Habari za Punde

MNEC Mhe. Theresia Mtewele Achangia Milioni Moja Kwa UWT Mkoa wa Njombe.

Mbunge viti maalum Neema Mgaya akikabidhiwa hati   ya pongezi na Mgeni rasmi MNEC Bi. Theresia Mtewele kwa kutoa mchango mkubwa wa kuijenga jumuiya hiyo
Mwenyekiti wa UWT (W) Njombe  Bi. Angel Mwangeni
akikabidhiwa hati ya pongezi na Mgeni rasmi MNEC 
Bi. Theresia Mtewele
Mbunge viti maalum Dkt. Suzan Kolimba akikabidhiwa hati ya pongezi na Mgeni rasmi MNEC Bi. Theresia Mtewele

Na.Fredy Mgunda -Njombe.
UMOJA wa Wanawake Mkoa wa Njombe chini ya Mwenyekiti wa jumuiya hiyo Ndugu Rosemary Lwiva na katibu wake Ndugu Angela Milembe wamezindua kadi maalum ya kuwezesha kujiimarisha kiuchumi katika Jumuiya hiyo.

Uzinduzi huo umezinduliwa na Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi Taifa, Ndugu Theresia Mtewele katika Baraza la UWT Mkoa wa Njombe lililofanyika jumamosi tarehe 6 Oktoba 2018.  Kilele cha harambee hiyo kinatarajiwa kufungwa na Mwenyekiti wa UWT Taifa siku za mbeleni.

Awali Ndugu Theresia Mtewele amewapongeza UWT Mkoa wa Njombe kwa kuwa wabunifu na namna wanavyofanya kazi kwa umoja.

Aidha Ndugu Theresia Mtewele amewaomba  Viongozi wa UWT wawe chachu ya kukemea maovu yanayotokana na unyanyaswaji, ukandamizaji na uonevu kwa wanawake na watoto. Pia katika kukuza uchumi wa Jumuiya amewataka UWT kuifanya ajenda ya kujiimarisha kiuchumi kuwa endelevu ili kuifanya jumuiya hiyo kujitegemea kiuchumi  waweze kuendesha vizuri shughuli zao za kila siku na kuacha alama katika uongozi wao.

MNEC amewaomba pia wajikite kuimarisha uhai wa jumuiya kwa kuwa na mkakati maalum wa kuingiza wananchama wapya na kuendelea kushirikiana na wanachama wa zamani ikiwa ni pamoja na ulipaji ada.

Katika kuelekea uchaguzi wa serikali za mitaa 2019 amewaomba waweke mkakati kabambe wa kuhakikisha CCM inashinda mitaa yote ya mkoa wa Njombe pia wawahamasishe wanawake kugombea nafasi mbalimbali na kuwaelimisha umuhimu wa kichagua viongozi wanaotokana na chama cha mapinduzi.

MNEC amewaomba UWT waisemee vizuri serikali na kuwalinda viongozi wao ikiwemo wabunge na madiwani kwa kuwatia moyo na kutoruhusu wasaka vyeo kuwaingilia katika majukumu yao kwa kuanza kampeni mapema.

Baraza hilo limehudhuriwa na wabunge wa viti maalum mkoa wa Njombe Mh .  Dkt .   Suzan Kolimba na Mh.  Neema Mgaya . Wabunge hao wameomba wanawake wa Mkoa wa Njombe kuendelea kuwapa ushirikiano ili waweze kutekeleza majukumu yao vema.

Mwisho, katika uzinduzi huo MNEC alichangia shilingi 1,000,000/=.  Zoezi hilo liliambatana na ugawaji wa hati za pongezi kwa viongozi ambao wamekua na mchango mkubwa kwa Jumuiya katika Mkoa wa Njombe.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.