Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa kwanza wa Kamati ya Mawaziri wenye dhamana ya Menejimenti ya Maafa kwa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini Mwa Afrika (SADC) uliofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Madinat Al Bahr Mbweni Jijini Zanzibar.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein ameitaka Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kuwa
na mipango na mikakati ya kupambana na maafa hasa yale yanayotokea mara kwa
mara.
Rais Dk. Shein
aliyasema hayo leo katika hotuba yake wakati akifungua Mkutano wa Kwanza wa
Kamati ya Mawaziri wenye Dhamana ya Menejimenti ya Maafa kwa Nchi Wanachama wa
Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) unaofanyika katika Hoteli ya
Madinat Al Bahr nje kidogo ya Jiji la Zanzibar.
Alieleza kuwa kwa
kuzingatia athari za maafa zinazogharimu maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika
nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) ni lazima jumuiya hiyo ikajipanga
vizuri kwa kuandaa mikakati imara ya kuvitambua na kuviwahi viashiria vipya vya
maafa kila vinapoanza kujitokeza.
Hivyo, Rais Dk. Shein
alieleza kuwa Kamati hiyo ina nafasi ya kutoa maelekezo na mapendekezo juu ya
nini kifanyike kwa ngazi ya kitaifa na kikanda ili kuweza kujikinga na maradhi
mapya yaliyoingia ya Virusi vya Corona (Covid-19) ambayo tayari yameshaenea
katika nchi mbali mbali duniani.
Aidha, alieleza kuwa
changamoto ya nzige iliyojitokeza hivi karibuni katika ukanda wa Afrika
Mashariki, ambao wanaweza kuathiri kwa kiasi kikubwa sekta ya kilimo na usalama
wa chakula katika baadhi ya nchi ni suala ambalo linahitaji kuzungumzwa na
kupangiwa mikakati ya pamoja.
“Wahenga wanasema
tahadhari kabla ya athari, naamini kwamba haya ni miongoni mwa majukumu ya
Kamati hii inayoshughulika na masuala ya maafa”,alisisitiza Rais Dk. Shein.
Katika hotuba yake
hiyo Rais Dk. Shein alimpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.
John Pombe Magufuli ambaye ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya SADC kwa kuendelea
kuiongoza vyema Jumuiya hiyo hatua ambayo imepelekea kupata mafanikio makubwa
sambamba na kuiletea maendeleo endelevu Tanzania.
Rais Dk. Shein alisema
kuwa kufanyika kwa Mkutano huo ni hatua muhimu katika kujenga matumaini mapya
ya wananchi kuhusiana na maafa, kuzingatia kwamba miaka ya hivi karibuni
kumekuwa na ongezeko kubwa la maafa pamoja na viashiria vyake katika nchi
wanachama wa SADC.
Rais Dk. Shein
aliongeza kuwa maafa hayo husababisha upotevu wa maisha, mali za watu na
uharibifu wa miundombinu na hivyo, yanaathiri sana ajenda za maendeleo
zinazopangwa kutekelezwa na nchi wanacha wa SADC.
Kwa maelezo ya Rais
Dk. Shein takwimu za utekelezaji wa “Mkakati wa Sendai” zinaonesha kuwa kati ya
mwaka 2015 na 2018, Ukanda wa SADC umepata zaidi ya matukio 160 ya maafa ambayo
yalisababisha vifo vya watu zaidi ya 20,000 na yameathiri wengine milioni 22.
Kadhalika, Rais Dk.
Shein aliongeza kuwa maafa hayo yalileta uharibifu mkubwa ambao gharama zake
zilikadiriwa kuwa ni Dola za Kimarekani bilioni 3.7 pamoja na madhara makubwa
ya kisaikolojia kwa jamii zilizoathirika.
Rais Dk. Shein
alieleza kuvutiwa na ajenda kuu ya Mkutano huo iliyo kwenye kaulimbiu isemayo “
Ushiriki wa kisekta kwenye kupunguza madhara ya maafa ni njia bora ya kujenga
uhilimi katika ukanda wa nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa
Afrika (SADC)”.
Aidha, alieleza kuwa
ilivyokuwa maafa ni matukio yanayoleta hasara kubwa kwa taifa lolote kutokana
na majanga yanayoambatana nayo, ajenda na kauli mbiu ya mkutano huo zimesadifu
sana katika lengo kuu la mkutano huo.
“Mkutano huu ni
muhimu, tukijua kwamba washiriki nyote mna uwezo na ushawishi mkubwa katika
nchi zenu wa kuyaingiza masuala ya kukabiliana na maafa katika mipango ya
maendeleo, mipango ya kisekta, miradi inayofadhiliwa na wahisani mbali mbali
pamoja na mipango mengine ya kiutawala”,alisema Dk. Shein.
Dk. Shein aliieleza
mikakati mbali mbali inayopangwa na
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kukabiliana na maafa ikiwa ni pamoja
na kuandaa Sera ya Kukabiliana na Maafa ya mwaka 2011, kutungwa Sheria na
hatimae kuanzishwa Kamisheni,
Rais Dk. Shein
alieleza kuwa Serikali imeandaa Mkakati wa Mawasiliano Wakati wa Maafa na Mpango
wa Kujiandaa na Kukabiliana na Maafa katika ngazi ya Kitaifa na Wilaya, kuanzisha
kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura kilichopo Maruhubi Unguja, kutoa
elimu ya maafa, pamoja na kuandaa
mikakati maalum ya kuimarisha huduma za usafiri baharini.
Mikakati mengine ni ununuzi
wa vyombo vya kisasa vya usafirishaji wa abiria, mizigo na mafuta Rais Dk.
Shein alisema kuwa Serikali imejenga vituo vya uokozi vinavyosimamiwa na Kikosi
Maalum cha Kuzuia Magendo (KMKM) katika eneo la Nungwi na Kibweni Unguja na kituo
cha Mkoani kwa upande wa Pemba.
Hatua nyengine
zilizochukuliwa na Serikali kwa maelezo ya Rais Dk. Shein ni ununuzi wa mitambo
mbali mbali na ndege zisizo na rubani (drones) ili kujua hali ya usalama wa
meli na vyombo vya habarini, boti za uokozi za kisasa sambamba na kutekeleza
Mradi wa Kuendeleza Huduma Mjini (ZUSP).
Sambamba na hayo, Rais
Dk. Shein aliwahamasisha wajumbe wa Mkutano huo wa nchi za SADC kuwaleta walimu
wao kuja kujifunza Kiswahili hapa Zanzibar kutokana na Zanzibar kuandaa mpango
wa mafunzo kwa ajili ya walimu wa kwenda kusomesha Kiswahili katika mataifa yao
katika Chuo chake Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA).
Aliongeza kuwa hatua
hiyo imekuja kutokana na lugha ya Kiswahili ilichaguliwa kuwa miongoni mwa
lugha za mawasiliano katika mikutano ya Jumuiya ya Nchi za SADC na kusisitiza
kuwa Zanzibar iko tayari kuisaidia Jumuiya ya SADC katika kuisomesha lugha hiyo.
Nae Waziri wa
Nchi,Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu Jenista
Mhagama alisema matukio mbali mbali ya maafa yaliyotokezea katika nchi za SADC
na athari zake kwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa nchi wanachama.
Alieleza athari za
vimbunga ambavyo vilipewa majina ya “Idai na Kenneth” vilivyotokea mwaka jana
2019 na kusababisha madhara makubwa katika nchi ya Msumbiji, Zimbwabwe, Comoro
na Malawi.
Aidha, alieleza uzoefu
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika masuala mbali mbali ya maafa pamoja
na mikakati iliyopangwa katika kuyakabili maafa ikiwa ni pamoja na kutungwa kwa
sheria na kanuni mbali mbali.
Mapema Katibu Mtendaji
wa SADC Dk. Stergomena Lawrence Tax
alitoa pongeza kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuandaa mkutano huo, mkutano ambao utaitangaza vyema
Zanzibar pamoja na vivutio vyake.
Viongozi mbali mbali
walishiriki katika mkutano huo akiwemo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
Balozi Seif Ali Idd, Mawaziri wa SADC wanaosimamia masuala ya maafa nchini
mwao, Mawaziri wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mawaziri wa Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar, Katibu Mtendaji wa Jumuiya ya SADC, Dk. Stergomena
Lawrence Tax pamoja na viongozi wengine wa nchi za Jumuiya hiyo.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment