RAIS
wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein,
amemtumia salamu za rambirambi Mkuu wa Mkoa wa Mwanza John Mongela kufuatia
ajali ya kuzama kwa kivuko cha MV. Nyerere iliyotokea katika Ziwa Victoria Mkoa
wa Mwanza na kusababisha vifo pamoja na majeruhi.
Dk.
Shein alieleza kuwa amepokea kwa mshtuko na huzuni kubwa taarifa ya ajali ya kuzama
kivuko hicho na kueleza kuwa yeye binafsi pamoja na wananchi wote wa Zanzibar
na Tanzania nzima kwa jumla wamegubikwa na simanzi nzito kufuatia msiba huo
mkubwa wa kitaifa.
“Kwa
hakika msiba huu umetugusa Watanzania sote, ni msiba wetu kwa sababu waliofikwa
na janga hili ni ndugu zetu, Watanzania wenzetu”, ilieleza sehemu ya salamu
hizo za rambirambi alizozituma Dk. Shein.
Aidha,
Rais Dk. Shein alisema kuwa kwa vile ajali ni moja kati ya matukio ambayo
mwanaadamu hana budi nayo alimuomba Mwenyezi Mungu azijaalie roho za wale wote
waliopoteza maisha zipumzike mahala pema.
Kwa
wale ambao kwa nguvu za Mola Muumba wameweza kuokolewa wakiwa hai, alimuomba
Mwenyezi Mungu awape nafuu kutokana na msukosuko mkubwa uliowapata ili waweze
kurudi katika hali zao za kawaida kiafya na waendelee na shughuli zao za kila
siku za kujenga nchi yao.
Pamoja
na hayo, Rais Dk. Shein alieleza kuwa wananchi wote wa Tanzania Zanzibar
wanaungana na Mkuu wa Mkoa huo, Uongozi wa TEMESA, ndugu jamaa na marafiki wa
marehemu na wanusurika wa ajali hiyo katika huzuni kubwa za msiba huo.
“Watanzania
tunatakiwa kuendelea kuwa na utulivu, umoja na mshikamano wakati huu ambapo
jitihada za kutafuta miili zaidi ya waliopata ajali hiyo zikiendelea”,alieleza
Dk. Shein katika taarifa hiyo.
Sambamba
na hayo, Rais Dk. Shein aliwataka Watanzania kuendelea kuwa na ustahamilivu
wakati huu ambapo uchunguzi wa sababu za tukio hilo ukifanyika na bila shaka
taarifa kamili zitatolewa hapo baadae.
Rais
Dk. Shein alimuomba Mwenyezi Mungu awape Watanzania wote na wanafamilia nyoyo
za subira na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu cha msiba.
Ajali
ya kuzama kwa kivuko hicho ilitokea katika Ziwa Victoria katika eneo la Ukerewe
wakati kilipokuwa katika safari yake ya kutoka Bugorola kwenda kisiwa cha Ukara
saa sita mchana hapo jana.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024
2231822
E-mail:
rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment