
“Mkifuata
taratibu, mkawafuata wakongwe wa tasnia ya habari kwa ajili ya kupata miongozo
mizuri, mna nafasi kubwa ya kupanda ngazi na kuwa mfano kama wamiliki wengine
maarufu wa blogi Tanzania na duniani kwa jumla,” alieleza.
Aidha
Waziri Kombo alisema Zanzibar ina mambo mengi yanayohitaji kuandikiwa na kutangazwa,
kazi aliyosema inaweza kufanywa vizuri na blogi za kihabari na mitandao ya
kijamii.
Alitoa
mfano wa vivutio vya kihistoria vilivyotapakaa kila pembe ya visiwa vya Unguja
na Pemba yakiwemo magofu ya kale, fukwe za kuvutia, historia za viongozi wa
dini, siasa na kijamii pamoja na rasilimali za bahari, misitu na mapango.
Aliwaahidi
viongozi hao kuwapa kila aina ya msaada ulio katika uwezo wake, kuhakikisha
blogi yao inasimama kwa miguu yake katika kipindi kifupi kijacho ili iendelee
kuwanufaisha wao na nchi yao Zanzibar na Tanzania kwa jumla.
Aliwashauri
kuunda safu ya uongozi makini utakaokuwa na muundo unaokubalika na unaokidhi
matakwa ya sheria ya uanzishaji wa vyombo vya habari na kampuni.
Mapema,
kiongozi mkuu wa Zanzibar 24 Suleiman Juma Is-haka, alisema blogi yao imepiga
hatua kubwa katika kipindi hicho kifupi, kwa kuwa kila siku inatembelewa
na wasomaji wasiopungua 10,000.
Hata
hivyo, alikiri kuwa bado wanahitaji nguvu za ziada kutoka katika mamlaka na
kampuni za biashara ili azma yao ya kuwa taasisi rasmi na kubwa iweze
kufanikiwa haraka iwezekanavyo.
Blogi
ya Zanzibar 24 imetimiza miaka mitatu Julai 7, 2018, na miongoni mwa mambo
waliyofanya katika maadhimisho hayo, ni pamoja na kukutana na Waziri wa Habari,
na kutembelea nyumba za kurekebisha tabia kwa vijana wanaoacha dawa za kulevya
(Sober Houses) iliyoko Mombasa kwa Mchina na kuwakabidhi misaada.
IMETOLEWA
NA WIZARA YA HABARI, UTALII NA MAMBO
YA KALE-ZANZIBAR
7
JULAI, 2018
No comments:
Post a Comment