Habari za Punde

ZAWA Kupeleka Maji Safi na Salama Kwa Wananchi Maeneo Mbalimbali ya Unguja na Pemba.


WANANCHI wanaoishi katika maeneo yenye shida ya maji Zanzibar wamempongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein kwa kutekelezwa vyema agizo alilolitoa kwa taasisi husika la kupatiwa maji safi na salama katika kipindi hichi cha mwezi wa Ramadhani.

Katika maelezo yao wananchi hao walitoa pongezi zao hizo kwa nyakati tofauti kufuatia agizo alilolitoa Rais Dk. Shein katika risala yake ya kuukaribisha mwezi mtukufu wa Ramadhani mwaka huu la kupatiwa huduma hiyo muhimu.

Katika risala hiyo Rais Dk. Shein aliiagiza Wizara ya Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati na uongozi wa Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA) kuhakikisha kuwa ule utaratibu wa kila mwaka wa kusambaza maji unatekelezwa katika maeneo yenye shida ya maji.

Mbali ya maeneo hayo pia, Rais Dk. Shein alitoa agizo hilo la kupelekwa huduma hiyo kwa maeneo ambayo bado huduma za maji safi na salama hazijafika kwa wananchi katika sehemu mbali mbali za Unguja na Pemba.

Wananchi katika maeneo hayo walieleza jinsi wanavyopata huduma hiyo vizuri katika kipindi hichi cha mwezi wa Ramadhani na kueleza jinsi wanavyofarajika kutokana na zoezi hilo linavyofanywa na Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA) linavyokwenda vizuri.

Wananchi wa maeneo mbali mbali katika kisiwa cha Unguja na Pemba wameeleza kufarajika kwao na juhudi za makusudi zinazochukuliwa na  Mamlaka ya Maji (ZAWA) katika kuhakikisha wanapata maji safi na salama katika kipindi hichi cha mwezi wa Ramadhani.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na maeneo tofauti hasa katika mji wa Zanzibar wananchi hao walitoa shukurani na pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa agizo lake hilo ambalo walisema kuwa limesaidia katika kuhakikisha wanapata huduma hiyo muhimu.

Walieleza kuwa huduma hiyo ni muhimu katika maisha yao hasa katika kipindi hichi cha mwezi wa Ramadhani ambao mahitaji huwa yanazidi kwa kiasi kikubwa hivyo waliupongeza utamaduni huo aliouweka Rais Dk. Shein wa kuikumbusha Wizara na Mamlaka yake ya Maji (ZAWA) kila mwaka inapowadia Ramadhani kuwasogezea karibu zaidi huduma hiyo wananchi.

“Kuna kila sababu za kuipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Rais Dk. Ali Mohamed Shein kwa agizo lake alilolitoa kwenye taarifa yake ya kuukaribisha mwezi wa Ramadhani na sisi wananchi tulio na shida ya maji tuletewe maji, tunampongeza jinsi anavyotujali”, alisema Bi Fatma Khamis mkaazi wa Uroa.

Hivi karibuni, Waziri wa Wizara Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati Salama Aboud Talib akisoma muhtasari wa taarifa ya utekelezaji wa Mpango Kazi wa Wizara hiyo kwa kipindi cha Julai 2018 hadi Machi 2019 alieleza kuwa Wizara hiyo kupitia Mamlaka ya Maji (ZAWA) imeendelea kusimamia shughuli za program za uhuishaji na upanuzi wa shughuli za maji mijini na usambazaji wa maji vijijini.

Aliongeza kuwa katika utekelezaji wa Programu hiyo Mamlaka ya Maji kupitia mradi wa ADF-12 imeendelea na kazi ya ujenzi wa Tangi la Saateni katika sehemu ya nne ya nguzo na kufikia asilimia 50 ya ujenzi na kwa upande wa Tangi la Kilimani Mnara wa Mbao lipo hatua ya jamvi la juu ambapo ujenzi wake umefikia asilimia 65.

Aidha, alieleza kuwa Mradi huo umefanikiwa kulaza mabomba kwa masafa ya kilomita 60 katika maeneo ya Bumbwisudi, Kizimbani, Kianga, Welezo, Mikunguni, Mwembemakumbi, Makadara, Mwembeladu, Rahaleo, Miembeni na Mkunazini.

Nao uongozi wa Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA), ulieleza  juhudi unazoendelea kuzichukua katika kuwapelekea maji safi na salama wananchi wa maeneo mbali mbali yakiwemo Uroa, Ndijani, Fukuchani, Michamvi, Jitimai ya zamani, Kwarara na maeneo mengine kwa upande wa Unguja.

Na kwa upande wa Pemba ulieleza kuwa miongoni mwa maeneo yanayopelekwa huduma hiyo ni pamoja na Kaskazini Pemba huko Kwale, Mnyati Gombani ya Kale, Fenewani Shehia ya Kwale Kusini, Kilimahodi, Kilimani, Mitamani Shehia ya Mfikiwa Mkoa wa Kusuni Pemba na maeneo mengineyo.

Nao wafanyakazi wa Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA) walieleza jinsi wanavyopata mashirikiano kutoka kwa wananchi na kuwapongeza wananchi hao kwa kutekeleza agizo la Rais Dk. Shein la kuwataka wananchi kwa upande wao kutoa mashirikiano kwa Mamlaka hiyo katika zoezi hilo.

Katika hotuba zake anazozitoa Rais Dk. Shein amekuwa akisisitiza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaendelea kutekeleza miradi kadhaa ya maji safi na salama kwa lengo la kuongeza kiwango cha upatikanaji wa maji katika maeneo mbali mbali ya Unguja na Pemba.

Uwamuzi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wa kuimarisha huduma za maji safi na salama ni wa busara na wa msingi katika kuondosha kero zinazowakabili wananchi unaokwenda sambamba na Malengo ya mwaka 2020 na Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini nchini (MKUZAIII) pamoja na utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM 2015-2020 katika kuimarisha huduma za maji safi na salama Zanzibar.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.