Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, Azungumza na Ujumbe wa Madaktari wa Chama Cha Wapatholijia Tanzania (APT) Ikulu Jijini Zanzibar leo.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein akizungumza na Ujumbe wa Madaktari  wa Chama Cha Wapatholojia Tanzania (APT) walipofika Ikulu Zanzibar kwa mazungumzo,( kulia kwa Rais) Mwenyekiti wa Chama Cha Wapatholijia Tanzania Dkt. Charles Massambura akiwa na ujumbe wake.  wakiwa Zanzibar kwa ziara ya siku mbili hafla imefanyika leo 1/11/2019 Ikulu  Jijini Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameahidi kuendelea kushirikiana na Wapatholojia wote nchini na kusisitiza haja ya kuwatunza na kuwalea kutokana na umuhimu mkubwa wa fani yao.

Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo Ikulu mjini Zanzibar wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Wajumbe wa Chama cha Wapatholojia Tanzania (APT), ambao wako Zanzibar kwa ziara maalum ya siku mbili kufuatia mwaliko wa Rais Dk. Shein.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein alisema kuwa Wapatholojia wana umuhimu mkubwa katika Taifa hili kutokana na kazi kubwa wanayoifanya ikiwemo kutoa huduma, kufundisha pamoja na kufanya tafiti mbali mbali hivyo, ni vyema wakapewa heshima maalum.

Rais Dk. Shein ambaye pia, ni mlezi wa Chama Cha Wanapatholojia Tanzania (APT), alisema kuwa nia yake ni kuhakikisha chama hicho kinaendelea kuwa madhubuti na kupelekea vijana wengi kujiunga kwa ajili ya kufikia lengo lililokusudiwa.

Rais Dk. Shein aliahidi kuendelea na utaratibu huo wa kuwaalika viongozi hao wa Chama Cha Wapatholojia Tanzania (APT) akiwa mlezi wa chama hicho na hata pale atakapokuwa si mlezi kwani azma yake ni kuhakikisha wanachama wa chama hicho wanaendelea kuwa wamoja sambamba na kuendeleza misingi ya Patholojia.

Aidha, Rais Dk. Shein alisisitiza haja ya kuwekewa utaratibu maalum wa kuendelea kuwatunza na kuwalea Wapatholojia wa Tanzania huku akieleza juhudi alizozichukua katika kuhakikisha Wapatholoji hawaharakishwi kustaafu na badala yake wanaandaliwa  mazingira mazuri na Serikali ili waendelee kutoa huduma kwa jamii.

Alieleza kuwa juhudi hizo ziliweza kuzaa matunda wakati akiwa Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya uongozi wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati ule Rais Jakaya Mrisho Kikwete na hivi sasa wataalamu hao wanafanya kazi hadi miaka 65.
Aliongeza kuwa juhudi za makusudi zinaendelea kuchukuliwa na Serikali anayoiongoza katika kuhakikisha fani ya Patholojia inaimarika kwa kiasi kikubwa hapa Zanzibar.

Aidha, alieleza kufarajika kwake kwa kuona vijana wanajiunga na chama hicho kwani wataweza kusaidia kwa kiasi kikubwa kuziba pengo la wataalamu hao hapo baadae.

Mapema, Rais wa Chama cha Wapatholojia Tanzania (APT) Dk. Charles Massambura alitoa pongezi kwa Dk. Shein kwa mwaliko wake huo aliowapa viongozi wa chama hicho wa kuitembelea Zanzibar sambamba na ukarimu mkubwa walipewa katika ziara hiyo.

Alieleza kuwa wajumbe wote wa Chama hicho waliofanya ziara yao hapa kuanzia jana 31 Septemba 2019 na kuimalizia leo wamefarajika kwa kiasi kikubwa kutokana na maendeleo makubwa yaliofikiwa na Zanzibar katika sekta mbali mbali za maendeleo.

Aliongeza kuwa katika ziara yao hiyo wameweza kuona mambo mbali mbali ya kimaendeleo ikiwa ni juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Rais Dk. Shein ikiwemo sekta ya afya, utalii, miundombinu, uwekezaji pamoja na huduma zote za kijamii.

Aidha, Rais huyo wa chama hicho cha Wapatholojia alitoa pongezi maalum kwa Rais Dk. Shein kwa kuendelea kushirikiana nao tokea walipomchagua kuwa mlezi wa  chama hicho mwaka 2014 na kabla ya hapo ambapo alikuwa nao bega kwa bega katika kuhakikisha chama hicho kinaimarika na kinaleta manufaa kwa Taifa.

Sambamba na hayo, wataalamu hao walieleza kufarajika kwao na hatua za Serikali zinazochukuliwa chini ya uongozi wa Rais Dk. Shein za kujenga Hospitali ya kisasa ya Rufaa na kufundisia huko Binguni, Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja na kupongeza huduma zinazokusudiwa kutolewa kupitia ramani na michoro waliyoiona  kwa ajili ya ujenzi huo.

Wataalamu hao walimpongeza Dk. Shein kwa mchango wake mkubwa alioutoa katika kufanikisha mkutano wao wa 10 uliofanyika hapa Zanzibar Septemba 5 mwaka huu akiwa ni mmoja wa waanzilishi wa Chama hicho kilichoanzishwa katika mwaka 1991.

Mnamo Septemba 5, 2019 Rais Dk. Shein wakati akifungua mkutano wa 10 wa Jumuiya ya Wapatholojia Tanzania (APT), uliofanyika hapa Zanzibar aliwapongeza Wapatholojia hao kwa uwamuzi wao wa kufanya mkutano wao hapa Zanzibar na kuwakaribisha kuitembelea Zanzibar wakati wowote.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.