Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, Azungumza na Mwenyekiti wa Kampuni ya Touchroad Group ya China Ikulu Zanzibar.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na mgeni wake Mwenyekiti wa Kampuni ya Touchroad Group ya China Ndg,He. Liehui, alipofika Ikulu Zanzibar kwa mazungumzo na Rais wa Zanzibar, kushoto Mwenyekiti wa Bodi ya Utalii Tanzania Mhe. Jaji Thomas Mihayo.Mazungumzo hayo yamefanyika leo 8-3-2019.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameikaribisha Kampuni Touchroad Group kutoka nchini China kuja kuekeza  Zanzibar huku akiipongeza kwa azma yake ya kuitangaza Zanzibar kiutalii.

Dk. Shein ameikaribisha Kampuni ya Touchroad Group wakati alipofanya mazungumzo na Mwenyekiti wa Kampuni hiyo He Liehui yenye Makao Makuu yake mjini Shanghai, nchini China.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein aliikaribisha Kampuni hiyo na kumueleza Mwenyekiti wake He Liehui kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iko tayari kutoa ushirikiano wake mkubwa na kuweka mazingira mazuri katika kuhakikisha azma ya Kampuni hiyo inafikiwa.

Dk. Shein alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imekuwa na mashirikiano ya muda mrefu na Kampuni kutoka nchini humo hiyo ni kutokana na uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati ya Zanzibar na China.

Alisema kuwa China imeweza kuiunga mkono Zanzibar na kutoa ushirikiano wake mkubwa katika kuendeleza na kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo zikiwemo afya, elimu, kilimo, viwanda, habari, miundombinu na sekta nyenginezo tokea kuasisiwa kwa Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964 ambapo ni miaka 55 hivi sasa.

Aidha, Dk. Shein alimuueleza Mwenyekiti huyo kuwa aliweza kujionea mweyewe hatua iliyofikiwa na Kampuni hiyo katika shughuli zake za uwekezaji inazozifanya nchini Djibout wakati wa ziara yake mnamo mwezi Mei mwaka 2017.

Katika ziara hiyo ambapo Rais Dk. Shein alitembelea maeneo mbali mbali nchini humo yakiwemo yale ambayo yameekezwa na Kampuni hiyo ikiwemo Bandari ya kisasa ya Djibout na eneo la Maeneo huru ya Kiuchumi.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alieleza kuwa azma ya Kampuni hiyo ya kuitangaza Zanzibar kiutalii itasaidia kwa kiasi kikubwa katika jitihada za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inazozichukua katika kuitangaza sekta hiyo Kitaifa na Kimataifa.

Aliongeza kuwa ushirikiano utakaoimarishwa kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Kampuni hiyo utasaidia kwa kiasi kikubwa katika kuwaletea maendeleo wananchi wa Zanzibar hasa ikizingatiwa kuwa uwezo wa Kampuni hiyo ni mkubwa sambamba na uzoefu ulionao ndani na nje ya Bara la Afrika.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuipongeza Kampuni hiyo kwa kuonesha nia ya kutangaza fursa za utalii zilizopo nchini.

Nae Mwenyekiti wa Kampuni ya Touchroad Group ya nchini China He Liehui, alipongeza mapokezi aliyoyapata pamoja na mazungumzo na majadiliano mazuri ya ushirikiano aliyoyafanywa kati ya Kampuni hiyo na uongozi wa Wizara ya Biashara, Viwanda pamoja uongozi wa Mamlaka ya Vitega Uchumi Zanzibar.

Aidha, Mwenyekiti huyo wa Kampuni ya Touchroad alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa kuna kundi kubwa la watalii wapatao 10,000 watakaokuja Tanzania mwaka huu wa 2019 ambao wataletwa na Kampuni hiyo na kusisitiza kuwa atahakikisha wanaitemebela Zanzibar.

Alieleza kuwa kundi hilo kubwa la watalii kutoka nchini China linalotarajiwa kuwasili kwa awamu katika mwaka huu mbali ya kuwashirikisha watalii pia watakuwemo wafanyabiashara pamoja na wawekezaji ambao watafika na Zanziar.

Mwenyekiti huyo alimuahidi Rais Dk. Shein kuwa kundi la mwanzo la watalii hao linatarajiwa kuwasili mwezi Mei mwaka huu ambalo litajumuisha watalii wasiopungua 300 ambao nao wataitemebelea Zanzibar.

Alieleza kuwa Kampuni yake ina azma ya kuitangaza Zanzibar na kutoa fursa mpya ya kuvitangaza vivutio viliyopo ili Zanzibar iendelee kuwa kivutio kikubwa cha watalii kutoka nchini China.

Alisisitiza kuwa Kampuni hiyo iko tayari kuanzisha usafiri wa moja kwa moja kati ya Zanzibar na China kwa lengo la kuwaleta watalii kuja kuitembelea Zanzibar na kuagalia vivutio vilivyopo.

Mwenyekiti huo alimueleza Rais Dk. Shein jinsi Kampuni yake ilivyopata mafanikio na kuwa Kampuni iliyoekeza kwa kiasi kikubwa  ambayo imeweza kushirikiana na nchi zipatazo 25 za Bara la Afrika zikiwemo Djibout, Afrika Kusini, Nigeria, Zimbabwe, Botswana na nyengienzo pamoja na kuwa na ofisi katika nchi nane za Afrika.


Mapema Mwenyekiti wa Bodi ya Utalii Tanzania Jaji Thomas Mihayo alimueleza Rais Dk. Shein kuwa ziara ya Mwenyekiti huyo wa Kampuni ya Touchroad Group ni sehemu ya utekelezaji wa Makubaliano yalioingiwa kati ya Tanzania na Kampuni hiyo ya kutangaza vivutio vya utalii vya Tanzania katika soko la China.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.