Habari za Punde

JPM Mgeni Rasmi Wiki ya Sheria Jijini Dodoma


Na. Eric Msuya- MAELEZO
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Dkt. John Pombe Magufuli anatarajia kuwa mgeni rasmi katika uzinduzi wa Wiki ya Sheria na Siku ya Sheria  itakayofanyika katika Jiji la Dodoma.

Akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dar es Salaam Jaji Mkuu wa Tanzania Prof. Ibrahim Juma, amesema lengo la wiki na siku ya Sheria ni kuwawezesha wananchi kupata uelewa wa sheria na pia kushabihisha mwelekeo wa Serikali ya Awamu ya Tano wa kukuza viwanda na uwekezaji, ambapo kauli mbiu ya mwaka huu ni 

UWEKEZAJI NA BIASHARA: WAJIBU WA MAHAKAMA NA WADAU KUWEKA MAZINGIRA WEZESHI YA UWEKEZAJI”.

Prof. Juma amesema kabla ya mwaka mpya wa Mahakama kuanza, huazimisha  wiki ya Sheria na siku ya Sheria ilikuwafanya wadau wa Sheria na wananchi kwa ujumla kupata uelewa juu ya masuala ya Sheria na  Elimu ya Mahakama kwa ujumla.

“Kwa mwaka huu wa 2020 wiki ya Sheria itaanza tarehe 31 January, hadi Februari 5 katika viwanja vya Nyerere Square Mjini Dodoma, aidha kilele cha wiki ya Sheria ambayo ni siku ya sheria nchini itafanyika Februari 6 mwaka huu siku ya Alhamisi katika kiwanja cha Jengo jipya la Mahakama Kuu ya Kanda ya Dodoma”Alisema Prof.Juma.

Aliongeza katika  kuipamba wiki hiyo, kutakuwa na maonyesho ya wiki nzima ya utoaji wa elimu juu ya Sheria yatakayofunguliwa siki ya tarehe moja Februari kwa maandamano  yatakayoanzia katika Mahakama Kuu kanda ya Dodoma na kuishia kwenye viwanja vya Nyerere Square.

Aidha, Jaji Mkuu amewataka watanzania kujitokeza kwa wingi katika matembezi hayo ya wiki ya Sheria yatakayo ongozwa na wadau wa Mahakama huku mgeni rasmi katika matembezi hayo akitarajiwa kuwa spika wa Bunge Mhe. Job Ndugai.

“Tunayofuraha kubwa sana kwa mwaka huu wa 2020, kwa mara nyingine tutajumuika na Mh. Rais ambaye ndio kinara na mtetezi mkuu wa wanyonge katika kuifanya siku ya sheria nchini kuwa ya kufana” Alisema Prof.Juma.

Amesema katika wiki ya Sheria ni wakati mzuri wa wananchi kuongeza uelewa na ufahamu wa Sheria na taratibu za kupata haki mahakamani hii ni kutokana na wananchi wengi kutojua Sheria na taratibu za kimahakama na kutoelewa lugha ngumu ya kimahama.

“Sambamba na kutoa elimu ya Sheria pia kutatolewa elimu ya taratibu za ufunguaji wa mashauri, Sheria na taratibu zinazotumika katika kuendesha mashauri, elimu ya msaada wa kisheria, elimu juu ya mfumo wa TEHAMA katika uendeshaji wa mashauri na utatuzi wa malalamiko mbalimbali ya wananchi” Alisema Jaji Mkuu.

Elimu ya sheria katika wiki hiyo, itatolewa  na Waheshimiwa Majaji, Wasajili, Naibu Wasajili, Mahakimu pamoja na wadau wa Mahakama wakiwemo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Tume ya Haki za Binadamu na utawala bora, Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake (TAWJA), Polisi, Magereza, pamoja na Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS).

Sambamba na hilo Jaji Mkuu amewataka  wadau na wananchi kutumia mfumo wa TEHAMA wa kusajili na kuratibu Mashauri  Judicial Statistical Dashboard System ( JSDS2) hasa katika karne hii katika utoaji wa haki  ambao ulizinduliwa na Rais Magufuli Februari 6, 2019.

“Katika maonesho hayo Mahakama itawasisitiza sana wananchi kutumia mfumo JSDS2, kwakuwa mfumo huo una faida sana  endapo wananchi watelewa utaraibu wa kufungua shauri na hata kupokea wito wa kuhudhuria shauri kwa njia ya ujumbe mfupi wa simu (sms notification)” Alisema.

Mahakama pia katika kuimarisha utendaji kwa kutumia mifumo ya TEHAMA, ina mfumo wa kusoma ramani za mahakama ngazi zote (Judiciary Map-JMAP), Mfumo wa kutambua mawakili wa kujitegemea wenye leseni (TAMS), Mfumo wa Majina ya madalali wenye Leseni hai na mfumo wa kuhifadhi hukumu za mahakama (TANZLII).

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.