Habari za Punde

Azma ya Marehemu Mzee Abeid Amani Karume Kutangaza Elimu Bure Kwa Watoto wa Zanzibar Bila ya Ubaguzi Ikiwa ni Ilani ya ASP.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (katikati) alipokuwa akitoa hutuba yake kwa Wananchi na Wanafunzi   katika sherehe ya  uwekaji wa   jiwe la msingi ujenzi wa Skuli mpya Sekondari ya Kinuni Jimbo la Pangawe Wilaya ya Magharibi"B" Mkoa wa Mjini Magharibi,sherehe zilizofanyika leo sambamba na Skuli 9 za Sekondari za Zanzibar,(kulia) Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Mhe.Riziki Pembe Juma(kushoto)Waziri Kiomgozi Mstaafu na Mbunge wa Jimbo la Kijito Upele Mhe.Shamsi Vuai Nahodha na Naibu katibu Mkuu CCM Zanzibar Dk.Juma Abdala Sadala(wa pili kushoto),[Picha na Ikulu.] 21/09/2018. 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa azma ya Marehemu Mzee Abeid Amani Karume kutangaza elimu bure kwa watoto wa Zanzibar bila ubaguzi ilikuwa ni utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya Chama Cha ASP ambayo inaendelea kutekelezwa hadi hivi leo.
Dk. Shein aliyasema hayo leo katika hafla ya uwekaji mawe ya Msingi ya Skuli 9 za ghorofa Unguja na Pemba ambapo kwa niaba ya skuli hizo aliweka jiwe la msingi skuli ya Kinuni, Mkoa wa Mjini Magharibi ikiwa ni kati ya skuli hizo mpya hatua ambayo ni miongoni mwa shamrashamra za kusherehekea miaka 54 ya Elimu bure ambapo kilele chake ni Septemba 23 mwaka huu.
Rais Dk. Shein alisema kuwa utekelezaji huo unaendelea kutoka kwa chama cha ASP na hivi sasa CCM ambapo ujenzi wa skuli hizo ni utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM kwani hayo ni mambo yaliopangwa na Chama hicho.
“Nilipoiona skuli hii mpya niliona kweli kinu kimejaa hapana hata mmoja kati yetu aliyekuwa na wazo kuwa Kinuni kutakuwa na skuli kama hii, lazima tushuruku neema hizi kwani tukishukuru Mwenyezi Mungu atatuongezea”, alisema Dk. Shein.
Aidha, Rais Dk. Shein alisema kuwa kutangazwa kwa elimu bure kulikuwa na maana kubwa katika kutekeleza Mapinduzi ya Januari 12, 1964 na kusisitiza kuwa elimu bure msingi wake ni kuondoa ubaguzi katika kuwapa elimu watoto wa Zanzibar kwani watoto wa kinyonge walikuwa hawapati elimu inayopaswa kwani walidhulumiwa kupata haki yao hiyo ya msingi.
Dk. Shein alisema kuwa elimu ndio msingi wa mwanzo wa maendeleo na maisha ya mwanaadamu duniani hivyo ndio maana Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeipa kipaumbele sekta hiyo na matokeo ya mafanikio yanayopatikana hivi sasa katika sekta za maendeleo ikiwemo sekta ya elimu yanayotokana na Mapinduzi ya Januari 12, 1964 ambayo Zanzibar inajivunia hadi hii leo.
Alieleza kuwa akiwa Rais wa Zanzibar anajivunia kuendelea kutoa elimu bure kwani Mzee Karume aliamua chini ya ASP na awamu ya Saba itaendeleza chini ya uongozi wa CCM na kusisitiza kuwa kuwa kasi ya Zanzibar ni kasi ya maendeleo katika kutoa elimu bora, na kuipanua elimu kwa mahitaji ya sasa na ya hapo baadae na.
Akieleza juhudi zinazochukuliwa katika kutatua changamoto kwenye sekta za elimu, Dk. Shein alieleza kuwa hivi karibuni madawati yapatayo 22,000 yatawasili kutoka nchini China na mengine yatafuata hapo baadae huku akieleza changamoto ya ukosefu wa walimu wa sayanasi ambapo Serikali kupitia vyuo vyake vikuu vilivyopo nchini kikiwemo chuo cha SUZA vinasomesha kada hiyo.
Hivi sasa Zanzibar inasomesha wataalamu wake wenyewe ili kuweza kutoa mafunzo hasa katika masomo ya sayansi. “Leo tumeandika historia potelea mbali wanaonuna na wanune lakini tushajenga na watoto wetu watasoma, watapata elimu itakayowasaidia leo, kesho hadi mtondogoo”, alisisitiza Dk. Shein.
Alisema kuwa utekelezaji huo ni mpango uliopangwa mnamo mwaka 2014 wa skuli 10 ambapo moja ya skuli hizo ni ya Mwembeshauri ambayo ni skuli mbili kwa pamoja ambapo Serikali imekopa pesa  kutoka ‘OPEC Fund” ili kuwaendeleza watoto wa Zanzibar kupata elimu kwa azma ya kuja kuwaendesha wao na wazee wao.
Rais Dk. Shein alieleza kuwa Serikali itaiendeleza Kinuni kutokana na eneo hilo kukua kwa idadi ya watu pamoja na makaazi yao.
Alitumia fursa hiyo kutoa agizo kwa Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji kwa kushirikiana na Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa   na Idara Maalum za SMZ kuhakikisha kuwa mwezi Septemba mwakani iwe imekamilisha ujenzi wa barabara ya Kinuni kwa kiwango cha lami ili wananchi wakiwemo wanafunzi waweze kupita bila usumbufu.
Rais Dk. Shein alisisitiza utekelezaji wa mipango ya ardhi katika kupanga majengo ya wananchi pamoja na miundombinu mengine na ndio maana Serikali imeanza kujenga majengo ya ghorofa kwa lengo la kutumia ardhi ndogo.
Alieleza kuwa pale Serikali inapotangaza wananchi wake wasivamie ardhi wawe wasikifu kwani ardhi ya Zanzibar ni ndogo na wananchi wake ni wengi kwani Zanzibar ina idadi ya watu wanaokadiriwa kufikia milioni 1.5 wakati mpaka panafanyika Mapinduzi ya Januari 12, 1964 Zanzibar ilikuwa na idadi ya wananchi 320,000 tu.
Rais Dk. Shein alieleza kuwa elimu ya Msingi na Sekondari itaendelea kutolewa bure na kwa wale watakaowalipisha watoto wa skuli za Msingi hatua kali za kisheria zitachukuliwa zidi yao huku akitumia fursa hiyo kuahidi kupelekwa walimu wa Sayansi katika skuli hiyo.
Sambamba na hayo, Dk. Shein aliwataka wananchi kuishi kwa amani, utumiliu na upendo na kuongeza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inafanya kazi ya kuwapelekea maendeleo wananchi wote wa Zanzibar bila ya ubaguzi kwa lengo la kufaidi matunda ya Mapinduzi.
Nae Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Riziki Pembe Juma alitumia fursa hiyo kumpongeza Rais Dk. Shein kutokana na Serikali anayoiongoza kutekeleza ahadi zake kwa vitendo ikiwa ni miongoni mwa utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM.
Waziri Pembe alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa Wizara yake itahakikisha inatoa elimu iliyo bora na yenye viwango huku akiahidi kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa kwa yule atakayekwenda kinyume na taratibu zilizowekwa.
Alitoa pongezi kwa Kampuni ya kizalendo ya Saleem Construction LMT (SALCON) kwa uzalendo mkubwa ulioufanya wa kusaidia ujenzi wa madarasa manne iliyoyajenga pembezoni mwa skuli hiyo mpya.
Mapema Katibu Mkuu Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Dk. Idrissa Muslim Hija alisema kuwa ujenzi wa skuli hiyo mpya ya Sekondari ya Kinuni ni miongoni mwa skuli tisa zinazojengwa Unguja na Pemba ambapo kati ya hizo tano zinajengwa Unguja na nne zinajengwa Pemba.
Akizitaja zinazojengwa Unguja kuwa ni Kinuni, Mwembeshauri, Chumbuni, Bububu na Fuoni na Pemba ni Wara, Mwambe, Kizimbani na Micheweni ambapo ujenzi huo unatekelezwa kwa mashirikiano makubwa kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na wahisani “Opec Fund for International Development” (OFID) kupitia mradi wa Zanzibar “Third Education Project” (ZATEP).
Alisema kuwa skuli hiyo na nyengine zinazojengwa zitasaidia sana kupunguza msongamano wa wanafunzi darasani na kuweka mazingira mazuri ya kujifunza kwa watoto na hatimaye waweze kufanya vizuri katika mitihani yao hasa ikizingatiwa kuwa watoto wanaosoma skuli ya Msingi ya Kinuni pekee wanapindukia 5017.
Aliongeza kuwa jumla ya Dola za Kimarekani milioni 10.2 za mkopo kutoka “OPEC Fund” zitatumika katika utekelezaji wa mradi na Serikali itachangia asilimia 11.17 ya gharama ya ujenzi kwa mujibu wa mkataba wa makubaliano hayo.
Katibu Mkuu huyo alieleza kuwa Skuli mpya ya Sekondari ya Kinuni ni ya ghorofa moja itakayokuwa na madarasa 14, maabara 3, maktaba 1, chumba cha compyuta, ukumbi mkubwa, ofisi za walimu pamoja na miundombinu kwa ajili ya wenye mahitaji maalum.
Alieleza kuwa ujenzi huo umesanifiwa na unasimamiwa na Mshauri Muelekezi OGM CO. LTD ya Dar-es-Salaam Tanzania na ujenzi unafanywa na Mkandarasi Saleem Construction LMT (SALCON) kutoka Zanzibar ambapo ujenzi ulianza mwezi Oktoba mwaka 2017 na utakamilika mwezi Januari 2019.
Dk. Hijja, alitumia fursa hiyo kuwaomba wazee, wanafunzi na jamii yote kwa ujumla inayozunguka mazingira ya skuli hiyo kuendelea kushirikiana katika kutunza majengo ya skuli hiyo na rasilimali zake zote kwa faida ya vizazi vilivyopo na vijavyo.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.