Habari za Punde

Wananchi wa Jimbo la Magomeni Zanzibar Wakabidhiwa Mipira ya Maji Safi na Salama.

Mwakilishi wa Jimbo la Magomeni Rashid Makame Shamsi akikabidhi Mipira ya maji kwa Mzee wa mtaa Azizi Mbarouk Omar ( Kushoto)  huko Shehia ya Magomeni Wandaras Mjini Unguja.
Picha na Mwashungi Tahir – Habari Maelezo.

Na Mwashungi Tahir   -   Maelezo Zanzibar.
MWAKILISHI wa Jimbo la Magomeni Rashid Makame Shamsi amewaomba wananchi wa magomeni wandaras  kuwa na mashirikiano na viongozi wao ili wanapopeleka huduma muhimu za maendeleo   kwa jamii zipate ufumbuzi.
Hayo ameyasema huko Magomeni Wandaras wakati alipokuwa akikabidhi wananchi mipira ya maji katika shehia hiyo ikiwa anatimiza ahadi yake  ili wananchi wa shehia  hiyo  waweze kupata huduma ya maji safi na salama  kwa ukaribu na kupunguza masafa marefu yaliyokuwa yakiwakabili.
Amesema iwapo viongozi wa jimbo wanajitokeza kwa kuleta huduma za maendeleo  inapaswa kuthamini na kuyafanyia kazi kwa moyo mmoja ili na wao waweze kufarijika zaidi na kuongeza kutatua changamoto nyengine zitazojitokeza .
Amesema wakati mliponichagua niliahidi  kutatua changamoto na kuleta  mambo ya maendeleo katika jimbo kati ya ahadi hizo ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma zote muhimu miongoni mwa hayo ni maji safi na salama  hii ikiwa ilani ya Chama chetu cha Mapinduzi kuwajali wananchi wake katika pande zote.
Aidha alisema kiongozi mzuri ni yule anaeahidi kwa wananchi wake na kutimiza ahadi zile alizoziahidi na asipotimiza huwa ni mnafiki na hata mwenyezi Mungu anahimiza ahadi zitimizwe kwani ahadi ni deni
“Kiongozi anaeahidi asitimize huwa ni mnafiki ni wajibu wetu kutimiza ahadi zetu kwa wananchi wetu ili na wao wajenge Imani na viongozi wao”.Alisema mwakilishi huyo.
Pia alisema Serikali yetu ya Mapinduzi ya Zanzibar inayoongozwa na Rais wetu wa Zanzibar Dkt Ali Mohamed Shein hivi sasa ina miradi  ya maji ambapo wafadhili wake ni India, Japan ifikapo 2020 maeneo mengi ya mijim yetu kwa asilimia kubwa itapata maji safi na salama.
 Vi le vile viongozi ndani ya majimbo ni wajibu kutimiza ahadi zetu iwapo hatutotimiza maendeleo yeyote baada ya miaka mitano tukitaka kurudi wananchi hawatotuelewa na pia chama chetu tutakirudisha nyuma  lakini tukikamilisha ahadi zetu tutazidi kusonga mbele kwa kuaminiwa na chama chetu tutakirahisishia ushindi wa kishindo ifikapo 2020.
Nae Mwenyekiti wa Wadi ya Magomeni Hussein Ali Mdungi amesema kukabidhiwa mipira hii kumewafurahisha sana  na  wanatoa shukurani zao za dhati kwani kutawapunguzia usumbufu wa maji waliokuwa wanaupata kwa kipindi kirefu na kuwaomba kuthamini jitihada za viongozi wetu wanazozifanya  .
Pamoja na hayo Mzee wa mtaa Azizi Mbarouk  Omar  na  wananchi wa shehia hiyo wametoa pongezi zao kwa kiongozi huyo na kusema wamepokea mikono miwili msaada wa mipira hiyo na kumuhakikishia wataitunza ili waweze kufaidika  na huduma hiyo katika maeneo hayo ili huduma hiyo iendelee kwa muda mrefu.
Jumla ya laki sita na arubaini elfu imetumika katika kupatiwa mipira hiyo ikiwa ametimiza  ahadi aliyoitowa katika shehia hiyo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.