Habari za Punde

Washiriki wa Mafunzo ya Upishi na Ukarimu Wametakiwa Kuyatumia Mafunzo Hayo kwa Ufanisi Sehemu zao za Kazi.


Katibu Mkuu Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Ndg. Salum Maulid Salum akihutubia wakati wa ufungaji wa Mafunzo ya Ukarimu na Upishi yaliotolewa na Taasisi ya China National Research Institute of Food &Fermentation Industries, ufungaji wa mafunzo hayo umefanyika katika ukumbi wa Sheikh. Idrisa Abdulwakil Kikwajuni Zanzibar. 

UTOAJI wa mafunzo ya watumishi katika maeneo ya kazi ni miongoni mwa vipaumbele vya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba chini ya uongozi wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein.

Hayo yameelezwa leo na Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Salum Maulid Salum wakati akifunga mafunzo  ya Upishi na Ukarimu ya awamu ya tatu hafla liyofanyika huko katika Ukumbi wa Sheikh Idrissa Abdul Wakil, Kikwajuni mjini Zanzibar.

Katika maelezo yake Katibu Mkuu huyo alieleza kuwa  hatua hiyo inatokana na ombi maalum la Rais  Dk. Shein kwa Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China la kuja kutoa mafunzo kwa watumishi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ili kuongeza ufanisi wa shughuli zao.

Aliongeza kuwa hicho ni kitendo cha kutekeleza sheria ya Utumishi wa Umma Namba 2 ya mwaka 2011 pamoja na kanuni za Utumishi wa Umma kwa vitendo na kuonesha dhamira yake ya dhati ya kuwaendeleza kitaaluma wafanyakazi wa taasisi mbali mbali hapa nchini.

“Kwa hakika tuna wajibu wa kuendelea kumshukuru Mheshimiwa Rais wetu kwa busara, mapenzi na uzalendo wake kwa maendeleo ya wafanyakazi na wananchi wote wa Zanzibar”,alisema Katibu Mkuu Salum.

Aidha, Katibu Mkuu huyo aliwataka Washiriki wa Mafunzo hayo kulipa hisani hiyo kwa Rais Dk. Shein ya kuwaombea mafunzo hayo kwa kuongeza ufanisi katika shughuli zao ili waoneshe tafauti ya kabla ya mafunzo na uwezo wao baada ya mafunzo hayo.

Alisema kuwa kutokana na umhimu wa mafunzo hayo pamoja na lengo la kuleta ufanisi na kuwapa washiriki taaluma ya mambo mbali mbali Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi iliongeza muda wa mafunzo kutoka wiki tatu kama ilivyokuwa mwaka jana hadi mwezi mmoja.

Alieleza kuwa uamuzi huo umewapa washiriki wa mafunzo hayo muda mrefu zaidi wa kupata mafunzo kwa kina na kujifunza mambo mengi kuliko wale waliopata mafnzo hayo kabla.

Pia, alieleza haja ya mafunzo hayo kufanyika hapa Zanzibar kwani imewajumuisha watendaji wengi kuliko ingefanyika nchini China ambapo fursa hiyo wasingeliipata wote.

Katibu Mkuu huyo alitoa shukurani kwa uongozi wa Taasisi ya “China National Research Institute of Food and Fermentation Industries Corpoation Ltd” kwa kukubali kuongeza muda wa mafunzo kama ilivyoombwa.

Aliwapongeza washiriki wa mafunzo hayo kwa kushiriki vyema kwa umakini, kujituma na kuonesha nidhamu katika kipindi chote cha mafunzo hayo na kuwapongeza kwa mwenendo huo kwani ni kielelezo cha kutambua umuhimu wa mafunzo na kulinda heshima ya taasisi zao.

Aliwataka washiriki hao waendelee kuudumisha mwenendo huo ili iwe chachu ya kupata ufanisi zaidi katika kuimarisha Utumishi wa Umma huku akitumia fursa hiyo kutoa shukurani kwa Mkufunzi Mwelekezi Mwalimu Abdalla Mohamed kutoka Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali ambaye amekuwa kiungo muhimu kati ya wakufunzi na washiriki wa mafunzo.

Aidha, alitoa shukurani za pekee kwa Uongozi wa Taasisi ya Utalii iliyo chini ya  Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA), na Uongozi wa Hoteli ya Verde kwa kuruhusu kutumika kwa maeneo yao katika kufanikisha mafunzo hayo.

Kwa niaba ya uongozi na watendaji wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Katibu Salum aliahidi kuendelea kuchukua hatua mbali mbali za kuwapatia mafunzo ya muda mrefu na muda mfupi watumishi ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao.

Katibu Mkuu huyo pia, alitumia fursa hiyo kutoa shukurani maalum kwa juhudi zinazoendelea kuchukuliwa na Balozi Mdogo wa Jamhuri ya Watu wa China aliyepo Zanzibar Xie Xiaowu pamoja na wafanyakazi wake kwa juhudi zao katika kuimarisha uhusiano uliopo baina ya China na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwemo Zanzibar.

Sambamba na hayo, Katibu Mkuu huyo alitoa shukurani kwa uongozi na wakufunzi kutoka Jamhuri ya Watu wa China kwa kuendelea kutoa mafunzo kwa wafanyakazi wa hapa nchini na kuahidi kuendeleza ushirikinao kwa manufaa ya wananchi wa pande mbili hizo.

“Naomba wakufunzi wetu muichukulie Zanzibar kuwa ni nchi yenu ya pili na msisite kurudi tena, fursa nyengine ya kufanya hivyo itakapojitokeza”,alisisitiza  Katibu Mkuu Salum.

Nae Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya “China National Research Institute of Food and Fermentation Industries Corporation Ltd” Bwana Dong Jianhui alitoa shukurani Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa kuratibu na kuandaa mafunzo hayo na kuzishirikisha taasisi nyengine za Serikali pamoja na Binafsi katika mafunzo hayo muhimu.

Aliwapongeza waahitimu wote 45 na kueleza kuwa mafunzo hayo yaliyojumuisha kada mbali mbali zilizojikita na ukarimu na upishi zimeweza kuwajenga vyema na kupata mafunzo yakiwemo ya vitendo ambayo yatawasaidia katika kufanikisha shughuli zao za kazi.

Alisisitiza kuwa Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China kupitia taasisi ya “ China National Research Institute of Food and Fermentation Industries Corporation Ltd” itaendelea kuiunga mkono Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar sambamba na kujenga uhusiano mzuri.
Mapema Mkuu wa Kitengo cha Uchumi na Biashara wa Ubalozi Mdogo wa Jamhuri ya Watu wa China aliyepo Zanzibar  Bibi Shen Qi alieleza kuwa hatua hiyo ni miongoni mwa juhudi za kuendeleza uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo baina ya pande mbili hizo.

Alieleza kuwa kufanyika kwa mafunzo hayo ni njia moja wapo ya kuendeleza uhusiano mwema uliopo na kusisitiza kuwa Jamhuri ya Watu wa China itaendelea kuziunga mkono nchi zote marafiki zikiwemo zinazoendelea katika kuhakikisha zinafikia malengo waliyoyaweka.

Nao washiriki wa mafunzo hayo katika hotuba yao walitoa pongezi za dhati kwa Rais Dk. Shein kwa kufikiria kwa kina na kuiomba Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China kuwaletea mafunzo hayo ya Ukarimu na Mapishi hapa Zanzibar.

Washiriki hao walieleza jinsi walivyofaidika na mafunzo hayo ya mwezi mmoja ambapo walijifunza kwa nadharia na vitendo mambo mbali mbali kupitia kwa wakufunzi wao yakiwemo kumpokea mgeni, kutayarisha chakula na vinyaji, kuhudumia wageni mashuhuri (VIP Services), kumuongoza mgeni wakati wa kumpokea, maamkizi na matumizi sahihi ya lugha katika mazingira tofauti pamoja na mafunzo mengineyo mengineyo.  

Sambamba na hayo, washiriki hao walionesha igizo la kuvutia katika miongoni mwa mafunzo yao waliyoyasoma ndani ya mwezi mmoja kutoka kwa wakufunzi wao.

Wakati huo huo, washiriki hao walishiriki katika chakula maalum cha mchana kilichoandaliwa na Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa ajili ya wahitimu hao  huko katika hoteli ya Verde, Mtoni Mjini Zanzibar.

Mafunzo hayo yaliofungwa leo yalianza Septemba 11, 2019 ambayo yaliwashirikisha watendaji 45 kutoka Taasisi za Serikali na Binafsi wakiwemo kutoka Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Baraza la Mapinduzi, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, Chuo Cha Utalii Maruhubi, Uwanja wa Ndege na Hoteli ya Verde.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.