Habari za Punde

Uganda na Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Ikiwemo Zanzibar Zina Uhusiano wa Kihistoria Wakati wa Kupigania Uhuru.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akizungumza na  Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Nchini Uganda Mhe.Dk.Aziz Ponary Mlima  alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo kumuaga Rais,Balozi aliteuliwa hivi karibuni na Rais wa Jamhri ya Muungano wa Tanzania Dkt.John Pombe Magufuli,[Picha na Ikulu.] 12 Oct 2018.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesisitiza haja ya kuimarisha ushirikiano na uhusiano wa kihistoria kati ya Uganda na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kama zilivyoshirikiana katika kupigania uhuru.

Dk. Shein aliyasema hayo leo Ikulu mjini Zanzibar, wakati alipofanya mazungumzo na Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Uganda Dk. Aziz Ponary Mlima, aliefika Ikulu kwa ajili ya kumuaga Rais.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein alisema kuwa Uganda na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwemo Zanzibar zina uhusiano wa kihistoria tokea wakati wa kupigania uhuru wa nchi hizo, hivyo ni vyema uhusiano na ushirikiano huo ukaendelezwa kwa maslahi ya pande zote mbili.

Alieleza kuwa mbali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwemo pia Zanzibar wakati huo wa kupigania uhuru mashirikiano na uhusiano mwema ulikuwepo kwa nchi hizo pamoja na nchi jirani ikiwemo Kenya ambapo hatimae nchi zote hizo zilipata uhuru.

Alieleza kuwa licha ya kuwepo kwa mazingira tofauti ya kupata uhuru ambapo zipo nchi katika ukanda wa Afrika Mashariki zipipata uhuru kwa njia ya demokrasia lakini pia kwa upande wa Zanzibar ilipata uhuru wake kwa njia ya Mapinduzi.

Hivyo, Rais Dk. Shein alisisitiza kuwa juhudi, maarifa, ari na upendo uliooneshwa wakati huo chini ya waasisi wa nchi hizo akiwemo Hayati Mwalimu Julisus Kambarage Nyerere na wenziwe ni vyema ukaendelezwa kwa manufaa ya wananchi wa pande hizo.

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza kuwa historia inaonesha kwamba sekta ya elimu ndio kiunganishi kikubwa kilichowaunganisha watu wa Uganda na Zanzibar ambapo wananchi wa Uganda waliowemgi walifuata elimu ya dini ya Kiislamu hapa Zanzbar.

Aliongeza kuwa kwa upande wa wananchi wa Zanzibar wengi wao waliosoma vyuo vikuu vya nje wakati huo walisoma nchini Uganda katika Chuo Kikuu cha Makerere ambapo historia inajirejea ambapo hivi sasa hapa Zanzibar wapo wanafunzi wanaosoma katika vyuo vikuu vya Zanzibar wanaotoka nchini Uganda.
Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kueleza juhudi za Rais Yoweri Kaguta Museven wa Uganda anazozichukua katika kuendeleza uhusiano na ushirikiano mwema uliopo kati ya Uganda na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa anafahamu kwamba Serikali  zote mbili zimedhamiria kutekeleza Diplomasia ya uchumi katika kuhamasisha uwekezaji hasa katika sekta ya viwanda kwani ndio kiu ya uchumi wa Tanzania hivi sasa hivyo, ni matumaini yake hilo atalifanyia kazi.

Rais Dk. Shein alimtakia kazi njema Balozi huyo na kumueleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kumpa mashirikiano makubwa.

Nae Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Uganda, Dk. Aziz Ponary Mlima alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa atahakikisha uhusiano na ushirikiano wakihistoria uliopo kati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiemo Zanzibar na Uganda unaendelezwa.

Alieleza kuwa juhudi za makusudi atazichukua katika kuhakikisha mahusiano mema kati ya Tanzania na pande mbili hizo yanaimarika huku akieleza kuwa sekta ya utalii pamoja na masuala ya kuwavutia wawekezaji kuja kuekeza Tanzania ikiwemo Zanzibar yote kwa pamoja yatapewa vipaumbele.

Pamoja na hayo, Balozi Mlima alimueleza Rais Dk. Shein haja ya Watanzania kukitumia ipasavyo kituo kipya cha Uongozi kiliopo nchini Uganda kilichoitwa “Julius Nyerere Leadership Centre” ili wananchi pamoja na vijana waweze kujifunza historia na mambo mengi hasa yanayomuelezea Hayati Julius Nyerere katika uongozi wake.

Kituo hicho kilichozinduliwa hivi karibuni na Rais Yoweri Museveni ambapo katika hotuba yake ya ufunguzi alisema “ nimefurahi sana kuanzishwa kwa kituo hiki na hasa kwa kuitwa jina la Julius Nyerere kwa kuamini ya kwamba wanasiasa wa Uganda, Afrika ya Mashariki, Afrika na hata duniani kwa ujumla watakitumia ili waweze kujifunza aina mbali mbali za siasa na uongozi kama urithi wake mwenyewe Baba wa Siasa za ukombozi barani Afrika Mzee Nyerere”.

Balozi Mlima alieleza kuwa katika mambo mengi ambayo ameyafanya Mwalimu Nyerere na kumjengea sifa kubwa ndani na nje ya Bara la Afrika ni pamoja na kuasisi Muungano wa Tanganyika na Zanzibar waliouasisi yeye na Hayati Mzee Abeid Amani Karume ambao ulionesha mfano kwa viongozi wa bara la Afrika.

Balozi Mlima aliteuliwa  na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli na kumuapisha Septemba 12, 2018 Ikulu ya Chamwino Jijini Dodoma, ambapo katika historia yake ya kazi Balozi Aziz Ponary Mlima aliwahi kuwa Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Malaysia.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.