Habari za Punde

VIJANA WAPATIWA VYETI VYA MAFUNZO YA KUANDIKA MIRADI NA VSO


Mwenyekii wa Baraza la Vijana Khamis Rashid Kheir(Makoti) akimkabidhi cheti cha mafunzo ya kuandika miradi,yaliyotolewa na (VSO) Mwanachama wa Baraza la Vijana Farashuu Mussa  huko katika Ukumbi wa Baraza la Sanaa Mwanakwerekwe   
Mwenyekii wa Baraza la Vijana Khamis Rashid Kheir (Makoti)akitoa maelezo kwa vijana juu  ya mafunzo ya mradi unaojitolea kuwasaidia vijana ( VSO). huko katika Ukumbi wa Baraza la Sanaa Mwanakwerekwe 
Kiongozi wa Baraza la Vijana Salum Issa Ameir akiwasisitiza  vijana kufanya kazi  baada ya kupata mafunzo ya kuandika mradi yaliotolewa na  mradi unaojitolea kuwasaidia vijana ( VSO). huko katika Ukumbi wa Baraza la Sanaa Mwanakwerekwe 
Picha ya pamoja ya Baraza la Vijana walioshiriki mafunzo ya kuandika miradi na vijana kutoka wilaya mbalimbali za Unguja pamoja na wakufunzi wa mradi  unaojitolea kuwasaidia vijana ( VSO). huko Baraza la Sanaa Mwanakwerekwe 

 Picha na Ali Hamadi Ali -Baraza la Vijana 
Na Khadija Khamis -Maelezo Zanzibar         22/12/2019.
Mwenyekii wa Baraza la Vijana Khamis Rashid Kheir(Makoti) amewataka vijana kuitumia elimu waliopata ya kuandaa miradi mbali mbali ili kupata fursa ya kujiendesha wenyewe na kuepukana na utegemezi .
Kauli hiyo ameitoa huko katika Ukumbi wa baraza la sanaa  Mwanakwerekwe wakati akiwatunuku vyeti vijana kutoka katika wilaya mbali mbali za unguja waliopata mafunzo ya kuwajengea uwezo vijana kujiendesha wenyewe uliofadhiliwa na  mradi unaojitolea kuwasaidia vijana ( VSO).
Alisema kutafuta miradi mbali mbali itawasaidia vijana kuwajengea uwezo na mbinu kiutendaji kwa kupatiwa fedha za miradi kwa wafadhili mbali mbali wa ndani na nje ya nchi  ili kujiwezesha kiuchumi .
Aidha aliwataka vijana kuwa wajasiri wasivunjike moyo haraka  waweze kujiwekea malengo yao ya baadae kwa kufanyakazi  kwa bidii .
“Ushiriki wa Vijana katika kazi ni mdogo kila wilaya tuacheni kutupiana  lawama tujilaumu wenyewe kila fursa zikitokea vijana wanashindwa kujaza namba  jambo ambalo linazorotesha maendeleo, “alisema Mwenyekiti.
Alieleza kuwa cheti ni muhimu sana kutokana na wakati wa sasa huzingatiwa kwamba nchi nyingi za Afrika zinatoa kipaumbele zaidi utaalamu kulingana na cheti sio uzoefu hivyo amewataka vijana waendelee kujiwekea malengo ya kujipatia  elimu ili kuisaidia nchi yao.
Hata hivyo alisema Baraza la Vijana linategemea vijana wao watafanyakazi kwa umahiri na juhudi kubwa ili mafanikio ya kimaendeleo katika kila shehia hadi wilaya yaonekane sio kuanza kuzungumza siasa jambo ambalo litazorotesha ufanyaji wa kazi zao.
Mwenyekiti huyo alisema zaidi ya asilimia 90 za shehia mbali mbali hazifanyi kazi ipasavyo jambo ambalo linalirejesha nyuma Baraza hilo
Nae Mkufunzi wa Mradi wa kujitolea unaosaidia vijana( VSO) Maria Rosalia aliwapongeza vijana hao kwa kuonyesha ushirikiano mkubwa katika zoezi zima la mafunzo hayo jambo ambalo limempa ari ya kuendelea kutoa ufadhili wa mafunzo mengine.
Aliwataka vijana wa kila wilaya kuandaa mipango yao ya miradi kwa kuwaonyesha njia ya  kuwasaidia kuitekeleza ili kuweza kuleta maendeleo endelevu ya dunia .
Nae Mshauri wa Vijana VSO  Abdon Fidelis  alisema ushirikiano wa vijana utasaidia kuigeuza sauti ya vijana isikike katika kujitetea na kujipatia haki zao .
Aidha alisema wataendelea kulisaidia  Baraza la Vijana kutokana na miradi mbali mbali ambayo wanaitarajia kuisimamia kutoka VSO ikiwemo afya na mazingira katika wilaya tofauti za Zanzibar.
Kwa upande wa vijana waliopatiwa mafunzo hayo Mosi Fumu Khamis alitoa shukrani zake kwa niaba ya wenzake kuishukuru VSO kwa kuwajengea uwezo wa kitaalamu jambo ambalo litawasaidia kujipatia fursa mbali mbali katika wilaya zao ili kujiletea maendeleo na kujikwamua na umasikini .
Alisema elimu hii itawasaidia kufanyakazizao  kwa mashirikiano ya pamoja na kujipatia kipato, kuepukana na utegemezi kuepukana na kujishirikisha katika vikundi viovu .
Zaidi ya wanafunzi 21 walishiriki mafunzo ya kuandaa miradi kutoka katika wilaya mbali mbali za unguja yalioendeshwa na Wakufunzi kutoka katika mradi wa VSO .

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.