Habari za Punde

Mtakwimu Mkuu wa Serikali: Tayari Kuendelea Kushirikiana Kuandaa Takwimu za Mazingira na Mabadiliko ya Tabianchi

Na.Mwandishi Wetu                                                                                                                         
Serikali imewahakikishia wadau kuwa iko tayari kuendelea kutoa ushirikiano unaohitajika katika uandaaji wa takwimu bora za mazingira na mabadiliko ya tabianchi.
Mtakwimu Mkuu wa Serikali Dkt. Albina Chuwa alieleza hayo wakati alipokuwa akifungua warsha ya siku moja ya kuhariri Ripoti ya Kitaifa ya Takwimu za Mabadiliko ya Tabianchi ya mwaka 2019 iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) jijini Dodoma.
Warasha hiyo ambayo iliratibiwa na kufadhiliwa na Ushirikiano wa Kimataifa wa Takwimu kwa Maendeleo Endelevu (GPSDD), Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEP) na Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Serikali ya Ujerumani (GIZ) ilijumuisha Wadau wa takwimu za mabadiliko ya tabianchi wa ndani na nje.
Katika hotuba yake ambayo ilisomwa kwa niaba yake na Kaimu Mkurugenzi wa Fedha, Utawala na Masoko Andrew Ulindula, Mtakwimu Mkuu wa Serikali alisifu ushirikiaono mzuri uliopo kati ya NBS na wadau wa takwimu na kueleza kuwa Ripoti ya kwanza ya Takwimu za mabadiliko ya tabianchi ya mwaka 2019 ni miongoni mwa matokeo ya ushirikiano huo.
“Ushirikinao huu ni dhahiri kuwa unaunga mkono jitihada na mipango mbalimbali ya Serikali ya usimamizi wa hifadhi ya mazingiza na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi” alieleza Dkt. Chuwa.
Alibanisha kuwa pamoja na ripoti hiyo kuwa ni ya kwanza kutolewa nchini lakini ni ya aina yake kwa kuwa imeandaliwa kwa kutumia takwimu za kiutawala kama chanzo kikuu cha takwimu hizo.
Dkt. Chuwa alifafanua kuwa Takwimu za Kiutawala zimetawanyika kwenye Wizara, idara na Wakala mbalimbali za Serikali na kwa wadau wengine nje ya Serikali hivyo huleta ugumu kwa watumiaji kuzipata kwa urahisi na kwa wakati.
“Hali hii huleta ugumu wa kufanya uchambuzi wa hali ya mazingira kwa kipindi cha muda mrefu, uchambuzi ambao ni muhimu ili kuweza kubaini picha halisi ya mwenendo wa mabadiliko ya kimazingira hasa mabadiliko ya tabianchi” Dkt. Chuwa alisema.
Kwa hivyo, kukamilika kwa ripoti hii kutawarahisishia watumiaji wa takwimu ikiwemo serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo kuzipata kwa wakati na utimilifu wake.
Mtakwimu Mkuu wa Serikali aliwataka washiriki wote kuhakikisha kuwa wanaijadili ripoti hiyo kwa kina ili iwe na ubora unaokusudiwa na kukidhi matumizi ya wadau mbalimbali kwenye upangaji, ufuatiliaji  na ufanyaji tathmini ya mipango mbalimbali ya hifadhi ya mazingira nchini, hasa katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na athari zake.
Akizungumza kwenye warsha hiyo mwalikilishi wa UNEP kutoka Ofisi ya Nairobi Bi. Diana Ngina alieleza kuwa Ofisi yake imetiwa moyo sana na Tanzania kupitia NBS kwa namna ilivyo mstari wa mbele katika kuandaa Takwimu za mazingira na mabadiliko ya tabianchi hivyo kuziba pengo lililopo ya Takwimu za aina hiyo.
“Ripoti hii iwe mwanzo mzuri… iwe mfano wa nchi nyingine kujifunza kutoka kwenu ili nao watamani kufikia pale Tanzania ilipofikia” alieleza Diana na kuipongeza NBS kwa kutoa ripoti hiyo na kuitaka kuendelea na ari hiyo hiyo ili kutoa ripoti nyingi za aina hiyo.
Kwa upande wake, mwakilishi wa Ushirikiano wa Kimataifa wa Takwimu kwa Maendeleo Endelevu Karen Bett alisema taasisi yao imefarijika kuona Tanzania imeweza kutoa ripoti hiyo kwa kutumia vyanzo vya takwimu za kiutawala.
“Kwa kuweza kutoa ripoti hii maridhawa kwa kutumia vyanzo vya takwimu za kiutawala inadhihirisha umuhimu wa takwimu za kiutawala katika kuzalisha takwimu rasmi. Kilicho muhimu ni Takwimu hizo sasa kutumika katika kupanga sera na mipango yetu kuboresha hali za maisha ya watu wetu ambao wengi wanakumbana na athari za mabadiliko ya tabianchi” alisisitiza Karen. 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.