Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.MheDk. Ali Mohamed Shein Azungumza na Rais wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binaadam na Watu Ikulu Jijini Zanzibar.


Rais  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akimsikiliza mgeni wake (kulia) Rais wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binaadamu na Watu.Mhe. Jaji Sylvain Ore, akiwa na Ujumbe wake wa Majaji, walipofika Ikulu Zanzibar kwa mazungumzo leo.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza kuwa Zanzibar imeweza kupiga hatua kiuchumi, kijamii na kisiasa kutokana na ushirikiano wa Mihimili yake mikuu mitatu ambayo ni Serikali, Mahakama na Baraza la Wawakilishi.

Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo wakati alipofanya mazunguzo na Rais wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binaadamu na Watu Jaji Sylvain Ore aliyefika Ikulu mjini Zanzibar akiwa amefuatana na ujumbe wa Majaji wa Mahakama hiyo.

Katika mazungumzo hayo, Rais Dk. Shein alisema kuwa Zanzibar imeweza kupiga hatua kwa kiasi kikubwa hali ambayo imepelekea kukuza na kuimarisha amani na utulivu na umoja  uliopo kutokana na mashirikiano mazuri wa mihimili hiyo.

Rais Dk. Shein alimueleza Rais huyo wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binaadamu na Watu kuwa mafanikio hayo makubwa ya kimaendeleo yameweza kufikiwa hapa Zanzibar kutokana na mihimili hiyo mitatu mikubwa kutoingiliana katika kazi zao na badala yake kuweza kushirikiana pamoja.

Alieleza kuwa kila muhimili kati ya mihimili hiyo mitatu mikuu ya Zanzibar imekuwa ikifanya kazi zake bila ya kuingiliwa na muhimili mwengine hatua ambayo imezidisha mashirikiano na kuendelea kuipa sifa kubwa Zanzibar ndani na nje ya nchi.

Rais Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo pamoja na ujumbe wake kuwa kipaumbele kikubwa kilishowekwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kuhakikisha amani, utulivu na umoja uliopo vinadumishwa na kuendelezwa kwa nguvu zote ikiwa ni pamoja na kutekeleza azma ya Dira ya 2020.

Aliongeza kuwa Zanzibar imeweza kupata mafanikio katika kutilia mkazo suala zima la haki za binaadamu na watu hali ambayo imepelekea Zanzibar kuimarika kiuchumi, kijamii na kisiasa.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kutoa ushirikiano wake kwa Mahakama hiyo na kupongeza wazo zuri la kuja kufanya mkutano wao hapa Zanzibar hasa kwa kutambua kuwa Zanzibar ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Rais Dk. Shein aliwakaribisha viongozi hao Zanzibar na kuwaeleza kuwa Zanzibar iko salama na hivi sasa inaendelea kuwa kivutio kikubwa cha watalii kutoka pande zote za dunia.

Aidha, Rais Dk. Shein aliwaeleza viongozi hao kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaendelea kuweka mazingira mazuri kwa wawekezaji wanaotaka kuja kuekeza Zanzibar.

Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kumpongeza Rais wa Mahakama hiyo Sylvain Ore kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binaadamu  na Watu huku akimtakia yeye pamoja na ujumbe wake mkutano mwema ulioanza Novemba 4 hadi 29 na ule utakaoanza Disemba 2 hadi Disemba 6.

Sambamba na hayo, alimkaribisha Zanzibar yeye na ujumbe wake na kuwataka kuitembelea Zanzibar kwani ina vivutio vingi vikiwemo vile vya kitalii. 

Nae Rais wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binaadamu na Watu Jaji Sylvain Ore alimpongeza Rais Dk. Shein kwa mafanikio makubwa yaliopatikana Zanzibar ikiwa ni pamoja na kuweko mazingira mazuri ya amani,utulivu pamoja na misingi ya sheria na haki za binaadamu.

Jaji Ore alieleza kuwa Zanzibar ni sehemu ambayo imekuwa ikiwavutia watu wengi kuja kuitembelea kutokana na vivutio vingi vilivyopo lakini kivutio kimoja wapo kikubwa ni kuwepo kwa amani na utulivu.

Sambamba na hayo, kiongozi huyo alipongeza hatua kubwa ya maendeleo iliyofikiwa Zanzibar na kusisitiza kuwa mafanikio hayo yametokana na kufuata misingi ya Haki za Binaadamu na Utawala Bora.

Alieleza kuwa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binaadamu na Watu yenye Makamo Makuu yake Arusha nchini Tanzania imekuwa ikifanya kazi kubwa katika kuhakikisha inatekeleza vyema matakwa kwa nchi za Umoja wa Afrika (AU).

Aliongeza kuwa mahakama hiyo imeweza kufanikiwa katika kuendesha programu mbali mbali zinazolenga kutoa elimu ya uwepo wake pamoja na shughuli zake katika nchi mbali mbali za bara la Afrika.

Kiongozi huyo alieleza kuwa uwepo wao hapa Zanzibar unaenda sambamba na vikao mbali mbali vya Mahakama hiyo ikiwa ni pamoja na Kikao cha 10 cha dharura cha mahakama hiyo kitakachoanza Disemba 2 hadi Disemba 6 mwaka huu.

Pamoja na hayo, viongozi hao wanatarajiwa kuwa na kikao ambacho kitatoa elimu juu ya uendeshaji wa mahakama na utoaji wa hukumu zikiwemo hukumu za wazi kikao kitakachowahusisha Mawakili na Majaji mbali mbali ambapo pia, wananchi nao watapata fursa ya kushiriki na kutoa maoni yao pamoja na changamoto walizonazo.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.