Habari za Punde

Dr Shein: Zanzibar ina mengi ya kujifunza kutoka Indonesia katika sekta ya uvuvi



STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Jakarta, Indonesia                         03.08.2018
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza kuwa Zanzibar ina mengi ya kujifunza kutoka Indonesia katika sekta ya uvuvi kutokana na nchi hiyo kupiga hatua na kupata mafanikio makubwa katika sekta ya uvuvi.

Dk. Shein aliyasema hayo wakati alipotembelea kiwanda cha kusarifu samaki cha Perum Perikanan kiliopo nje kidogo ya mji wa Jakarta nchini Indonesia ambacho kipo chini ya mamlaka ya Serikali ya nchi hiyo.

Katika hotuba yake fupi aliyoitoa mara baada ya kufika kiwandani hapo kabla ya kutembelea katika vitengo mbali mbali vya kiwanda hicho, Rais Dk. Shein alipongeza mafanikio makubwa yaliyopatikana katika sekta yauvuvi mchini Indonesia.

Alieleza kuwa kiwanda hicho kinaonesha jinsi ya Indonesia ilivyoweka mikakati madhubuti katika kuhakikisha sekta ya uvuvi inaimarika na kuweza kuuimarisha uchumi wa nchi hiyo pamoja na kuwanufaisha wananchi wake ambapo imekuwa chanzo kikubwa cha ajira hasa kwa vijana.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kueleza juhudi zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha sekta ya uvuvi ambapo tayari imeshaanzisha Kampuni ya Uvuvi ya (ZAFICO) kwa azma ya kuinua sekta hiyo.

Aliongeza kuwa hatua zinazoendelea hivi sasa  katika kuimarisha sekta hiyo ni pamoja na ununuzi wa vifaa na boti kwa ajili ya kuvulia pamoja na ujenzi wa bandari na hatimae kuwa na viwanda vidogo vidogo vya samaki huku akitumia fursa hiyo kuwakaribisha wawekezaji wa nchi hiyo kuja Zanzibar kuwekeza katika viwanda vya samaki.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alitoa shukurani kwa uongozi wa kiwanda hicho kwa kumualika kwenda kuona mafanikio waliyoyapata na kusisitiza haja ya kuwepo ushirikiano kwa lengo la kubadilishana uzoefu na utaalamu katika sekta ya uvuvi.

“Nakushukuruni kwa kunikaribisha vizuri kuja kuona maendeleo mliyoyafikia katika sekta hii ya uvuvi…tumejivunza mengi hasa ikizingatiwa kuwa ikiwanda hichi ni cha serikali”alisema Dk. Shein.

Katika ziara hiyo kiwandani hapo, Rais Dk. Shein alitembelea sehemu zinazosarifu aina mbali mbali za samaki ambao baadae husafirishwa  nje ya nchi na kueleza kuwa wanunuzi wakubwa wa samaki hao ni Marekani, Japan pamoja na nchi za Mashariki ya Kati.

Aidha, Rais Dk. Shein alipata kuona jinsi ya usarifishwaji wa samaki unavyofanywa kiwandani hapo na kuweza kupata maelezo kutoka kwa uongozi wa kiwanda hicho hatua ambayo pia, imeonesha jinsi vijana walio wengi ambao wameweza kupata ajira.

Nao uongozi wa kiwanda hicho ulieleza jinsi ulivyofarajika na ziara ya Dk. Shein katika kiwanda chao hicho ambacho ni kiwanda kikubwa cha samaki nchini humo ambapo uongozi huo ulieleza umuhimu wa kuwepo kwa mashirikiano katika sekta hiyo kati ya Indonesia na Zanzibar hasa ikizingatiwa kufanana kijiografia kwa pande mbili hizo.

Uiongozi huo ulitumia fursa hiyo kueleza mafanikio makubwa yaliopatikana  kwa muda mrefu tokea kuanzishwa kwa kiwanda hicho ikiwa ni pamoja na mafanikio waliyoyapata tokea kuanzishwa kwa ufugaji wa samaki.

Pia, uongozi huo ulizitaja aina za samaki wanaosariwa kiwandani hapo wakiwemo samaki wa jodari, kamba na wengineo pamoja na namna wanavyosafirishwa kwenda nje ya nchi.

Pia, uongozi huo ulieleza namna ulivyoweka mikakati katika kuhakikisha wananchi wanapata fursa kutoka katika sekta hiyo ya uvuvi kwa kutoruhusu wageni kuvua katika bahari ya nchi hiyo na kueleza namna ulivyoweka utaratibu wa kuwasaidia wavuvi wa nchi hiyo.

Wakati huo huo, Rais Dk. Shein akiwa na Mama Mwanamwema Shein na ujumbe wake alitembelea Hospitali ya Harapan Kita ambayo ni hospitali kubwa nchini humo inayotibu maradhi ya moyo na kupata fursa ya kuona vitengo mbali mbali vya vya hospitali hiyo.

Katika hotuba yake fupi hospitalini hapo, Rais Dk. Shein alitoa shukurani kwa uongozi wa hospitali hiyo kwa kumpa fursa ya kutembelea na kujionea namna ya huduma za matibabu ya moyo yanavyofanywa kwa kutumia utaalamu wa kisasa wa matibabu ya moyo kwa muda mfupi tena bila ya kufanyiwa upasuaji.

Rais Dk. Shein alisema kuwa ziara yake hiyo hospitalini hapo itasaidia kujifunza mambo mengi muhimu ambayo yatasaidia juhudi za serikali katika kukuza na kuendeleza sekta ya afya ikiwa ni pamoja na kujenga hospitali mpya ya kisasa ambayo pia itatoa mafunzo juu ya huduma za  sekta hiyoya afya.

Alieleza kwamba hivi sasa katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Tano imechukua juhudi kubwa katika kuhakikisha huduma za afya pamoja na miundombinu yake inaimarika.

Aliongeza kuwa Serikali imeendelea na juhudi zake katika kupambana na maradhi yasiyo ya kuambukiza ambayo yamekuwa yakiisumbua sana jamii.

Lakini hata hivyo, Dk. Shein alieleza kuwa bado Zanzibar inahitaji kujifunza kutoka hospitali hiyo hasa ikizingatiwa kuwa kitengo cha maradhi ya moyo katika hoapitali ya MnaziMmoja hakijawa na wataalamu wengi pamoja na vifaa vya kutosha kama ilivyo hospitali hiyo.

Dk. Shein alieleza azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha ushirikiano na hospitali hiyo hasa katika kubadilishana wataalamu, utoaji wa mafunzo na utafiti.

Nao uongozi wa Hospitali hiyo ulieleza azma yake ya kushirikiana na Zanzibar katika kupambana na maradhi ya moyo ikiwa ni pamoja na kuutumia uzoefu walionao katika kutibu na kutoa huduma kwa maradhi hayo.

Sambamba na hayo, uongozi wa hospitali hiyo ulieleza kufurahishwa kwao na ziara hiyo ya Rais Dk. Shein ambaye na yeye pia ni bingwa katika fani hiyo na udaktari na kuahidi kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta ya afya.

Mapema Rais Dk. Shein alikutana na kufanya mazungumzo na uongozi wa Benki ya Exim ya Indonesia katika ukumbi wa Hoteli ya Borobudur mjini Jakarta, ambapo uongozi huo ulieleza azma yake ya kushirikiana na Zanzibar katika kuimarisha miradi mbali mbali ya maendeleo kama ilivyofanya kwa nchi kadhaa za Afrika ikiwemo Ethiopia, Nigeria, Algeria na nyenginezo.

Nae Dk. Shein kwa upande wake aliipongeza azma ya Benki hiyo kubwa nchini humo na kueleza jinsi alivyofarajika kwa uwamuzi huo na kutumia fursa hiyo kuukarisha Zanzibar ili uje kuangalia fursa zilizopo pamoja na kushirikiana na serikali kwa kuipatia mikopo yenye masharti nafuu ili kuendeleza miradi iliyopo na inayojipangia kutekelezwa.

Akiendelea na ziara yake nchini Indonesia, Rais Dk. Shein na ujumbe wake wameelekea kisiwa cha Bali ambapo akiwa huko atapata fursa ya kukutana viongozi wakuu wa Bali pamoja na kutembelea maeneo kadhaa aliyopangiwa na wenyeji wake katika kisiwa hicho cha Bali ambacho ni maarufu kwa utalii duniani.

 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.