Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Ali Mohamed Shein. Amewatowa Wasiwasi Wananchi Waliokuwa Hawajapata Vitambulisho Vya Mzanzibar Mkaazi Kuwataka Kuwa na Subra ni Haki ya Kila Mwanchi wa Zanzibar.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akihakikiwa taarifa zake na Afisa wac Tume ya Uchaguzi Zanzibar(ZEC) Ndg. Salum Abdulrahman Nadhif, alipofika Kituo cha Kujiandikisha Wapiga Kura Skuli ya Msingi Bungi Wilaya ya Katiu Unguja leo.29-2-2020.  


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, amewatoa wasi wasi wananchi waliokuwa hawajapatiwa vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi na kuwataka kuwa na subira kwani kitambulisho hicho ni haki ya kila mwananchi wa Zanzibar.

Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo, katika mahojiano na waandishi wa habari mara baada ya kuhakiki taarifa zake kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura katika kituo cha kupigia kura cha skuli ya Msingi Bungi, Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja.

Rais Dk. Shein akiwa amefuatana na Mama Mwanamwema Shein katika zoezi hilo, alisema kuwa kitambulisho cha Mzanzibari Mkaazi kina umuhimu mkubwa kwa mwananchi wa Zanzibari kutokana na kusaidia katika shughuli mbali mbali na si ya kutumia kwa uchaguzi pekee.

Hivyo, Rais Dk. Shein aliwataka wananchi wasiwe na wasi wasi kwani Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar itachukua jukumu lake la kuhakikisha kila mwenye sifa ya kupata kitambulisho hicho basi anakipata kwa taratibu na sheria zilizopo.

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza kuwa zoezi hilo linakwenda vizuri kutokana na muda na taratibu zilizowekwa ambazo zimekuwa zikiwasaidia kwa kiasi kikubwa wananchi kuweza kuhakiki taarifa zao kwa ufanisi mkubwa pale wanapofika vituoni.

Alieleza kuwa kazi zote zina changamoto na hasa zile zinazowahusu watu wengi sambamba na kuwepo kwa utaalamu mpya, hivyo aliwataka wananchi waendelee kuwa wastahamilivu na bila ya kukiuka sheria na kuwahakikishia kuwa kila mwenye haki yake ya kupata Kitambulisho cha Mzanzibari Mkaazi atakipata.

“zoezi linakwenda vizuri, nimetumia muda mfupi na wasimamizi na waandishi wanafanya kazi zao vizuri “alisema Rais Dk. Shein.

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imejiandaa kuhakikisha kuwa uchaguzi ujao wa Zanzibar mwaka huu 2020 una kuwa huru na wa haki na wala hakutakuwa na zogo wala khasia zozote.

Rais Dk. Shein ambaye alifika kituoni hapo mnamo majira ya saa tatu za asubuhi na kujumuika na wananchi waliojitokeza katika zoezi hilo, alisisitiza kuwa na kwa wale wote ambao wenye nia ya kuvuruga uchaguzi kwa njia zozote zile  Serikali itawadhibiti.

Rais Dk. Shein aliwahakikishia wananchi kuwa atahakikisha Zanzibar inaendelea kuwa salama na yenye amani katika wakati wote wa uongozi wake na hata wakati wa kiongozi mwengine ajae.

Alieleza kuwa Serikali ni ya watu wote na si ya mtu mmoja na kusisitiza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itakuwepo na anapoondoka yeye atakuja kiongozi mwengine na anaamini atatokana na Chama chake cha Mapinduzi (CCM) ambacho kitaendelea kushinda kama ilivyo kawaida ya chama hicho katika uchaguzi ujao.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein aliwataka wananchi kuendelea kumuombea dua yeye pamoja na kuiombea Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ili makusanyo ya mapato yaendelee kuwa mazuri kwa azma ya kutekeleza ahadi yake ya kuongeza mshahara kabla ya kumaliza madaraka yake japo kwa asilimia ndogo.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar ni Tume Huru ambayo imekuwepo muda mrefu tokea kuanzishwa chaguzi hapa Zanzibar  ambayo imekuwa ikifanya vizuri  kutokana na kuendeshwa kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar ikiwa ni pamoja na kufuata sheria na taratibu zilizowekwa.

Aliongeza kuwa licha ya kuwepo kwa mabadiliko ya uongozi kwa kila ufikapo muda uliowekwa lakini bado Tume hiyo ipo vizuri na haijatetereka na imekuwa ikifanya kazi zake vyema kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alieleza imani yake kwa Tume hiyo na kusisitiza kuwa inaimani kubwa kuwa Tume hiyo itafanya vizuri sana katika uchaguzi mkuu ujao kwani tokea alipoingia madarakani mwaka 2010 Tume hiyo imekuwa ikifanya vizuri. Hivyo, aliwataka wananchi watulie na wala wasiwe na wasi wasi.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.