Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, Azungumza na Waziri wa Kilimo na Masuala ya Ardhi Kutoka Jamuhuti ya Kiarabu ya Watu wa Misri Ikulu leo.

 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Waziri wa Kilimo na Masuala ya Ardhi wa Jamuhuri ya Kiarabu ya Watu wa Misri.Dkt. Ezzaldin O. Abusteit, alipofika Ikulu Zanzibar na Ujumbe wake, kwa mazungumzo na kufanya Ziara Maalum Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein  ameipongeza azma ya Jamhuri ya Kiarabu ya Misri ya kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta ya kilimo hapa nchini.
  
Hayo aliyasema leo Ikulu mjini Zanzibar wakati alipofanya mazungumzo na Waziri wa Kilimo na Masuala ya Ardhi wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri Dk. Ezzaldin Abusteit ambapo katika mazungumzo hayo Waziri huyo pia, aliahidi kushirikiana na Zanzibar katika kuliimarisha na kuliendeleza shamba la pamoja na Kilimo la JKU- Bambi, liliopo Mkoa wa Kusini Unguja.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein alieleza kuwa Misri imekuwa  mshirika mkubwa wa Zanzibar katika kuunga mkono juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar za kuimarisha sekta za maendeleo ikiwemo kilimo ambayo ni sekta muhimu katika maisha ya Wazanzibari.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa azma ya Serikali ya Misri ya kuendeleza mashirikiano katika uendelezaji wa mradi wa Shamba la pamoja la JKU-Bambi ambalo ni ushirikiano kati ya nchi hiyo na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar umeweza kuleta tija na maendeleo makubwa katika sekta ya kilimo.

Alieleza kuwa miongoni mwa mafanikio yaliopatikana ni pamoja na kuwepo kwa wataalamu na utaalamu unaotokana na msaada wa Misri ambapo juhudi hizo zimeweza kusaidia kwa kiasikikubwa katika kuendeleza sekta ya kilimo nchini hasa katika mradi huo.

Hivyo, katika maelezo yake Rais Dk. Shein alisisitiza haja ya kuendeleza ushirikiano huo sambamba na kuzidisha mikakati kwa kuendeleza tafiti za pamoja katika sekta hiyo kwa lengo la kuzidisha uzalishaji, mbegu, aina za udongo na tafiti nyenginezo kwenye vianzio vya kilimo.

Aidha, Rais Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo mikakati iliyowekwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha sekta ya kilimo hasa katika kuliendeleza na kuliimarisha Shamba hilo sambamba na Serikali ilivyojipanga katika masuala ya utafiti wa kilimo ikiwa ni pamoja na kuipa kipaumbele taasisi ya utafiti pamoja na Chuo cha Kilimo kiliopo Kizimbani.

Alieleza kuwa kwa upande wa chuo hicho cha Kilimo, tayari kimeshaungwanishwa na Chuo Kikuu cha Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) kwa lengo la kupata mafanikio zaidi katika utoaji wa taaluma ndani ya sekta ya kilimo.
Rais Dk. Shein alisema kuwa tayari mwanzo mzuri umeanza kuonekana katika  mashirikiano ya uendelezaji wa sekta hiyo ya kilimo kati ya Misri na Zanzibar na kusisitiza haja ya kuuendeleza ushirikiano huo ili uzidi kuleta mafanikio kwa pande zote mbili.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alitilia mkazo suala la mafunzo kwa wataalamu wa kilimo wa Zanzibar na kueleza haja ya kuendelezwa utamaduni uliokuwepo hapo siku za nyuma ambapo watalamu walio wengi walipata mafunzo nchini humo katika Chuo Kikuu cha Al-Azhar.

Katika maelezo hayo, Rais Dk. Shein pia, alipongeza uhusiano na ushirikiano wa muda mrefu uliopo kati ya Misri na Zanzibar na kusisitiza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na Serikali ya Misri pamoja na Kiongozi wake mkuu Rais Abdel Fattah El-Sisi na wananchi wote wa Taifa hilo.

Nae Waziri wa Kilimo na Masuala ya Ardhi wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri Dk. Ezzaldin Abusteit alimueleza Rais Dk. Shein azma ya Serikali ya Jamhuri ya Kiarabu ya Misri ilivyokusudia kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta ya kilimo hapa nchini.

Katika maelezo yake kiongozi huyo wa Serikali ya Misri aliyefika Ikulu mjini Zanzibar akifuatana na ujumbe wake kutoka serikali hiyo pamoja na Balozi wa nchi hiyo anaefanyia kazi zake katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Gaber Mohamed ambapo Waziri Abusteit alizipongeza juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar za kuimarisha sekta ya kilimo.

Katika maelezo yake Waziri huyo wa Kilimo wa Misri alimueleza Rais Dk. Shein kuwa Misri inathamini uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati ya pande mbili na kueleza kuwa Serikali ya nchi yake utauendeleza na kuuimarisha ili uzidi kuleta tija na manufaa makubwa.

Waziri Abusteit alitumia fursa hiyo kumpa Rais Dk. Shein salamu kutoka kwa Rais wa Jamuri ya Kiarabu ya Misri Abdel Fattah El-Sisi ambazo salamu hizo pia, zilisisitiza kuimarisha uhusiano na mshirikiano katika ya Zanzibar na Misri huku zikieleza kutambua juhudi zinazochukuliwa na Serikali anayoiongoza Dk. Shein katika kuimarisha sekta ya kilimo.

Aidha, Waziri huyo alimueleza Rais Dk. Shein kuwa kutokana na Wizara yake kubeba mambo muhimu yakiwemo kilimo, uvuvi na mengineyo ambayo yanashabihiana na Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi ya Zanzibar itajenga ukaribu mkubwa zaidi katika kushirikiana.

Aliongeza kuwa Misri itahakikisha inashirikiana na Zanzibar katika kuleta Mapinduzi ya Kilimo kwa kuweka kipaumbele suala la mafunzo kwa wataalamu, teknolojia ya kisasa katika kilimo pamoja na vifaa vya kilimo ili kuendana na kilimo cha kisasa na chenye tija.

Pia, Waziri huyo wa Kilimo wa Misri alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa Misri iko tayari katika kuyaunga mkono malengo ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iliyoyaweka katika kuendeleza na kuimaisha sekta ya kilimo kwa ajili ya maendeleo ya Zanzibar na watu wake.  
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.