Habari za Punde

UNDP Yatowa Pongezi Kwa Ukuaji wa Uchumi wa Zanzibar Kwa Kasi .

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein akizungumza na Mwakilishi Mkaazi wa UNDP Nchini Tanzania.Bi. Christne Musisi alipofika Ikulu Jijini Zanzibar kuonana na Rais leo, hafla hiyo imefanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar.

SHIRIKA la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Miradi ya Maendeleo (UNDP) limepongeza kasi ya ukuaji wa uchumi wa Zanzibar, chini ya uongozi wa Rais wa Zanzibar  na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein.

Pongezi hizo zimetolewa leo na Mwakilishi Mkaazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Miradi ya Maendeleo (UNDP) nchini Tanzania Christine Musisi wakati alipokuwa na mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein.

Katika mazungumzo hayo, Mwakilishi huyo Mkaazi wa (UNDP), alitoa pongezi hizo kwa Rais Dk. Shein na Serikali anayoiongoza kutokana na kasi kubwa ya ukuaji uchumi sambamba na hatua kubwa za maendeleo zilizofikiwa Zanzibar.

Mwakilishi huyo Mkaazi wa Umoja wa Mataifa alieleza kuwa Katika kipindi cha uongozi wa Rais Dk. Shein Shirika hilo la Umoja wa Mataifa limeona mageuzi makubwa ya kiuchumi na kimaendeleo sambamba na kuimarika kwa utawala Bora.

Aliongeza kuwa Shirika la Umoja wa Maifa linaloshughulikia Miradi ya Maendeleo (UNDP) litaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuendeleza na kuimarisha miradi mbali mbali ya maendeleo ili Zanzibar izidi kupata mafanikio.

Aidha, Mwakilishi huyo Mkaazi wa (UNDP), alieleza kuwa katika uongozi wa Rais Dk. Shein Shirika hilo limeweza kushuhudia mafanikio makubwa ya kiimaendeleo ikiwa ni pamoja na juhudi za kupamba na umasikini na kukuza uchumi chini ya Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini Zanzibar (MKUZA) ukiwemo (MKUZA II) na kuahidi kuuunga mkono (MKUZAIII).

Alieleza kuwa huduma za kijamii zimezidi kuimarika zikiwemo huduma za afya, elimu, maji safi na salama pamoja na huduma nyenginezo sambamba na juhudi kubwa zilizofanyika katika kupambana na maambukizi ya Virusi vya UKIMWI.

Hivyo, Kiongozi huyo alieleza kuwa (UNDP), iko tayari kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha na kuendeleza miradi ya maendeleo ikiwa ni pamoja na kusaidia vipaumbele vyote vilivyowekwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Nae Rais Dk. Shein kwa upande wake alieleza kuwa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Miradi ya Maendeleo (UNDP), ni miongoni mwa Mashirika ya Umoja wa Mataifa (UN) ambalo limekuwa na mashirikiano na kuweza kuiunga mkono Zanzibar kwa muda mrefu.

Hivyo, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kulipongeza Shirika hilo na kueleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na wananchi wake wanafarajika na juhudi kubwa inazozichukua Shirika hilo katika kuhakikisha Zanzibar inazidi kupata mafanikio ya kiuchumi, kijamii na kisiasa.

Rais Dk. Shein aliongeza kuwa uchumi wa Zanzibar umezidi kuimarika kutokana na mashirikiano makubwa kati ya uongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na wananchi wake bila ya kuwasahau washirika wa Maendeleo kama vile Shirika hilo la Umoja wa Mataifa (UNDP).

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza juhudi na mikakati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha na kukuza uchumi wake ikiwa ni pamoja na kuiimarisha sekta ya uwekezaji, viwanda sambamba na kuiendeleza na kuiimarisha sekta ya utalii ambayo inachangia kwa asilimia 27 ya Pato la Taifa la Zanzibar na asilimia 80 ya fedha za kigeni.

Katika mazungumzo hayo, Rais Dk. Shein alieleza kuwa sekta ya utalii imeweza kuimarika kwa kiasi kikubwa ambapo pia, juhudi za makusudi zinaendelea kuchukuliwa katika kuiendeleza sekta hiyo ikiwa ni pamoja na ujenzi wa Hoteli kubwa za kitalii pamoja na kuviimarisha vivutio vlivyopo.

Kwa upande wa uwekezaji, Rais Dk. Shein alimueleza Mwakilsihi Mkaazi huyo wa (UNDP) kuwa Mamlaka ya Ukuzaji wa Vitega Uchumi Zanzibar (ZIPA), imekuwa ikifanya kazi kubwa katika kuhakikisha maeneo huru ya Uchumi yanaimarika na yanafikia yale malengo yaliyowekwa ambapo kwa upande wa Unguja alieleza kuwa eneo la Fumba tayari limeanza kutumika kiuwekezaji huku juhudi zikichukuliwa kwa upande wa eneo la Micheweni huko Pemba.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alieleza kuwa huduma za  kijamii zimezidi kuimarika na miradi yote ya maendeleo imeendelea kupata mafanikio na kueleza kuwa huduma za afya kwa upande wa kupunguza vifo vya akina mama na watoto vimepungua kwa kiasi kikubwa.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alisema kuwa juhudi za makusudi zinaendelea kuchukuliwa katika kuhakikisha Zanzibar inatekeleza azma ya Uchumi Bahari (Blue Economy), ikiwa ni pamoja na kuimarisha viwanda vidogo vidogo, kukuza sekta ya utalii, uvuvi pamoja na sekta nyenginezo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.