Na. Eric Msuya- MAELEZO
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Dkt.
John Pombe Magufuli anatarajia kuwa mgeni rasmi katika uzinduzi wa Wiki ya
Sheria na Siku ya Sheria itakayofanyika
katika Jiji la Dodoma.
Akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dar es
Salaam Jaji Mkuu wa Tanzania Prof. Ibrahim Juma, amesema lengo la wiki na siku
ya Sheria ni kuwawezesha wananchi kupata uelewa wa sheria na pia kushabihisha
mwelekeo wa Serikali ya Awamu ya Tano wa kukuza viwanda na uwekezaji, ambapo
kauli mbiu ya mwaka huu ni
“UWEKEZAJI NA
BIASHARA: WAJIBU WA MAHAKAMA NA WADAU KUWEKA MAZINGIRA WEZESHI YA UWEKEZAJI”.
Prof. Juma amesema kabla ya mwaka mpya wa Mahakama kuanza, huazimisha wiki ya Sheria na siku ya Sheria ilikuwafanya
wadau wa Sheria na wananchi kwa ujumla kupata uelewa juu ya masuala ya Sheria
na Elimu ya Mahakama kwa ujumla.
“Kwa mwaka huu wa 2020 wiki ya Sheria itaanza tarehe 31
January, hadi Februari 5 katika viwanja vya Nyerere Square Mjini Dodoma, aidha
kilele cha wiki ya Sheria ambayo ni siku ya sheria nchini itafanyika Februari 6
mwaka huu siku ya Alhamisi katika kiwanja cha Jengo jipya la Mahakama Kuu ya
Kanda ya Dodoma”Alisema Prof.Juma.
Aliongeza katika kuipamba wiki hiyo, kutakuwa na maonyesho ya wiki
nzima ya utoaji wa elimu juu ya Sheria yatakayofunguliwa siki ya tarehe moja
Februari kwa maandamano yatakayoanzia
katika Mahakama Kuu kanda ya Dodoma na kuishia kwenye viwanja vya Nyerere
Square.
Aidha, Jaji Mkuu amewataka watanzania kujitokeza kwa wingi
katika matembezi hayo ya wiki ya Sheria yatakayo ongozwa na wadau wa Mahakama
huku mgeni rasmi katika matembezi hayo akitarajiwa kuwa spika wa Bunge Mhe. Job
Ndugai.
“Tunayofuraha kubwa sana kwa mwaka huu wa 2020, kwa mara
nyingine tutajumuika na Mh. Rais ambaye ndio kinara na mtetezi mkuu wa wanyonge
katika kuifanya siku ya sheria nchini kuwa ya kufana” Alisema Prof.Juma.
Amesema katika wiki ya Sheria ni wakati mzuri wa wananchi
kuongeza uelewa na ufahamu wa Sheria na taratibu za kupata haki mahakamani hii
ni kutokana na wananchi wengi kutojua Sheria na taratibu za kimahakama na
kutoelewa lugha ngumu ya kimahama.
“Sambamba na kutoa elimu ya Sheria pia kutatolewa elimu ya
taratibu za ufunguaji wa mashauri, Sheria na taratibu zinazotumika katika kuendesha
mashauri, elimu ya msaada wa kisheria, elimu juu ya mfumo wa TEHAMA katika
uendeshaji wa mashauri na utatuzi wa malalamiko mbalimbali ya wananchi” Alisema
Jaji Mkuu.
Elimu ya sheria katika wiki hiyo, itatolewa na Waheshimiwa Majaji, Wasajili, Naibu Wasajili,
Mahakimu pamoja na wadau wa Mahakama wakiwemo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa
Serikali, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Ofisi
ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Tume ya Haki za Binadamu na utawala bora, Chama cha
Majaji na Mahakimu Wanawake (TAWJA), Polisi, Magereza, pamoja na Chama cha
Wanasheria Tanganyika (TLS).
Sambamba na hilo Jaji Mkuu amewataka wadau na wananchi kutumia mfumo wa TEHAMA wa
kusajili na kuratibu Mashauri Judicial Statistical Dashboard System (
JSDS2) hasa katika karne hii katika utoaji wa haki ambao ulizinduliwa na Rais Magufuli Februari
6, 2019.
“Katika maonesho hayo Mahakama itawasisitiza sana wananchi
kutumia mfumo JSDS2, kwakuwa mfumo huo una faida sana endapo wananchi watelewa utaraibu wa kufungua
shauri na hata kupokea wito wa kuhudhuria shauri kwa njia ya ujumbe mfupi wa
simu (sms notification)” Alisema.
Mahakama pia katika kuimarisha utendaji kwa kutumia mifumo ya
TEHAMA, ina mfumo wa kusoma ramani za mahakama ngazi zote (Judiciary Map-JMAP),
Mfumo wa kutambua mawakili wa kujitegemea wenye leseni (TAMS), Mfumo wa Majina
ya madalali wenye Leseni hai na mfumo wa kuhifadhi hukumu za mahakama (TANZLII).
No comments:
Post a Comment