Habari za Punde

Takwimu Rasmi Zatajwa Kuchochea Ufanisi wa Miradi

Mtwakwimu Mkuu wa Serikali.Dkt. Albina Chuwa akisisitiza kuhusu ushirikiano mzuri uliopo kati ya Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) na Benki ya Dunia, hayo yamejiri Oktoba 31, 2019 Jijini Dodoma wakati wa kikao cha ujumbe huo na menejimenti ya NBS ilikufanikisha Mpango Kambambe wa Taifa wa Kuboresha na Kuimarisha Takwimu (TSMP) awamu ya pili.
Na. Mwandishi Wetu
Serikali ya Awamu ya Tano imetajwa kufanikiwa katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo kutokana na matumizi bora ya takwimu zinazozalishwa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS).

Akizungumza leo Jijini Dodoma, Mtakwimu mkuu wa Serikali Dkt. Albina Chuwa amesema kuwa Ofisi hiyo imefanikiwa kuzalisha takwimu zenye ubora wa viwango vinavyokubalika kimataifa hali inayochochea mafanikio ya miradi inayotekelezwa ikilenga kuchochea ustawi wa wananchi.

“Tunatarajia kujenga Ofisi katika mikoa yote hapa nchini ili kuboresha zaidi mfumo wa ukusanyaji takwimu kuiwezesha Serikali kupanga mipango yake kwa ufanisi mkubwa zaidi” Alisisitiza Dkt. Chuwa

Akifafanua  amesema kuwa takwimu bora ni msingi wa maendeleo yaliyofikiwa hapa nchini katika sekta zote zinazolenga kuleta ustawi wa wananchi.

Akizungumzia utekelezaji wa mpango Kabambe wa Taifa wa Kuboresha na Kuimarisha Takwimu (TSMP) awamu ya pili Dkt. Chuwa amesema kuwa unalenga kufanya maboresho zaidi katika ukusanyaji na uchakataji wa takwimu kwa kujenga miundombinu bora zaidi hadi ngazi ya mikoa ikiwemo majengo.

“Lengo namba 17 la Malengo ya Millenia linasisitiza ushirikiano kati ya Serikali na wadau ili kuchochea maendeleo ya wananchi ndio maana tumekuwa na ushirikiano huu na Benki ya Dunia” Alisisitiza Dkt Chuwa

Kwa upande wake mchumi mwandamizi kutoka Benki ya Dunia Bi. Bi Nadia Belhaj Hassine Belghith amesema kuwa Tanzania ni nchi ya kupigiwa mfano kwa maendeleo yaliyofikiwa katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu, afya, miundombinu na nyingine kutokana na matumizi ya takwimu zenye viwango na ubora unaotakiwa.

“Takwimu zinawawezesha wakulima kujua wapi yalipo masoko ya mazao yao hivyo kuchochea maendeleo yao na nchi kwa haraka zaidi” Alisisitiza Bi. Belghith

Akifafanua amesema kuwa takwimu ni msingi na kichocheo cha maendeleo katika Taifa lolote kama ilivyo kwa Tanzania ambayo katika Afrika ni ya pili kwa kuzalisha Takwimu Bora.

Ujumbe wa Benki ya Dunia na Ofisi ya NBS wamekutana Jijini Dodoma kwa wiki moja katika mkutano wa mashauriano wa kuimarisha ushirikiano wao. Katika mkutano huo moja ya masuala yaliyozungumziwa ni kufanikisha utekelezaji wa Mpango Kabambe wa Pili wa Taifa wa Kuboresha na Kuimarisha Takwimu (TSMP II) unaotarajiwa kutekelezwa kwa kipindi cha miaka 5 kuanzia 2019/ 2020 hadi 2024/ 2025 baada ya kumalizika kwa mpango kama huo mwezi Juni mwaka jana.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.