JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
OFISI YA WAZIRI MKUU
Simu: +255-26-216-0161/216-0167
Mlimwa Kusini,
11 Barabara ya Edward Sokoine,
Nukushi: S. L. P. 980,
22
Julai, 2018
TAARIFA
KWA VYOMBO VYA HABARI
WAZIRI MKUU MAJALIWA AFANYA
MAZUNGUMZO YA KISERIKALI NA WAZIRI MKUU WA JAMHURI YA KOREA
*Wote wawili washuhudia uwekaji saini mkataba wa kuondoa hitaji la viza
WAZIRI MKUU Kassim
Majaliwa amefanya mazungumzo rasmi ya kiserikali na mgeni wake, Waziri Mkuu wa
Jamhuri ya Korea, Lee Nak-yon ambaye yuko hapa nchini kwa ziara ya
kikazi ya siku tatu.
Viongozi hao wawili, kwa
pamoja, leo mchana (Jumapili, Julai 22, 2018) wameshuhudia uwekaji saini
mkataba wa kuondoa hitaji la viza kwa watu wenye hati za kusafiria za
kidiplomasia na za kikazi (diplomatic and service passports).
Uwekaji saini huo
ulifanywa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Dk. Augustine
Mahiga na Makamu wa Kwanza Wizara ya Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Korea, Bw. Lim
Sung-nam kwenye ukumbi wa Kikwete, Ikulu jijini Dar es Salaam.
Akizungumza
na waandishi wa habari waliohudhuria hafla ya uwekaji saini, Waziri Mkuu
amesema kwenye mazungumzo yao wamejadiliana mambo mengi ambayo yamelenga kukuza
uhusiano wa kidiplomasia baina ya nchi hizo mbili.
“Tumejadili
namna ya kuimarisha mahusiano yetu kidiplomasia; kuimarisha ushirikiano katika sekta
ya uchumi na maendeleo; ushirikiano katika elimu, sayansi na TEHAMA ushirikiano
katika sekta ya utamaduni na utalii,” amesema.
“Pia tumeongelea fursa ya mradi
mkubwa wa reli, ujenzi wa daraja la Salender, mradi wa hospitali ya Mloganzila;
mradi wa NIDA ambao tumepata mkopo wa masharti nafuu kwa ajili ya kuendelea
kutoa vitambulisho vya uraia; ujenzi wa daraja la Kigongo - Busisi lenye urefu
wa mita 3,200; ujenzi wa barabara ya Kazirambwa – Chaya yenye urefu wa km. 42
na uimarishaji wa sekta ya afya kwa kujenga hospitali tano za rufaa kwenye kanda
zetu,” amesema.
Waziri Mkuu amesema
amewaalika makampuni ya kutoka Jamhuri ya Korea yaje kuwekeza nchini ili
kuiwezesha Tanzania kufikia azma yake ya kuwa nchi ya uchumi wa viwanda ifikapo
mwaka 2025. “Pia wafanyabiashara aliokuja nao, kesho watashiriki kongamano la kibiashara
baina ya Korea na Tanzania ili waweze kubadilishana uzoefu na wenzao wa
Tanzania.”
“Tumewaomba pia watangaze
vivutio vya utalii vya hapa nchini huko kwao na Balozi wetu wa Tanzania huko
Korea atasimamia utangazaji wa vivutio vya hapa nchini kwetu. Sisi pia
tumewapongeza kwa uamuzi wa Korea Kusini kukaa pamoja na Korea Kaskazini na
kuimarisha amani kwa nchi zao,” amesema.
Mkutano huo pia ulihudhuriwa
na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Eng. Isack Kamwele; Waziri wa
Nishati, Dk. Medard Kalemani; Waziri wa Viwanda na Biashara wa Zanzibar, Balozi
Amina Salum Ally; Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais wa Zanzibar, Bw. Issa Gavu na Naibu
Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Eng. Stella Manyanya. Wengine ni Makatibu
Wakuu wa wizara mbalimbali na wakuu wa taasisi.
Waziri Mkuu Lee Nak-yon
anatembelea Tanzania ikiwa ni hatua ya kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia
baina ya nchi hizi mbili. Hii ni mara ya kwanza kwa kiongozi wa ngazi ya juu wa
nchi hiyo kufanya ziara ya kiserikali tangu nchi hizo zianzishe mahusiano ya
kidiplomasia mwaka 1992.
Jamhuri ya
Korea ni mshirika mkubwa wa maendeleo wa Tanzania ambapo kupitia Shirika
la Kimataifa la Maendeleo (KOICA) na Mfuko wa Ushirikiano wa Uchumi na
Maendeleo (EDCF) yamekuwa yakitoa misaada na mikopo ya masharti nafuu ikiwemo
misaada ya fedha katika bajeti, ujenzi wa miundombinu ya jamii, mafunzo ya muda
mfupi na mrefu, wataalamu wa kujitolea, vifaa na mashine kwa ajili ya sekta
mbalimbali ikiwemo ya afya.
Baadhi ya
miradi ambayo imegharamiwa na Serikali ya Korea ni pamoja na Mradi wa kuboresha
Huduma ya Mama na Mtoto katika Hospitali ya Chanika, Mradi wa Mfumo wa Usajili
wa Meli na Mabaharia kwa Njia ya Mtandao Zanzibar, Mradi wa Ujenzi wa Hospitali
ya Taifa ya Taaluma na Tiba (MUHAS) kampasi ya Mloganzila na ujenzi wa daraja
katika mto Malagarasi.
Vile vile,
Korea ni mshirika mkubwa katika kusaidia maendeleo ya Bara la Afrika ambapo
hivi karibuni katika mkutano wa Sita wa Jukwaa la Ushirikiano wa Kiuchumi kati
ya Korea na Afrika (KOAFEC VI) uliofanyika Mei 2018, Busan, Korea ambapo
Serikali ya Korea ilitangaza msaada wa dola za Marekani bilioni 5 kwa ajili ya
Bara la Afrika kwa kipindi cha 2018-2020. Tanzania ni miongoni mwa nchi
zitakazonufaika na msaada huo.
(mwisho)
IMETOLEWA
NA:
OFISI YA
WAZIRI MKUU,
JUMAPILI, JULAI
22, 2018.
No comments:
Post a Comment