Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein Afungua Semina ya Kitaifa Kuhusu Masuala ya Ardhi na Rasilimali Zisizorejesheka Zanzibar.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akihutubia wakati wa kufungua Semina ya Kitaifa Kuhusu Masuala ya Ardhi na Rasilimali Zisizorejesheka Zanzibar, iliofanyika katika Ukumbi wa Sheikh Idrissa Abdulwakil Kikwajuni Zanzibar.kushoto Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja Mhe. Ayoub Mohammed Mahmoud na Waziri wa Ardhi Maji Nyumba na Nishati Zanzibar Mhe. Salama Aboud Talib.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza kuwa  licha ya kuwepo Sheria tisa zinazohusiana na matumizi bora na endelevu ya ardhi hapa Zanzibar lakini bado watu hawaziheshimu na hawazifuati.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika hotuba yake ya ufunguzi wa Semina ya siku moja ya Kitaifa kuhusu masuala ya Ardhi na Rasilimali zisizorejesheka iliyofanyika katika ukumbi wa Sheikh Idrissa Abdulwakil, Kikwajuni Mjini Zanzibar ambayo imewahusisha viongozi mbali mbali wakuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Katika hotuba yake hiyo, Rais Dk. Shein alisema kuwa kwa lengo la kuhakikisha ardhi ndogo inatumika vyema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa nyakati mbali mbali imetunga Sheria tisa kuhusiana na matumizi bora na endelevu ya ardhi ikiwa ni pamoja na kuwepo wka rasilimali zisizorejesheka kama vile mchanga, mawe, udongo na rasilimali za misitu lakini hazifuatwi.

Alizitaja baadhi ya Sheria hizo ni Sheria ya Matumizi ya Ardhi Namba 12 ya mwaka 1992, Sheria ya Uhaulishaji wa Ardhi Namba 8 ya mwaka 1994 na Sheria ya Mahakama ya Ardhi Namba 7 ya mwaka 1994 ambayo ndiyo inayohusiana na uanzishwaji wa Mahakama ya Ardhi.

Rais Dk. Shein aliongeza kuwa katika ziara yake aliyoifanya katika Wilaya zote za Unguja na Pemba kuanzia tarehe 12 Februari hadi tarehe 25 Februari mwaka 2019 ameweza kufahamu mengi kuhusiana na kadhia ya kuvunjwa kwa sheria mbali mbali zinazohusiana na matumizi bora ya ardhi.

Aliongeza kuwa kwa bahati mbaya wavunjaji wa sheria hizo ni viongozi an watendaji wa Serikali na matukio mengine yanayofanywa na wananchi wa kawaida.

“Taarifa za Wilaya zilizowasilishwa kwangu zote zimethibitisha kuendelea kuibuka kwa migogoro mipya ya ardhi katika Wilaya ambazo inatofautiana kwa idadi na kwa aina yake baina ya Wilaya na Wilaya....Nna taarifa kwamba ipo migogoro ya uvamizi wa maeneo ya Serikali, ipo migogoro baina ya wananchi na wawekezaji na mingine kadhaa”,alisema Dk. Shein.

Aidha, Rais Dk. Shein alisema kuwa jambo jengine ni kuwepo kwa uharibifu mkubwa wa mazingira katika maeneo yanayochimbwa mchanga aliyoyatembelea ikiwa ni pamoja na kuwepo kwa upungufu wa mchanga wenyewe.
Alieleza kuwa katika maeneo aliyoyatembelea katika ziara yake hiyo yakiwemo aneo la Donge Chechele, Pangatupu na Kiombamvua kwa Unguja na Finya (Selem) na Shumba Viamboni kwa uapnde wa Pemba amejionea hali halisi ya rasilimali hiyo ya mcvhanga na kusisitiza kuwa mchanga ni mali ya Serikali hivyo ni mali ya wananchi wote.

Rais Dk. Shein alisitiza kuwa rasilimali ya mchanga hapa Unguja imepungua kwa kiasi kikubwa na haipo isipokuwa kuna maeneo sita yenye rasilimali hiyo lakini ni maeneo ya kilimo ambayo wananchi wanalima mazao mbali mbali ya chakula hivyo kunatakiwa maamuzi ya kuendelea na na kilimo au kuchimbwe mchanga ambao utachimbwa kwa wastani wa mwaka mmoja na nusu tu.

Alisema kuwa kwa upande wa kisiwa cha Pemba tatizo la uhaba wa rasiliamli ya mchanga halipo kwa hivi sasa lakini kwa Unguja hasa katika maeneneo yanayochimbwa mchanga ya Pangatupu na Donge Chechele mchanga haupo.

Alieleza kuwa Sheria ya Usimamizi wa Mazingira Namba  3 ya mwaka 2015 pamoja na kanuni zake  inafahamisha kwamba mchimbaji mchanga anatakiwa apate kibali, achimbe kwa kuzingatia kima maalum na ajaze mkataba wa kurejesha eneo ikiwemo kupanda miti baada ya kumaliziza shughuli za uchimbaji.

Dk. Shein alieleza kuwa utekelezaji wa Sheria hiyo umekosa usimamizi mzuri na  matokeo yake maeneo mengi  yaliokwisha kuchimbwa mchanga yamebaki kuwa ni jangwa na miti iliyopandwa katika maeneo hayo haikustawi na  haikunawiri kama ilivyokusudiwa.

Alieleza kwua takwimu zinaonesha kwamba zipo gari 750 Unguja na gari 165 Pemba zinazochukua mchanga ambapo gari hizo ni nyingi mno kwa shughuli hio na kati ya gari hizo zipo zenye uwezo wa kuchukua hadi tani 30 ambazo nazo kwa kipindi kirefu zimekuwa zikichangia uharibifu wa miundombinu ya barabara.

Hivyo, Rais Dk. Shein alisema kuwa ameamua kuitisha Semina hiyo ili kwa pamoja viongozi wakae, wajadili na hatimae wafuate njia bora zaidi ya kupambana na changamoto zilizopo kwani wao ni viongozi ambao wananchi wamewapa dhamana ya kuwaongoza wakiamini kwamba kila wakati watakuwa waadilifu, wabunifu na wenye na wenye kufanya maamuzi yenye kuzingatia maslahi mapana na nchi.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alisisitiza haja ya kufanywa kwa utafiti kama anavyosisitiza mara kwa mara katika uongozi wake kwa lengo la kukabiliana na changamoto zilizopo katika utekelezaji wa mipango ya maendeleo.

Alieleza kuwa kwa kutumia tafiti ndipo itawezekana kuwepo wka mipango imara ya matumizi ya rasilimali zilizopo sambamba na kwua na mipango na njia mbadala za kutumia pale inapolazimika kuafnaya hivyo.

Aliongeza kuwa tafiti ndizo zinazowezesha kutambua vizuri vyanzo na uhalisia wa migogoro ya ardhi na mambo yanayosababbisha na hatimae kuwa na njia za kisayansi za kutatua “Na sisi ni lazima tufanye utafiti kwani tunazotaasisi za tafiti na Kila Wiaza ina Idara inayohusiana na utafiti”,alisisitiza Dk. Shein.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alieleza kuwa mara kadhaa amekuwa akisisitiza juu ya umuhimu wa kuwa na mipango madhubuti itakayowezesha kutekeleza mipango ya kuimarisha ufukiaji wa ardhi (Land Reclamation) na kueleza azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kufanya ufukiaji huo katika eneo la Gulioni hadi Mpigaduri.

Alieleza kuwa huo ndio mwelekeo wa nchi nyingi za visiwa hivi sasa kama ni hatua muhimu ya kuongeza maeneo ya ardhi waliyonayo na kutolea mfano nchi ya Singapore ambayo imeweza kuongeza eneo la ardhi yake kwa zaidi ya asilimia 24 ikilinganishwa na ukubwa wa ardhi hio ilivyokuwa mwaka 1960.

“Vile vile Uholanzi, Umoja wa Falme za Kiarabu na kadhalika nazo zimeongeza eneo la nchi zao kwa kuifukia bahari”,aliongeza Dk. Shein.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alieleza kuwa mradi mkubwa wa Mtoni Marine uliofanywa na mzalendo Sheikh Said Salim Bakhressa umedhihirisha kwamba inawezekana kuongeza ukubwa wa eneo la ardhi iliyopo na ikatumika vizuri katika miradi ya uwekezaji na shughuli nyengine za kiuchumi na kijamii.

Pia, Rais Dk. Shein ameeleza jinsi anavyosisitiza ujenzi wa majengo ya ghorofa kwa lengo la kuihami ardhi ndogo iliyopo.

“Sisi ni viongozi lazima tuamini kwamba mamo haya yote tunaweza kuyafanya sisi wenyewe hapa Zanzibar.......kwa hivyo, nyinyi ni wataalamu na viongozi naamini kwamba katika semina hii, suala la matumizi bora ya ardhi na rasilimali zetu mtalitazama kwa upana zaidi na kwa kuzingatia maendeleo ya sayansi na teknolojia hivi sasa, ili nasio nasi tuweze wkenda kwa kasi zaidi”,alisisitiza Rais Dk. Shein.

Mapema Waziri wa Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati Salama Aboud Talib akimkaribisha Rais Dk. Shein alieleza alieleza kuwa Semina hiyo itasaidia kwa kiasi kikubwa kujua hali halisi iliyopo juu ya suala zima la ardhi na mali zisizorejesheka hapa Zanzibar.

Katika Semina hiyo Mada  mbali mbali zitatolewa ikiwemo Sheria Zinazosimamia Matumizi ya Ardhi Zanzibar, Haliya Maendeleo ya Rasilimali za Misitu na Changamoto zake, Hali Halisi ya Maliasili Zisizorejesheka Zanzibar, Hali ya Mchanga Zanzibar na Muelekeo wake na hatimae Majumuisho na Maazimio ya Semina hiyo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.