Habari za Punde

Kwawa wa Arctic ndege wanaosafiri masafa marefu zaidi duniani.


Na Ali Shaaban Juma

Kwawa wa Arctic ni ndege wa pwani wa jamii ya kwawa ambao kwa kiingereza huitwa Arctic Tern. Jina la kisayansi la ndege huyo ni Sterna paradisaea. Ndege hao hupatikana kwa wingi katika bahari Arctic katika pembe ya kaskazini mwa dunia kwenye baridi kali. Bahari hiyo ya Arctic ndiko linakopatikana  jimbo la Alaska huko Marekani, Canada, Greenland(Denmark), Iceland, Norway, Urusi na Sweden.

Kwawa hao ni tofauti na kwawa wanaopatikana katika pwani ya Afrika Mshariki ikiwemo visiwa vya Zanzibar. Kwawa wa Arctic ni ndege wenye ukubwa wa wastani wenye uzito wa Gramu mia moja na urefu wa Inchi 11-15 ambapo  mbawa zao zina upana wa inchi 28 hadi 30. Ndege hawa huishi kwa kula samaki wadogo na vijidudu vya baharini.  Wastani wa maisha ya ndege hao ni kati ya miaka kumi na tano hadi thelathini na nne ambapo wataalamu wa sayansi za maisha ya ndege wanakisia kuwa kuna zaidi ya Kwawa wa Arctic milioni moja.

Kwawa  wa Arctic ambao huishi jike na dume huanza kutaga akiwa na miaka minne na hurejea kutaga katika kiota chao kila mwaka. Wataalamu wa sayansi za ndege wa pwani  “Marine Ornithologists” wanasema kuwa uhusiano kati ya Kwawa jike na dume huanza kwa kwawa jike kumfukuza dume juu sana angani na baada ya hapo kwawa dume hubaka samaki na kumpa kwawa jike. Baada ya hapo kwawa jike na dume huruka na kuzunguka angani pamoja. Kisha  ndege hao hutafuta kiota na baada ya kukubaliana kuhusu kiota hicho, dume huwa ndio mlinzi wa kiota hicho. Kwa kawaida Kwawa wa Arctic hutaga kati ya yai moja hadi matatu, lakini mara nyingi hutaga mayai mawili. Jike na dume hulalia pamoja kwa zamu ambapo hutotoa baada ya siku 27 na kinda huruka siku 24 baada ya kutotolewa. Kutokana na mzunguuko mdogo wa kizazi chao, Kwawa wa Arctic ni miongoni mwa ndege wachache duniani ambao hutumia muda wao mwingi kulea watoto kidogo.

Kwawa wa Arctic ni maarufu mingoni mwa wanasayansi na wanamazingira duniani kutokana na kuwa ndio ndege pekee wanaosafiri masafa marefu kila mwaka kutoka huko Greeland eneo la Arctic kaskazini ya dunia wanakotaga  hadi eneo Weddell la bahari  Antarctic  kusini ya  dunia.

Huko Greenland ndege hao hutaga katika maeneo mengi ya visiwa vidogo vidogo vilvyo katika pwani ya nchi hiyo. Maeneo makuu ambayo ndege hao huishi na kutaga kwa wingi ni  Disko Bay, Sand Island, Upernavik na Kitsissunnguit. Kwawa wengi  hupatikana katika kisiwa cha Kitsissunnguit ambapo zaidi ya kwawa laki moja wanaishi na kutaga katika kisiwa hicho.

Kwa kawaida majira ya baridi na theluji kali upande wa kaskazini ya dunia wanakoishi kwa hao huanza mwezi wa Disemba na kumalizika Machi na majira ya kiangazi katika eneo hilo ni kati ya Juni hadi Septemba.  Tofauti na maeneo mengine ya dunia, eneo la Arctic wanakoishi kwawa hao ni lenye theluji nyingi ambapo wakati wa kiangazi baadhi ya siku jua halitui na kinyume chake wakati wa baridi kali baadhi ya siku jua halitoki.

Kutokana na mzunguko huo wa hali ya hewa, ndege hao huhama katika makaazi yao ya kawaida kaskazini ya dunia pale baridi inaponza kuanzia mwezi wa Novemba na kuhamia katika aneo la bahari ya Antarctic kusini ya dunia ambapo mara nyingi ndege hao hufikia katika kisiwa cha Farne  kilichoko huko Northumberland katika pwani ya Uingereza. Hurejea katika makaazi yao ya kudumu kaskazini ya dunia kuanzia mwezi wa Machi. Kutokana na mzunguko huo wa safari ndefu, ndege hao hutumia sehemu kubwa ya mwaka katika safari hiyo.

Kwa vile  ndege hao kusafiri masafa marefu kuliko ndege wowote duniani, kwa miaka kadhaa wanasayansi na watafiti kutoka mashirika ya mazingira, Vyuo Vikuu na taasisi nyenginezo wamekuwa wakifuatilia safari za ndege hao ili kujua ukweli wa safari za ndege hao. Katika majira ya kiangazi ya Oktoba mwaka 1982, Kwawa mmoja aliyekamatwa katika kisiwa cha Farme huko Uingereza alifungwa kipande kidogo chenye alama mguuni na baada ya miezi mitatu katika mwezi wa Disemba ndege huyo aifika pwani ya Melbourne nchini Australia. Hiyo ni safari ya kilomita 22 Elfu ya kuvuka bahari.

Utafiti mwengine ulofanywa na Carsten Egevang kutoka kituo cha utafiti cha Greenland kiitwacho “Greenland Institute  of  Natural  Resources”, umeonesha kuwa  wakati wa kurudi kaskazini ya dunia, ndege hao  hufaidika na mwendo wa upepo ambao huvuma mwelekeo wa safari yao  na hivyo kutumia nguvu kidogo katika safari yao. Katika utafiti huo ndege hao waliruka kutoka Greenland tarehe 1 Septemba 2006 na walipofika pwani ya visiwa vya Cape Verde katika bahari kuu ya Atlantiki ndege hao walijigawa makundi mawili.

Kundi moja lilikwenda hadi pwani ya Afrika Kusini na kupumzika katika eneo hilo tarehe 1 Novemba,2006 ikiwa ni miezi miwili tokea kuondoka huko Greenland. Kundi la pili lilivuka bahari kuu ya Atlantiki na kutua katika mwambao wa Amerika ya Kusini hapo tarehe 1 Novemba,2006 ikiwa ni miezi miwili baada ya kuondoka huko Greenland.  Baadae makundi yote hayo mawili yalielekea katika eneo la Weddell katika bahari Antarctic kusini ya dunia na kubaki hapo hadi kwa miezi mine. Ramani ya setelaiti ilionesha kuwa ndege hao walianza safari ya kurejea kaskazini ya dunia tarehe 1 Aprili.2007 na baada ya mwezi mmoja walipumzika katikati ya bahari kuu ya Atlantiki hapo tarehe 1 Mei 2007. Kutokana na urefu wa safari hiyo, ndege hao walifika Alaska baada ya miezi mitano na uwasili huko Greenland mwezi  Novemba 2007.

Utafiti  mwengine ulofanywa na Wanasayansi wa taasisi ya  British Antarctic Survey”  kwa kuwafunga miguuni ndege hao kifaa kidogo cha Kieletroniki cha “Geolocator”, imebainika kuwa ndege hao husafiri masafa ya maili 44 Elfu (Kilomita 71,000) kila mwaka kutoka kaskazini ya pembe ya dunia hadi kusini ya pembe ya dunia. Safari hiyo huanzia huko Greenland kaskazini ya dunia katika makaazi ya ndege hao na kuishia katika fukwe za pwani ya Weddlle kusini ya dunia wakati wa kiangazi. Kwa vile ndege hao huishi wastani wa miaka 34, safari hiyo ya kwenda kusini ya dunia na kurejea kaskazini ya dunia kila mwaka  ni sawa na safari  ya umbali wa Maili  Milioni 1.25 kwa kipindi hicho cha miaka 34 safari ambayo ni sawa na safari tatu za  kwenda mwezini!

Kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia, hapo mwaka 2013 wanasayansi  nchini Uholanzi waliwafunga miguuni Kwawa kumi na mbili vifaa vidogo vya Kieletroniki vijulikanavyo kitaalamu  kama “Geolocator tags” kifaa hicho chenye uzito wa gramu 1.5 ambao ni sawa na asilimia 3% ya uzito wa ndege huyo kiliwawezesha ndege hao kuruka kama kawaida. Kazi ya kifaa hicho kidogo cha kieletroniki chenye betri inayofanya kazi mwaka mzima amabcho kilikuwa bora zaidi kuliko vile vilivyotumiwa mwanzo ni  kurikodi nyendo za ndege hao. Vifaa hivyo viliunganisha mawasiliano kati ya Kwawa hao na Setelaiti angani ambapo setelaiti hiyo nayo kwa kupitia kompyuta ilipeleka taarifa ya ramani ya njia walimopita ndege hao katika kituo cha watafiti na hivyo moja kwa moja watafiti hao kufanikiwa kufuatilia safari yote ya ndege hao bila kupoteza hata  sekunde moja ya mawasiliano. Utafiti huo ulionesha kuwa ndege hao walisafiri masafa marefu zaidi kuliko ilivyokadiriwa na tafiti zilizofanywa hapo awali na wanasayansi wengine.

Ramani iliyotumwa na setelaiti ilionesha kuwa Kwawa hao walisafiri umbali wa Kilomita 90,000 (Maili 56 Elfu). Ramani  hiyo ilionesha kuwa katika safari yao ya kuelekea kusini ya dunia, ndege hao walipita katika mwambao wa bahari kuu ya Atlankiti pembeni ya bara Ulaya na Afrika Magharibi. Baada ya kupinda katika pembe ya bahari ya Afrika ya Kusini, Kwawa hao waliingia katika bahari kuu ya Hindi (Indiani Ocean) ambapo baadhi ya ndege hao walielekea upande wa Australia na kisha kugeuza na kuelekea upande wa kusini mwa bahari kuu ya Hindi  na kutua katika kisiwa cha Wilkesland kaskazini mashariki mwa bahari ya Antarctic.

Ramani hiyo ilimuonesha ndege mmoja ambaye alisafiri kilomita mia kadhaa kusini mwa mwambao wa  Australia na kisha kuelekea upande wa kusini katika bahari ya Antarctic, ambapo ndege mwengine alisafiri kupitia eneo lote la mwambao wa pwani ya Australia kati ya bara hilo na kisiwa cha Tasmania hadi pwani ya mjini Melbourne nchini Australi.  Baada ya kuruka kutoka pwani ya Melbourne, Kwawa huyo alielekea upande wa kusini katika bahari ya kisiwa cha Wilkesland kaskazini mashariki ya bahari ya Antartic kupitia kisiwa kidogo kiitwacho “South island” kulichoko kusini magharibi mwa New Zealand hadi nchini Uholanzi  nchi ambayo ndege huyo aliondokea. Taarifa za setelaiti zilionesha kuwa safari ya ndege huyo ilikuwa ni Kilomita 91,000 (Maili 57 Elfu) ambayo ndiyo safari ndefu kabisa ya kiumbe kurikodiwa. Kumbukumbu zilionesha kuwa safari ya ndege hao kuelekea kusini ya dunia ilichukua siku tisiini na tatu ambapo ndege hao walisafiri kwa kasi ya kilomita 330 kwa siku. Hata hivyo kutokana na kusukumwa na upepo, safari ya kurejea kaskazini ya dunia ilikuwa ni nyepesi kwani ndege hao walitumia siku Arobaini na kusafiri kwa kasi ya Kilomita 670 kwa siku. Ndege hao hutua kwa zaidi ya mwezi mmoja katikati ya eneo la kaskazini mwa bahari ya Atlantiki kwenye samaki wengi ili kupumzika na kula.
Kwawa  wa Arctic aliyefungwa mguuni kifaa kiitwacho geo- locator akirejea katika maskani yake ya kutaga katika kisiwa kidogo  kiitwacho Sand Island huko kaskazini mashariki ya Greenland hapo mwaka 2007 baada ya kumaliza safari ya mzunguuko wa Kilomita 70,000 iliyoanzia kisiwani hapo mwezi Novemba, 2006.

Mwandishi wa makala haya ni Mwalimu wa Chuo cha Uandishi wa Habari cha ZJMMC, Kilimani mjini Zanzibar.
E-Mail: Rafikifumba1@hotmail.com

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.