Habari za Punde


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Ali Mohamed Shein amewataka wananchi kuendelea kuvumiliana,kuheshimiana na kusaidiana bila ya kujali rangi, kabila wala dini kwa lengo la kudumisha amani na utulivu uliopo ili kuitekeleza saumu kwa usalama.

Alhaj Dk. Shein aliyasema hayo katika risala maalum aliyoitoa kwa wananchi kupitia vyombo vya habari katika kuukaribisha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani katika mwaka huu wa 1440 Hijria sawa na mwaka 2019 Miladia.

Katika risala yake hiyo, Alhaj Dk. Shein alisema kuwa kila mmoja ana wajibu wa kuzingatia sheria na  kujiepusha na vitendo vyote vinavyoweza kusababisha kuvunjika kwa amani.

Alhaj Dk. Shein alisisitiza kuwa zipo baadhi ya nchi ambazo wananchi wake wanaikosa neema hiyo ya amani kwa nyakati mbali mbali na wanalazimika wafunge wakiwa katika mtihani wa migogoro ya wenyewe kwa wenyewe isiyokwisha.

“Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kuukaribisha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani wakati nchi yetu ikiwa katika hali ya amani na utulivu…….hizi ni miongoni mwa neema nyingine ambazo Subhana wa Taala ametushushia”,aliongeza Dk. Shein.

Aidha, Dk. Shein alisema kuwa hizo ni tunu ambazo wananchi wanapaswa kuzitunza kwa sababu mahali panapokosa amani na utulivu nafsi za watu wake huwa muda wote katika wahka na taharuki, mambo ambayo yanaondoa unyenyekevu na taqwa katika utekelezaji wa ibada.

Alieleza kuwa utulivu wa nafsi unahitajika katika kufanya ibada kwa umakini na pia, unahitajika katika kutekeleza shughuli nyengine za maendeleo na zile za kujitafutia riziki za kila siku.

Aliongeza kuwa kwa mnasaba huo hali ya amani na utulivu ni msingi muhimu unaolazimika kuenziwa na kuendelezwa kwa nguvu zote.

Pamoja na hayo, Alhaj Dk. Shein aliwasisitiza waumini wa dini ya Kiislamu kuendeleza wajibu wao kwa kujiandaa na kutia nia ya kuukabili Mwezi Mtukufu wa Ramadhani kwa kuongeza jitihada katika uchamungu ili kuweza kunufaika na fadhila za mwezi huo.

“Ni dhahiri kwamba sisi waja ni watendaji makosa, na baadhi ya wakati huwa tunatenda kwa kujua na mara nyengine bila ya kujua. Hivyo, jitihada zatu za kufanya ibada kwa wingi katika mwezi huu zitatupelekea kusamehewa makosa yetu”,alisisitiza Alhaj Dk. Shein.

“Namuomba Mwenyezi Mungu atuwezeshe kuufunga Mwezi Mtukufu wa Ramadhani kwa salama na atuwezeshe kupata fadhila za mwezi huu…….Mwenyezi Mungu atupe wasaa wa kuapa riziki za halali na atufanyia wepesi kwa kila zito ambalo lina heri kwetu”.

“Tunamuomba Mola wetu atuwezeshe kufanya ibada kwa wingi ili iwe sababu ya kutughufiria makosa yetu kadhalika kwa barabaka za Mwezi huu Mtukufu wa Ramadhani, tunamuomba awape maghufira ndugu zetu na wazee wetu waliokwishatangulia mbele ya hahi”, Alhaj Dk. Shein alimalizia risala yake hiyo.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.