Habari za Punde

Rais wa Shirikisho la la Michezo ya Jumuiya ya Madola (IOC ) Bi. Dame Kuunga Mkono Juhudi za Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Kuimarisha Michezo Mbalimbali Zanzibar.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Rais wa Shirikisho la Michezo ya Jumuiya ya Madola Bi. Dame Louis Martin, alipofika Ikulu Zanzibar kwa mazungumzo leo.

Na. Abdi Shamna Ikulu. Zanzibar.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, amelipongeza Shirikisho la Michezo la Jumuiya ya Madola (IOC), kwa kuunga mkono juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha michezo mbali mbali nchini.

Dk. Shein ametowa pongezi hizo wakati alipokutana na Rais wa IOC Dame Louse Martin aliefika Ikulu na ujumbe wake kwa ajili ya mazungumzo.

Rais huyo wa IOC yupo Zanzibar kwa ajili ya kuhudhuria mkutano  maalum  wa Shirikisho la Michezo Jumuiya ya Madola (IOC), Kanda ya Afrika ulioanza jana katika hoteli Verde Mtoni mjini hapa.

Mkutano huo wa siku tatu  unawashirikisha wajumbe kutoka nchi 19 za Afrika, ambapo pamoja na mambo mengine unatathmini maendeleo ya michezo katika kanda hiyo, ushindani wa kimichezo katika michuano ya Jumuiya ya Madola pamoja na ushiriki wa Kanda hiyo katika michuano ijayo ya Jumuiya ya Madola itakayofanyika Birmigham nchini Uingereza, mwaka 2022.

Dk. Shein alisema kwa miaka kadhaa sasa IOC imekuwa ikiunga mkono kikamilifu  juhudi za Serikali katika kuendeleza michezo mbalimbali nchini kupitia nyanja za kiufundi, mafunzo na rasilimali fedha.

Alisema hatua hiyo imeiwezesha Zanzibar kupata mafanikio makubwa ya michezo na hivyo kuleta ushindani mkubwa katika ukanda wa Afrika Mashariki na duniani kwa ujumla.

Alisema Zanzibar ina historia kubwa ya mafanikio kupitia sekta ya michezo, akitolea mfano wa ushindani mkubwa uliokuwa ukionyeshwa na wanamichezo wake katika michuano mbali mbali, ikiwemo ile ya Gossage, iliyokuwa ikizikutanisha nchi za Afrika Mashariki.

Aidha, aliliomba Shirikisho hilo kuendelea kuisaidia Zanzibar harakati zake za kuinua michezo, pamoja na  kukiendeleza kizazi kipya kiliopo ambacho kimebarikiwa kuwa na vijana wengi wenye vipaji.

Nae, Rais wa IOC, Dame Louse Martin alimhakikishia Dk. Shein azma ya Shirikisho hilo kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha michezo mbali mbali kupitia nyanja tofauti.

Alisema ameridhishwa sana na juhudi zinazochukuliwa na  viongozi wa michezo nchini katika kuhakikisha Zanzibar inapiga hatua kubwa za maendeleo kimichezo na kutajika duniani kote.

Katika ujumbe wake, Rais huyo wa IOC alifuatana na Makamu wa Rais wa IOC Kanda ya Afrika Miriam Moyo , Rais wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC) Gulam Abdalla Rashid pamoja na Katibu Mkuu wa TOC Filbert Bayi.      
Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 
 E-mail: abdya062@gmail.com


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.