Habari za Punde

Norway Kusaidia Tanzania ukusanyaji wa Mapato


Na Grace Semfuko-MAELEZO
Serikali ya Norway imeingia makubaliano ya kuisaidia Tanzania katika kuijengea uwezo na kuimarisha mifumo ya ukusanyaji kodi ambapo imetoa  kiasi cha shilingi bilioni 25 kwa ajili ya shughuli hiyo lengo likiwa ni kuongeza mapato ya Serikali ambayo yatasaidia ujenzi wa miradi ya maendeleo kwa ajili ya kunufaisha jamii. 

Aidha Norway imesema kupitia Mfuko wa Dunia (Global Fund) itaendelea kuifadhili Tanzania kutokana na kuridhishwa kwake na Sera za kuimarisha uchumi,kuondoa rushwa na ufisadi hali ambayo wamesema inaimarisha na kuongeza ufanisi kiuchumi.

Hayo yamebainishwa na Waziri wa Maendeleo ya Kimataifa wa Norway Bwana Nikolai Astrup wakati yeye na masafara wake walipokutana na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Dkt Ashatu Kijaji, Ofisini kwake Jijini Dar Es Salaam.

Norway imekua ikichangia zaidi ya Dola Milioni 660 kwenye mfuko wa Dunia (Global Fund) huku Tanzania ikinufaika zaidi ambapo kwa mwaka huu kiasi cha Dola Milioni 56 sawa na zaidi ya Sh. Bilioni 127 zimetolewa  kwa ajili ya kuanzisha na kuimarisha miradi ya maendeleo.

“Tunatambua kuwa Wananchi wanataka Maendeleo na ndio maana sisi Norway tunafadhili kiasi hiki cha fedha ili kuhakikisha kuwa wananchi wanapata huduma za kijamii, tutaendelea kuifadhili Tanzania hasa kwenye Sekta za Elimu, Kilimo, Nishati na Gesi.” Alisema waziri huyo na kuongeza kuwa lengo la ziara yake ni kuangalia  kwa namna gani pande mbili zitaendelea kushirikiana zaidi.

Katika mazungumzo yao ,Bwana Astrup amesema kuimarisha mifumo ya ukusanyaji wa kodi, ni hatua muhimu kwa Serikali zote Duniani kwani fedha zinazokusanywa ndizo zinazofanya maendeleo na hivyo hatua ya Serikali yake ya kuisaidia Tanzania katika eneo hilo imekuja wakati muafaka na wanamatumaini makubwa kuwa lengo litafanikiwa.

Kwa Upande wake, Dkt Ashatu Kijaji alisema wakati Serikali ya awamu ya tano inaingia madarakani mwaka 2015, ukusanyaji wa mapato  ulikuwa ni wastani wa Shilingi Bilioni 800 kwa mwezi  ambapo kufuatia mifumo ya kodi kuimarishwa, wastani huo umeongezeka  kutoka kaiasi cha awali hadi Shilingi Trilioni 1.4 kwa mwezi.

“Serikali ya awamu ya tano ikishirikiana na Norway katika kuimarisha mifumo ya kodi tumeongeza asilimia 75 ya ukusanyaji wa mapato, ongezeko hilo ni kubwa na tunawashukuru sana kwani mnaona jinsi ambavyo Rais Magufuli anavyotekeleza miradi ya maendeleo kupitia fedha hizi,nyote ni mashahidi” Alisema Dkt Ashatu Kijaji, Naibu Waziri wa Fedha na Mipango.

Naye Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika katika Wizara ya Mambo ya Nje, Jestas Nyamanga alisema  Norway imekuwa ikiisaidia Tanzania kwenye miradi mingi ikiwepo ya Afya kwenye maeneo matatu kupiga vita masuala ya ukimwi , malaria na kifua kikuu.

Alisema katika Sekta ya nishati wamesaidia kufadhili  usambazaji wa umeme wa vijijini (REA) katika Mikoa ya Shinyanga, Tabora,Iringa , singida na Dodoma, ambapo zaidi ya vijiji 121 vimepata umeme huo kwa  ufadhili wa Nchi za Norway na Sweeden.

Waziri wa Maendeleo ya Kimataifa Nicolai Astrup aliwasili Nchini Novemba 28, mwaka huu kwa ziara ya kikazi akiwa na  ujumbe wake, ambapo atafanya mazungumzo na viongozi mbalimbali wa Serikali, kutembelea Wilaya ya Korogwe kukagua mradi wa umeme wa REA unaofadhiliwa na nchi yake na pia atakagua mtambo wa kuzalisha umeme wa maji uliojengwa na Norway, Sweden na Finland kwenye miaka ya 1990 na kukarabatiwa hivi karibuni na Serikali ya Norway, ambapo ataondoka Novemba 30 mwaka huu.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.