Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Shein Azungumza na Balozi wa Rwanda Nchini Tanzania Mhe. Eugine Kayihura.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein azungumza na Balozi wa Jamuhuri ya Rwanda Nchini Tanzania Mhe.Eugine Kayihura alipofika Ikulu Zanzibar kuja kumuaga baada ya kumaliza muda wake wa kazi Nchini Tanzania.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza kuwa lugha ya Kiswahili itakuwa ni kiunganishi kizuri katika kukuza ushirikiano na uhusiano kati ya Rwanda na Zanzibar.

Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo Ikulu mjini Zanzibar wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Rwanda nchini Tanzania Eugine Kayine Kayihura ambaye alifika Ikulu kwa ajili ya kuaga.
  
Katika maelezo yake, Rais Dk. Shein alimueleza Balozi Kayihura kuwa azma ya Rwanda na Zanzibar kushirikiana katika sekta ya elimu hasa katika mafunzo ya lugha ya Kiswahili itajenga uhusiano mwema kati ya pande mbili hizo.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa hatua hiyo itakuwa na mafanikio makubwa hasa ikizingatiwa kuwa hivi sasa lugha ya Kiswahili tayari imeteuliwa kutumika rasmi katika Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC).

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza kufurahishwa kwake na uhusiano mzuri uliopo kati ya Rwanda na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwemo Zanzibar jambo ambalo amesisitiza kuwa ni vyema likaendelezwa kwa nguvu zote.  

“Mahusiano na mashirikiano yetu ni lazima yaendelezwe kwani sote ni ndugu na haya ndio yanayotupa nguvu na ari ya kuyaimarisha na kuyaendeleza maendeleo yetu tulioyapata sambamba na kufikia malengo tuliyoyakusudia”,alisema Dk. Shein.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alimueleza Balozi huyo mafanikio yaliopatika Zanzibar kutokana na sekta ya utalii ikiwa ni pamoja na kuongezeka kwa idadi kubwa ya watalii ndani ya miaka hii tisa ya uongozi wake.

Alimueleza Balozi huyo kuwa idadi ya watalii wanaokuja kuitembelea Zanzibar imeongezeka kwa kiasi kikubwa ikifananishwa na ile ya mwaka 2010 ambapo kwa hivi sasa watalii wanakadiriwa kufikia laki sita wametembelea Zanzibar.

Hivyo, alieleza kuwa kuwepo kwa mashirikiano kati ya Rwanda na Zanzibar katika sekta hiyo kutakuwa na manufaa kwa pande zote mbili.

Katika kuhakikisha sekta ya utalii inaimarika zaidi, Dk. Shein alimueleza Balozi huyo mikakati iliyowekwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kuendeleza ujenzi wa jengo jipya la abiria katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume.    

Alisisitiza kuwa hatua hiyo ya kuendeleza ujenzi huo ambao ulisita kwa muda itazidisha na kuongeza idadi ya watalii watakaoingia Zanzibar na kupelekea sekta hiyo izidi kuimarika na kuongeza pato la Taifa sambamba na fedha za kigeni.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alimuhakikishia Balozi Kayihura kuwa Serikali ya Zanzibar chini ya uongozi wake itashirikiana nae vyema Balozi mpya wa Rwanda atakayekuja kuchukua nafasi yake.

Nae Balozi Eugine Kayihura alisema kuwa Rwanda inajivunia uhusiano na ushirikiano mzuri uliopo kati yake na Zanzibar na kusisitiza kuwa miongoni mwa mahusiano hayo ni kushirikiana katika sekta ya elimu hasa katika kujifunza lugha ya Kiswahili ambayo Zanzibar ndio kitovu cha lugha hiyo.

Kutokana na hali hiyo, itakuwa ni jambo la busara kwa Rwanda kuleta vijana wake kwa lengo la kujifunza Kishwahili sambamba na kubadilishana uzoefu kati ya vijana hao na wenzao wa Zanzibar hatua ambayo itakuza na kuimarisha uhusiano na ushirikiano.

Aidha, alisema kuwa Rwanda ina mambo mengi ya kujifunza na kupanua wigo kutoka Zanzibar kutokana na mafanikio makubwa yaliopatikana katika sekta ya utalii ambapo, watalii wengi wanaotembelea Rwanda pia, hufika na Zanzibar.

Sambamba na hayo, Balozi huyo alieleza kufurahishwa kwake na mafanio iliyoyapata Zanzibar hasa katika kuimarisha sekta ya Utalii na kupongeza juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Dk. Shein katika kufanikisha sekta hiyo.

Balozi Kayihura ambaye alimueleza Rais Dk. Shein kuwa anatarajia kituo chake kipya cha kazi kitakuwa ni Afrika ya Kusini alimuhakikishia Rais kuwa Rwanda kupitia Balozi wake mpya atakayechukua nafasi yake ataendelea kushirikiana na Zanzibar. 

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.