Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, Azungumza na Spika na Uongozi wa Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Ikulu leo.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amelipongeza Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya uongozi wa Spika wa Bunge hilo Job Ndugai kwa kutekeleza vyema kazi zake ikiwa ni pamoja na kuwawakilisha vyema wananchi.

Dk. Shein aliyasema hayo leo wakati alipokuwa na mazungumzo na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Ndugai aliyefika Ikulu Mjini Zanzibar akiwa pamoja na  viongozi wa Kamati ya uongozi wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein alieleza kuvutiwa kwake na uongozi mzuri wa Spika wa Bunge hilo hali inayoonesha kuwa Bunge hilo limepata maendeleo makubwa katika kuwawakilisha wananchi.

Alieleza kuwa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limeweza kupata mafanikio makubwa kutokana na kuwa na uongozi makini sambamba na kuwepo Wabunge wenye ari na moyo wakuwatumikia wananchi waliowachagua.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa kasi ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika mijadala yake ni kubwa na inaonesha jinsi Wabunge walivyokuwa na ari ya kuwaletea maendeleo wananchi.

Kutokana na juhudi hizo, Rais Dk. Shein aliwataka Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuendelea kulitumikia vyema Bunge hilo kwa manufaa na maslahi ya nchi na wananchi wote wa Tanzania kwani anaamini kuwa Tanzania itajengwa na Watanzania wenyewe.

Aliongeza kuwa licha ya kuwepo baadhi ya changamoto ndogo ndogo lakini bado Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limekuwa likifanya kazi zake kwa ufanisi ukubwa na kuleta matumaini makubwa kwa wananchi kwa kuyatetea maslahi yao.

Alieleza kuwa kutokea kwa baadhi ya changamoto ndani ya Bunge kwa baadhi ya wakati kunatokana na uhalisia wa Bunge kwani Mabunge yote duniani yamekuwa yakikabiliwa na changamoto kadhaa, ambapo kwa  Bunge la Tanzania hutokea kama yalivyo Mabunge mengine na hatia hupatiwa ufumbuzi kutokana na uongozi makini uliopo.

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza kuwa kwa upande wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar nalo kwa upande wake limekuwa likifanya kazi vyema na kwa ari kubwa kutokana na Wajumbe wake kuwa makini na kuwa na uwelewa na utambuzi mkubwa wa mambo.

Kwa upande wa maendeleo ya kiuchumi yaliofikiwa katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais Dk. Shein alisema kuwa Tanzania iko vizuri kutokana na uchumi wake kukua kwa haraka ikilinganishwa na nchi nyengine za bara la Afrika hivyo ipo haja ya kuendelea kuongeza kasi kwa mashirikiano ya pamoja.

Alieleza kwa upande wa Tanzania Bara maendeleo yaliofikiwa leo sio yale yaliokuwa mwaka 1961 na kwa Zanzibar hatua za maendeleo zilizofikiwa haiwezi kulinganishwa na ilivyokuwa mwaka 1964 ambapo Zanzibar ilipata uhuru wake.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alieleza kuwa uchumi wa Zanzibar nao kwa upande wake umekuwa ukiimarika siku hadi siku kutokana na juhudi kubwa zinazochukuliwa na uongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kulisimamia hilo.

Akieleza kuhusu suala zima la amani, utulivu na usalama, Rais Dk. Shein alimueleza Spika huyo wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Ujumbe wake kuwa Zanzibar iko salama.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alisisitiza kuwa akiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ataendelea kuiongoza vyema Zanzibar na watu wake wote bila ya ubaguzi wa aina yoyote.

Nae Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Ndugai alimueleza Rais Dk. Shein madhumuni makubwa ya uwepo wa viongozi wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hapa Zanzibar.

Spika Ndugai alimueleza Rais Dk. Shein kuwa viongozi wa Bunge hilo wapo Zanzibar kwa mafunzo maalum ya siku mbili yanayowahusisha wajumbe wa Kamati ya uongozi, makamu wenyeviti na wajumbe wa Tume ya Bunge yaliyoanza jana na kumalizika hivi leo huko katika ukumbi wa Ofisi ndogo za Bunge ziliozpo Tunguu, Mkoa wa Kusini Unguja.

Alieleza kuwa katika mafunzo hayo pia, wamewahusisha Spika wastaafu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Zanzibar kwa lengo la kuchota busara, maarifa, uzoefu na umakini mkubwa wa ungozi wa Mabunge kutoka kwa viongozi hao.
Spika huyo wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amesifu amani, utulivu na usalama mkubwa uliopo Zanzibar na kupongeza hatua na juhudi kubwa zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Rais Dk. Shein katika kuendelea kuiletea maendeleo Zanzibar na watu wake.

Pia, Spika huyo wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amesifu hatua zilizochukuliwa katika ujenzi wa hoteli za kisasa katika mji wa Zanzibar ambazo zimekuwa kivutio kikubwa kwa wageni na wenyeji wa Zanzibar ikiwemo hoteli mpya ya  kisasa ya Verde.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.