Habari za Punde

TANZANIA YA YAIBAKIDHI SEYCHELLES UONGOZI WA MAPAMBANO DHIDI YA UTAKASISHAJI FEDHA HARAMU NA UFADHILI WA UGAIDI MASHARIKI NA KUSINI MWA AFRIKA

Makamu wa Rais wa Seychelles, Mhe. Vincent Meriton, akifungua Mkutano wa 18 wa Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Udhibiti wa Fedha Haramu wa Nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika (ESAAMLG), mjini Mahe, Seychelles ambapo nchi hiyo imekabidhiwa kijiti cha kuongoza Umoja huo kwa mwaka mmoja (2018/2019) ukiwa ni utaratibu wa nchi wanachama kukabidhiana uongozi kwa kipindi cha mwaka mmoja mmoja
Mwenyekiti wa  Umoja wa Udhibiti wa Fedha Haramu wa Nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika (ESAAMLG), aliyemaliza muda wake, Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb), (kulia), akiwa Meza Kuu na Mwenyekiti mpya wa umoja huo, Waziri wa Fedha, Biashara, Uwekezaji na Mipango ya Kiuchumi wa Seychelles, Balozi Maurice Lousteau – Lalanne, wakati wa mkutano wa 18 wa Umoja huo uliofanyika, Mahe-Seychelles.
Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha na Mipango, Bi. Susana Mkapa (kushoto) na Mhasibu Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi, Zanzibar, Bi. Mwanahija Almas Ali, wakifuatilia kwa makini Mkutano wa 18 wa Baraza la Mawaziri wa  Umoja wa Udhibiti wa Fedha Haramu wa Nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika (ESAAMLG) uliofanyika Mahe, Nchini Seychelles.
 Baadhi ya wajumbe kutoka nchi zaidi ya 19 za Afrika, wakifuatilia kwa makini Mkutano wa 18 wa Baraza la Mawaziri la  Umoja wa Udhibiti wa Fedha Haramu wa Nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika (ESAAMLG) uliofanyika Mahe, Nchini Seychelles, ambapo Tanzania imeikabidhi Seychelles uongozi wa Umoja huo kwa kipindi cha mwaka mmoja ukiwa ni utaratibu wa nchi wanachama kupokezana uongozi.
Rais wa Seychelles Mhe. Danny Faure (katikati), akimsikiliza kwa makini Mwenyekiti wa  Umoja wa Udhibiti wa Fedha Haramu wa Nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika (ESAAMLG), aliyemaliza muda wake, Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb), (hayupo pichani), wakati akitoa hotuba ya kukabidhi uongozi wa Umoja huo kwa nchi ya Seychelles.
 Katibu wa Waziri wa Fedha na Mipango, Bw. Edwin Makamba, na Meneja Idara ya Uhusiano wa Umma na Itifaki wa Benki Kuu ya Tanzania -BOT, Zalia Mbeo, akifuatiwa na Bi. Tausi Abdallah, Mwanasheria BOT, wakifuatilia matukio mbalimbali ya Mkutano wa 18 wa Baraza la Mawaziri wa  Umoja wa Udhibiti wa Fedha Haramu wa Nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika (ESAAMLG) uliofanyika Mahe, Nchini Seychelles
 Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb) (katikati) akiwa na Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania BOT, Dkt. Bernard Kibesse (kushoto), na Katibu Mkuu Wizara ya Sheria na Katiba, Profesa Sifuni Mchome (kulia), wakati wa Mkutano wa 18  Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Udhibiti wa Fedha Haramu wa Nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika (ESAAMLG).
Makamu wa Rais wa Seychelles, Mhe. Vincent Meriton, akifungua Mkutano wa 18 wa Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Udhibiti wa Fedha Haramu wa Nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika (ESAAMLG), mjini Mahe, Seychelles ambapo nchi hiyo imekabidhiwa kijiti cha kuongoza Umoja huo kwa mwaka mmoja (2018/2019) ukiwa ni utaratibu wa nchi wanachama kukabidhiana uongozi kwa kipindi cha mwaka mmoja mmoja
(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini-Wizara ya Fedha na Mipango, Seychelles)


Na Benny Mwaipaja, WFM, Mahe, Seychelles
TANZANIA imekabidhi uongozi wa mwaka mmoja wa Umoja wa Udhibiti wa Fedha Haramu wa Nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika (ESAAMLG) kwa nchi ya Seychelles, huku ikijivunia mafanikio makubwa ya kuhakikisha kuwa nchi wanachama wa umoja huo zinakuwa na sera, sheria, taasisi na mifumo imara inayowezesha mapambano dhidi ya vitendo vya utakasishaji fedha haramu na  ufadhili wa ugaidi.

Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, amekabidhi uongozi huo kwa niaba ya Serikali ya Tanzania kwa Waziri wa Fedha, Biashara, Uwekezaji na Mipango ya Kiuchumi wa Seychelles Balozi Maurice Lousteau – Lalanne, wakati wa Mkutano wa 18 wa Baraza la Mawaziri wa Umoja huo, uliofanyika Mjini Mahe, nchini Seychelles na kushuhudiwa na Rais wa Nchi hiyo, Mhe. Danny Faure.

Miongoni mwa mafanikio yaliyofikiwa katika kipindi hicho cha mwaka mmoja, ni kufanyika kwa tathimini ya mifumo ya kudhibiti utakasishaji wa fedha haramu na ufadhili wa ugaidi wa nchi tatu wanachama wa umoja huo za Mauritius, Madagascar na Seychelles, na kwamba zoezi la kuzitathmini nchi nyingine mbili za Zambia na Malawi, linaendelea.

"Rasilimali za nchi zetu zinahitaji kutumika  vizuri, kwa sababu zinapotumika vibaya zinapunguza uwezo wa nchi zetu kuchochea maendeleo haraka, pale zinapo hatarisha sekta yetu ya fedha, matumizi adili ya rasilimali hizi na usalama wa nchi zetu" alisema Dkt. Mpango

Aidha, Dkt. Mpango amesema kuwa utakasishaji wa fedha haramu unazuiwa kwa sababu unamadhara makubwa kiuchumi, kijamii na kiusalama kwa nchi wanachama..

"Fedha ambazo zinakuja kuja tu hivi! Hujui kama zinakwenda kugharamia ugaidi, au ni fedha za wananchi wetu lakini wanazitorosha ambapo badala ya kuzitumia ipasavyo wanazitumia kufanya mambo haramu" aliongeza Dkt. Mpango

Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa Umoja wa nchi za Mashariki na Kusini Mwa Afrika ESAAMLG, Dkt. Elliawony  Kisanga amesema kuwa tangu umoja huo uanzishwe miaka 19 iliyopita, yamekuwepo mafanikio makubwa na kazi iliyopo mbele ya uongozi mpya ni kuanza na kuendelea kufanyika kwa tathmini ya mifumo ya udhibiti ya nchi za Zambia, Malawi na Tanzania.

Mwenyekiti Mpya wa ESAAMLG, Waziri wa Fedha, Biashara, Uwekezaji na Mipango ya Kiuchumi wa Seychelles Balozi Maurice Lousteau – Lalanne, ameipongeza Tanzania chini ya Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, kwa uongozi wake mahili na kuuwezesha umoja huo kutekeleza majukumu yake ipasavyo na msukumo wake utakuwa kuwezesha nchi wanachama kuendelea kusimamia utekelezaji wa sheria.

Aidha  Mkutano wa Baraza la Mawaziri wa ESAAMLG ulitanguliwa na Mkutano wa 36 wa Kikosi Kazi cha Maafisa waandamizi wa ESAAMLG, ambapo Bw. Onesmo Makombe alikabidhi kwa niaba ya Tanzania Uenyekiti wa Kikosi Kazi hicho kwa Bw. Philip Moustache wa Jamhuri ya Seychelles.

Tanzania ilipokea uongozi wa Umoja huo Septemba 7 mwaka jana wakati wa Mkutano wa 17 wa Baraza la Mawaziri wa Nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika uliofanyika Zanzibar, ikipokea majukumu ya uongozi huo kutoka nchi ya Zimbabwe ambapo Umoja huo unaundwa na nchi 18 ambazo ni Angola, Botswana, Eswatini, Ethiopia, Kenya, Lesotho, Madagascar, Malawi, Mauritius, Mozambique, Namibia, Rwanda, Seychelles, South Africa, Tanzania, Uganda, Zambia na Zimbabwe.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.