Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein Afungua Daraja la Dk.Ali Mohamed Shein Kibonde Mzungu Barabara ya Fuoni leo Ikiwa ni Shamrashamra za Sherehe za Mapinduzi ya Zanzibar.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein akiwapungia mkono Wananchi wa Kijiji cha Kibondemzungu wakati wa hafla ya ufunguzi wa Daraja la Dk.Ali Mohamed Shein Kibondemzungu barabara ya Fuoni Wilaya ya Magharibi "B" Unguja akipita katika daraja hilo baada ya kulifungua, (kushoto kwa Rais) Waziri wa Ujenzi Mawasiliano na Usafirishaji Zanzibar.Mhe. Dkt, Sira Ubwa na Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar Zuberi Ali Maulid na (kushoto kwa Rais) Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi Mawasiliano na Usafirishaji Zanzibar Ndg. Mustafa Aboud Jumbe.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa ujenzi wa barabara na daraja la Kibonde Mzungu ni uthibitisho wa Mapinduzi kwani kabla ya Mapinduzi hapakuwepo madaraja na barabara nzuri kama zinazojengwa hivi sasa hapa Zanzibar.

Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo katika hotuba yake aliyoitoa katika hafla ya ufunguzi wa Daraja la Kibonde Mzungu, lililopewa jina “Daraja la Dk. Shein”, liliopo Wilaya ya Magharibi B, Mkoa wa Mjini Magharibi, hafla iliyofanyika eneo hilo la Kibonde Mzungu ikiwa ni shamrashamra za miaka 56 ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Aliongeza kuwa wakati huo daraja kubwa hapa Zanzibar lilikuwa ni daraja la Tingatinga lililopo Kaskazini Unguja ambalo halikuwa na sifa wala vigezo kama madaraja na barabara zinazojengwa hivi sasa ambazo zina ubora kwa wananchi kwa  ajili ya usarifi wao na bidhaa zao.

Alisema kuwa baada ya Mapinduzi ya Januari 12, 1964 kila kitu kilishamiri zikiwemo barabara, nyumba na mambo mengineyo., “lakini hivi sasa tunachokitaka wenyewe tunajenga, na mimi nataka nikukumbusheni ujenzi wa daraja hili mara tu baada ya kulitembelea mnamo mwaka 2017 yalipotokea mafuriko na kuamuru kujengwa”.

“Nilisema tujengeni daraja kubwa la kisasa hapa, daraja liwepo tena liwe kubwa na zuri na leo limejengwa na kila mtu analiona”. Alisisitiza Dk. Shein.

Katika hafla hiyo,  Rais Dk. Shein alieleza kwa ufupi historia ya Mapinduzi ya Januari 12, 1964 na kueleza juhudi zilizochukuliwa katika kuhakikisha wanyonge wa Zanzibar wanakuwa huru sambamba na kuimarika kwa sekta za maendeleo zikiwemo barabara.

Rais Dk. Shein alisema kuwa Mapinduzi yataendelea kusemwa kila siku kwani ni jambo ambalo lina maslahi ya wananchi wote licha ya kuwepo baadhi ya watu ambao hawapendi kuyataja, kuyazungumza wala kuyasikia.
Alisema kuwa Mapinduzi yalikuwa ni lazima yafanywe na yatokee kutokana na dhulma zilizokuwepo Zanzibar kutoka kwa watawala wa Kigeni wa Kisultani na Kiengereza hatua ambayo ilipelekea kuanza kwa vuguvugu la Mapinduzi na hadi uhuru kupatikana.

Alisema kuwa uchumi wa Zanzibar ulihodhiwa na Wakoloni hao ikiwemo elimu, afya na sekta nyenginezo na mnyonge alikuwa hana maana wala hawezi kufanya starehe za aina yoyote na badala yake kulikuwa na mipaka na mahala pa kushereheka na muda maalum pamoja na saa maalum za kufanya starehe.

Rais Dk. Shein pia, alisema kuwa Mapinduzi ya Januari 12, 1964 nchi zote duniani ziliyatambua hasa kwa malengo yake ya kujenga umoja wa watu wa Zanzibar, kujenga mshikamano na maelewano, amani sambamba na kuondosha ubaguzi.

Alisema kuwa hatua hiyo ilipelekea kutungwa kwa Sheria ya mwanzo ya Rais, Sheria  Namba 6, iliyotiwa saini mnamo tarehe 25 Februari mwaka 1964 ambapo katika uongozi wa Rais Karume kila kitu kiliongozwa kwa sheria na taratibu za nchi.

Alisema kuwa wakoloni hawakujenga chochote kwani tokea wakati huo Kibonde Mzungu ilikuwepo na Wakoloni walikuwepo lakini hawakujenga barabara wala daraja kama hilo na badala yake waliimarisha usafiri katika maeneo ya Mji Mkongwe pamoja na kujenga treni katika eneo la mjini pekee.

Alisema kuwa ndani ya miaka 56, kumefanywa mambo mengi na Zanzibar sivyo ilivyo leo huku akisisitiza kuwa kila fedha zitakaporuhusu, zitajengwa barabara hata barabara za juu (Fly-over).

Alisisistiza haja kwa Serikali kuanza utaratibu wa kujenga barabara za juu (Fly-over) kwani tayari ameshatoa agizo kwa Wizara hiyo kutafuta jibu la ujenzi wa barabara hiyokuelekea Kaskazini ili iaze wapi kwani ni lazima Serikali ifanye.

Rais Dk. Shein aliitaka Wizara hiyo kuhakikisha mjenzi anayejenga barabara ya kutoka katika daraja hilo mpaka kituo cha Polisi Fuoni akabidhi barabara hiyo mwezi Februari kama ulivyomkataba na kusisitiza kuwa mkataba huo usivukwe.

Aidha, Rais Dk. Shein aliiagiza Idara ya Ujenzi na Utunzaji wa Barabara (UUB) waunganishe barabara inayotokea katika daraja hilo hadi eneo la barabara inayoelekea Koani, kwani wana vifaa vipya, wataalamu wanao huku akisisitiza kuwa ni basi kutoa tenda za ujenzi wa barabara kwa ile barabara wanayoweza kuifanyia kazi.

Alisisitiza kuwa kwamwe haiwezekani Serikali kununua vifaa vya Bilioni 14 halafu kukaanza kutolewa tenda za ujenzi wa barabara zinazowezwa kujengwa na Idara hiyo na kuitaka kujenga wenyewe barabara za Pemba na Unguja na pale zitakapotaka kujengwa barabara kubwa waendelee kutoa tenda lakini kwa ile wanayoweza wafanye wenyewe na waepuke kupigwa changa la macho.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alikubali Daraja hilo kuitwa jina lake na kupokea heshima hiyo na kumpongeza Wazari, katibu Mkuu na wafanyakazi wote wa Wizara hiyo kwa kushirikiana na mkandarasi wa ujenzi huo.

Dk. Shein alieleza haja ya kutiwa taa za barabarani katika eneo hilo kuanzia eneo la Jumbi bango la Mkoa hadi kituo cha Polisi cha Fuoni jambo ambalo limeungwa mkono na Wizara husika na kusema kuwa hayo ni maendeleo kwani barabara kutiwa taa na kujengwa mitaro pembezoni ni jambo muhimu.

Nae Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji  Dk. Sira Ubwa Mamboya alisema kuwa ilikuwa ni changamoto kubwa sana hasa wakati wa mvua na maji yalikuwa yanajaa katika eneo hilo na kusababisha madhara ambapo kwa sasa tatizo hilo limeondoka na litakuwa ni historia na wananchi hivi sasa wanapita usiku na mchana.

Katika maelezo Waziri huyo alisema kuwa ujenzi huo ni utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM na kumpongeza Rais Dk. Shein kwa miongozo yake na kumuhakikishia kuwa watafanya kazi kwa kadri ya uwezo wao katika kuwaletea wananchi wa Zanzibar maendeleo hasa katika sekta ya usafiri.

Waziri Sira aliipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar hasa Mfuko wa Barabara kwa juhudi kubwa zilizochukuliwa katika kuhakikisha daraja hilo linajengwa na barabara hiyo nayo inajengwa na kupitika tena kwa kiwango kizuri na kuwapongeza wale wote waliofanikisha ujenzi huo  huku akiwaomba wananchi wote wa Unguja na Pemba kuzitunza barabara kwani zinagharimu fedha nyingi katika ujenzi wake.

Alisema kuwa barabara zinagharimu fedha nyingi hasa pale zinapoharibika kwa bahati mbaya ama pale zinapoharibiwa kwa makusudi hivyo aliwataka wananchi kuzitunza vizuri.

Sambamba na hayo, Waziri Dk. Sira alisisitiza haja ya kuyaenzi, kuyalinda na kuyadumisha Mapinduzi ya Januari 12, 1964 kwani ndio dira  ya maendeleo..

Hata hivyo, Waziri Dk. Sira alimuomba Rais Dk. Shein kuwa daraja hilo liitwe kwa jina lake Rais Dk. Shein ili iwe kumbukumbu ya wananchi kutokana na juhudi zake alizozichukua katika kuhakikisha tatizo la eneo hilo linapatiwa ufumbuzi.

Mapema Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji, Mustafa Aboud Jumbe alisema kuwa ujenzi wa Daraja la Kibonde Mzungu ni miongoni mwa jitihada zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuwaondolea wananchi changamoto mbali mbali za usafiri wananchi wa Unguja na Pemba.

Alisema kuwa ujenzi huo ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020 kama ilivyoelekezwa kwenye ukurasa wa 138 Sura ya 88 kilichoeleza kuwa “Serikali itaendelea na kazi ya utunzaji na matengenezo ya barabara zilizokwisha kujengwa na kufanya marekebisho katika maeneo yanayotuama maji ya mvua na kuathiri ubora wa barabara hizo”.

Katibu Mkuu huyo alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ilifanya uamuzi wa kulijenga daraja katika eneo hilo la Kibonde Mzungu kutokana na athari zilizokuwa zinajitokeza kila wakati wa mvua kwa kutuwama kwa maji mengi ambayo yalipelekea kufungika barabara na kushindwa kutumika.

Aidha, alisema kuwa kutokana na hali hiyo, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ilifanya maamuzi ya kulitafutia ufumbuzi wa kudumu sehemu ya Kibonde Mzungu kwa kujenga Daraja kubwa ambalo litaweza kuondoa changamoto iliyokuwepo.

Aliongeza kuwa ujenzi wa daraja hilo ni sehemu ya ujenzi wa barabara ya Mkunazini-Kariakoo-Magomeni-Fuoni-Tunguu yenye urefu wa kilomita 16.76 ambao ujenzi wake unakwenda awamu kwa awamu ambapo pia, ni barabara ambazo zimo katika Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2015-2020.

Alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji mnamo tarehe 31 Agosti, 2018 ilitiliana saini Mkataba wa ujenzi wa daraja hilo na Kampuni ya Mwananchi Engineering Construction Company (MECCO) kwa ajili ya ujenzi huo.

Kwa maelezo ya Katibu Mkuu huyo alisema kuwa mradi huo hadi kukamilika kwake umegharimu jumla ya TZS Bilioni 4.319 fedha ambazo zimetolewa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Mfuko Mkuu wa Hazina uliochini ya Wizara ya Fedha na Mipango Zanzibar.

Pia, Katibu Mkuu huyo alisema kuwa Wizara hiyo inaendelea na ujenzi wa barabara kutoka Kibonde Mzungu hadi Fuoni Polisi yenye urefu wa mita 1.2 kazi ambayo inafanywa na Kampuni hiyo ya MECCO na inatarajiwa kukamilika mwezi Februari, 2020.
Rais wa 
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.