Habari za Punde

Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mwanamwema Shein Azindua Huduma ya Upimaji wa Afya Kwa Wazee wa Welezo na Sebleni Zanzibar.


MKE wa Rais wa Zanzibar Mama Mwanamwema Shein akishuhudia huduma ya Upimaji wa  Afya kwa Wazee wa Sebleni na Welezo ikitolewa na Daktari Bingwa kutoka Jamuhri ya Watu wa China.Dr.Yang Xiaodong  akimpima presha Bi.Nagawiya Ramadhani,wakati wa uzinduzi huo uliofanyika katika ukumbi wa nyumba za  Wazee Sebleni Wilaya ya Mjini Unguja, (kulia kwa Mama Mwanamwema Shein) Mke wa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar.Mama Asha Suleiman Iddi

MKE wa Rais wa Zanzibar, mama Mwanamwema Shein amesema kwa kuzingatia umuhimu wa wananchi kuwa na afya bora, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeweka kipaumbele katika sekta ya Afya, kwa kuimarisha huduma mbali mbali .

Mama Mwanamwema amesema hayo katika uzinduzi wa huduma za upimaji afya kwa wazee wanaoishi katika nyumba za wazee Sebleni na Welezo, hafla iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano Sebleni, mjini hapa.

Timu ya madaktari bingwa kutoka Jamuhuri ya watu wa China, wakishirikiana na madaktari wazalendo wameendesha zoezi la upimaji wa Afya kwa wazee wanaoishi katika nyumba hizo na kutoa huduma za uchunguzi, dawa na ushauri.

Alisema ili kufanikisha dhamira hiyo, Serikali imechukuwa hatua mbali mbali, ikiwa pamoja na kuimarisha miundombinu, kununua vifaa vya kisasa vya  uchunguzi, kuongeza bajeti ya dawa, kuongeza madaktari pamoja na kusomesha vijana wake ndani na nje ya nchi.

Alisema hivi sasa huduma za za Afya katika hospitali na vituo vya Afya kote nchini zimeimarika  na kutolewa bure , ikiwa ni hatua ya kufanikisha malengo ya muasisi wa Mapinduzi ya Zanzibar, marehemu mzee Abeid Amani Karume.

Alieleza kuwa hatua ya  washirika wa maendeleo, ikiwemo Jamuhuri ya Watu wa China, kuunga mkono juhudi hizo kwa wataalamu wake kupima afya za wazee hapa nchini, ni jambo la kutia moyo na linalopasa kupongezwa.

“Kuwapima afya wazee wetu ni kuendeleza jitihada za kuwaenzi na kuwahudumia wazee wetu, hakika wazee hawa  walifanya kazi ya kutulea na kuijenga nchi yetu, hii ni kuonyesha tunawathamini, tunawajali na tunawapenda”, alisema.

Aliwataka wazee hao kuitumia vyema fursa waliyoipata na kutoa ushirikiano kwa wataalamu hao, ili kufikia malengo yaliokusudiwa.

Aidha,  alitowa wito kwa wazazi na walezi kote nchini kusimamia vyema malezi ya watoto wao kwa kuzingatia maadili mema, utamaduni  na silka za Wazanzibari, ili hatiame waweze kuwa raia wema.

Mama Mwanamwema alisitiza haja ya kuwahimiza watoto kuzingatia masomo yao ya skuli na madrasa pamoja na kuwafuatilia nyendo zao ili kuwaepusha na vitendo viovu, udhalilishaji na matumizi ya dawa za kulevya.

Alitowa shukrani kwa timu hiyo ya madaktari kwa mara ya pili kukubali kutoa huduma za upimaji wa afya, hatua aliyobainisha inaonyesha mapenzi makubwa na urafiki uliopo kati ya wananchi wa China na Zanzibar.

Aidha, mama Mwanamwema alitowa ombi maalum kwa Ubalozi mdogo wa China uliopo Zanzibar akiomba huduma hizo zifikishwa kisiwa Pemba kwa ili wazee wanaoishi katika nyumba za wazee Limbani, nao waweze kufaidika.

Altowa pongezi kwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein kwa kutimiza miaka tisa ya uongozi wake na kubainisha maendeleeo makubwa ya kiuchumi na  kijamii yaliofikiwa.

Mapema, Mke wa Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mama Asha Suleiman Idd, aliwashukuru madaktri hao kwa moyo wao wa kujitolea na kuona umuhimu wa kuwaenzi na kuwahudumia wazee wa Zanzibar.

Aidha, aliishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, chini ya Chama cha Mapinduzi kwa kuwajali na kuwathamini wazee.
  
Nae, Waziri wa Kazi, Uwezeshaji, wazee, wanawake na watoto, Moudline Castico alipongeza juhudi endelevu za Mama Mwanamwema na Mama Asha Suleiman , ambapo kwa nyakati tofauti wamekuwa mstari wa mbele kutoa misada mbali mbali ya kijamii kwa wazee na watoto wanaolelewa katika nyumba za Serikali.

Alisema wazee wamekuwa wakikabiliwa na magonjwa mbali mbali, ikiwemo sukari, shinikizo la damu, kiharusi, macho, masikio na mengineyo, hivyo akabainisha hatua ya Ubalozi wa China kuedesha zoezi hilo kuwa ni ya kupongezwa.

Alimpongeza Mke wa Balozi mdogo wa Jamuhri ya Watu wa China Zanzibar.Bi Liu Jie kwa juhudi kubwa alizochukuwa kufanikisha kazi ya kuwapima afya wazee, hatua aliyoeleza inayonesha imani na mapenzi kwa wazee hao.

Aidha, Mke wa Balozi mdogo wa China aliopo Zanzibar, Liu Jie aliipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, chini ya uongozi wa Dk. Shein kwa juhudi mbali mbali inazozichukuwa kudumisha amani na kuimarisha uchumi.

Alisema China itaendelea kuiunga mkoni Zanzibar katika dhamira  zake za kuimarisha uchumi, sambamba na kuendeleza mashirikiano yaliopo kati ya nchi mbili hizo.

Alisema ushirikiano kati ya China na Zanzibar ni wa kihistoria, hivyo akaahidi kuendelezwa na kubainisha upimaji wa afya kwa wzee hao ni hatua inayoonesha heshima na upendo.

Nao, wazee mbali mbali waliopatiwa huduma hizo, wameishukuru Serikali, Ubalozi mdogo wa China pamoja na Mke wa Rais wa Zanzibar kw akufanikisha zoezi hilo muhimu.

Wamesema wamefurahishwa kupata fursa hiyo, kwani imemwawezesha kueleeza changamoto mbali mbali za maradhi yanayowakabili na kuchunguzwa na hatiame kupata dawa na ushauri wa kitaalamu.

Katika hafla hiyo Mke wa Balozi wa China aliopo nchini Bi Liu Jie aliikabidhi zawadi na vifaa mbali mbali kwa wazee wanaoishi nyumba za wazee Welezo na Sebleni.
Nyumba za kutunzia wazee ziliopo  Welezo na Sebleni zina jumla ya wazee 71 wa kike na kiume, ambao hupatiwa huduma zote muhimu, ikiwemo Chakula, malazi, matibabu na Serikali.

Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 
 E-mail: abdya062@gmail.com

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.