Habari za Punde

TANESCO YAMWAGIWA SIFA MAONESHO SABASABA


 Mtaalamu kutoka kampuni tanzu ya TANESCO ya uendelezaji jotoardhi Tanzania, (aliyechuchumaa), akiwapatia maeelzo wananchi hawa wakiwemo wanafunzi jinsi jotoardhi linavyoweza kuzalisha umeme, wakati walipotembelea banda la TANESCO Sabasaba Julai 7, 2019.

NA K-VIS BLOG, SABASABA
WANANCHI wanaofika kwenye banda la Shirika la Umeme nchini (TANESCO), wamesifu hali ya upatikanaji umeme kwa hivi sasa. 
Bw. Majid Omary ni mkazi wa Mbagala jijini Dar es Salaam, aliyefika kwenye banda la TANESCO kwenye viwanja vya Sabasaba kunakofanyika Maonesho ya 43 ya biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam leo Jumapili Julai 7, 2019 alisema 
“Kwakweli mnastahili pongezi, tulikuwa katika shida kubwa ya kupata umeme wa uhakika kwa muda mrefu, lakini hali kwa sasa imebadilika sana, umeme hausumbui kama ilivyokuwa hapo awali.” Alisema.
Alisema "Eneo ninakotoka Mbagala Kilungule, tulikabiliwa na tatizo la kupata umeme usiokuwa na nguvu ya kutosha kwa muda mrefu, pia ulikatika katika, tulisononeka sana lakini tunashukuru Mungu tatizo hilo sasa halipo, hali ya umeme ni nzuri sana." Alisema Bw. Omary

Kama bado kuna mtu anawalaumu basi ana sababu zake, lakini kwakweli mimi ninawapongeza sana, nimeona nipite tu hapa kuwapa pongezi, alisema Bw. Omary wakati akizungumza na wahudumu wa TANESCO waliokuwa kwenye kitengo cha huduma kwa wateja kwenye banda hilo.
Mwingine aliyepongeza huduma bora za TANESCO ni Bi. Agatha Moses, yeye anatoka Gongolamboto jijini Dar es Salaam, alisema huduma za umeme zimeimarika sana, kwani katika eneo anakoishi hawakumbuki ni lini umeme ulikatika.
“Hata ukikatika inachukua muda mfupi unarejea, sio kama zamani hali ilikuwa tete, umeme ukikatika ndio basi tena.” Alifafanua.
Aidha katika banda la TANESCO wananchi wanaalikwa kutembeela kwenye banda hilo kujipatia huduma mbalimbali kama ambazo zinazotolewa kwenye ofisi za TANESCO.
Leila Muhaji ni Kaimu Meneja Uhusiano wa TANESCO alisema, wananchi wanaotaka fomu za maombi ya awali ya kuombea umeme wanaweza kufika kwenye banda hilo na wataalamu watawapatia fomu bure kabisa.
“Uje tu na picha ya passport size na kitambulisho chako utajaza fomu na itachukuliwa hapa hapa Sabasaba na kupelekwa katika mkoa husika ili maombi yashughulikiwe.” Alifafanua Bi. Leila.
Katika banda la TANESCO wananchi wanaweza kujionea mashine (mfano) ya kufua umeme wa maji, ambayo wataalamu wanaonyesha hatua zote kuanzia ufuaji umeme hadi unapomfikia mteja.
“Pia unaweza kujinunulia umeme, wapo watu wanokuja kwenye maonesho na inatokea umeme umeisha nyumbani basi TANESCO tunatoa huduma hiyo kwenye banda na unaweza mkununua umeme.” Aliongeza Bi. Leila Muhaji.
 Mtaalamu wa Mita za umeme, Bi. Matilda Cassian (wakwanza kushoto) akimfafanulia mambo mbalimbali yahusuyo huduma ya kupatiwa mita za umeme kwa mwananchi huyu aliyefika banda la TANESCO Julai 7, 2019.
Afisa Huduma kwa wateja TANESCO, Bw. Khairu Rashid, (kushoto) akimsikilzia mteja aliyefika banda la Shirika hilo Julai 7, 2019.
Mhandisi Ajuaye Jeggo (wapili kulia) na Mhandisi Esther Mushi, wote kutoka Idara ya usambazaji umeme, wakimsikiliza kwa makini mteja huyu alyetembelea banda la TANESCO Julai 7, 2019.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.