Habari za Punde

Walezi wa Vituo Vya Watoto Yatima Wapata Elimu ya Kukabiliana na Maafa.

Na Khadija Khamis –Maelezo Zanzibar  10/07/2019.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kamisheni ya kukabiliana na maafa Zanzibar Ndg.Makame Khatib Makame amesema elimu ya majanga ya maafa ni muhimu kupewa  watoto na walezi ili kuweza kujikinga pindipo yakitokea .
Akifungua mafunzo ya siku moja ya kutoa elimu kwa walezi na watoto wa Kituo cha kulelea Watoto Yatima Mazizini ili kujua jinsi ya kukabiliana na maafa ikiwemo mtetemeko wa ardhi ,moto ,mafuriko pamoja na kimbunga .
Alisema kuwa watoto, wazee, walemavu na mama wajawazito ni waathirika wakubwa hivyo wakipata elimu itawasaidia kujiokoa na majanga na kusaidiana na wengine.
Alifahamisha kuwa  suala la maafa linamgusa kila mtu hivyo iko haja ya kuwafikishia taaluma watoto waliomo katika vituo mbali mbali ili kuweza kujikinga kwani maafa huwa hayachagui umri wala jinsia  .
“Suala la maafa linamgusa kila mtu wala halichagui muda na hutokea wakati wowote lazima tuwe na tahadhari .“alisema MkurungenzI Makame  .
Nae Mkurugenzi wa Wanawake na Watoto ambae pia ni Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Wazee na Ustawi wa Jamii Nasima Haji Chum alisema mafunzo yatasaidia kuwapa uwezo walezi na watoto kupambana ili kupunguza athari .
Alisema maisha ya binaadamu yamezungukwa na mambo mengi ikiwemo majanga ya maafa ya kimaumbile na maafa ambayo yanayosababishwa na binaadamu hivyo ni muhimu kujua jinsi ya kuweza kujiokoa hasa kwa wale makundi maalum .
Ofisa Mratibu wa kutoa Elimu kutoka Kamisheni ya Kukabiliana na Maafa Aziza Ali Rajabu alisema  elimu watakayopata walezi na watoto wa vituoni itasaidia kuokoa na kupunguza  athari za majanga ya maafa  katika sehemu mbali mbali .
Aliwataka walezi na watoto wenye umri mkubwa ambao tayari wanajitambua kuwa na tahadhari kwa wenzao wadogo ili  kuwaepusha na kuchezea vitu hatarishi kama umeme na  kuwasha vibiriti  karibu na majiko ya gesi .
Nae Mdhamini wa Kituo cha Kulelea watoto Yatima Mazizini Chum Ali  Abeid alisema wamefurahishwa na kupata fursa ya mafunzo hayo watayafanyia kazi na kuwa na tahadhari kubwa kwa watoto wao.
Aidha alisema elimu hii itawajengea uwezo wa kujua jinsi gani wataweza kumuokoa mtoto pindipo ataanguka na kuzimia na kuwadhibiti pindi maafa yakitokea ili kuokoa maisha yao.
Nao watoto waliopata  mafunzo hayo wamesema wamefurahishwa na taaluma hiyo na kuahidi kuyafanyia kazi na kuyafikisha kwa wenzao ,
Mafunzo hayo ya siku moja yalijumuisha vituo vya kulelea watoto yatima ikiwemo  kijiji cha kulelea watoto yatima SOS pamoja na mazizini .

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.