Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, Atembelea Jengo Linalotarajiwa Kuwa la Uchunguzi wa Virusi Zanzibar Binguniu Wilaya ya Kati Unguja leo.25/3/2020.ymK


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Waandishi wa habari wa vyombo mbalimbali vilioko Zanzibar wakati alipotembelea Jengo linalotarajiwa kuwa la Uchunguzi wa Virusi Zanzibar,Wilaya ya Kati Unguja lilioko katika enelo la Taasisi ya Utafiti wa Afya Zanzibar, (hawapo pichani) na (kushoto kwa Rais) Waziri wa Afya Zanzibar.Mhe. Hamad Rashid Mohammed na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Afya Zanzibar.Dkt. Mayasa Salum Ally. 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein  amewataka wananchi kuacha ukaidi na kufuata kikamilifu maelekezo ya Serikali, ikiwa ni hatua za kuunga mkono juhudi za Serikali katika kukabiliana na Virusi vya Ugonjwa wa Corona.

Dk. Shein amesema  hayo leo wakati alipotembelea eneo linalotarajiwa kujengwa jengo la Uchunguzi wa maradhi makuu, liliomo ndani ya Taasisi ya Utafiti wa Afya, huko Binguni, Wilaya Kati Unguja.

Amesema katika kukabiliana na virusi vya ugonjwa huo, Serikali tayari imetowa malekezo kadhaa, ikiwa njia ya kujikinga na virusi vya ugonjwa huo, hivyo akawataka wananchi kuacha ukaidi na kutekeleza maelekezo ya kudumisha usafi kama inavyoelekezwa.

Alisema Virusi vya Ugonjwa wa Corona ni janga na Kimataifa na ni maradhi yasiotaka mzaha wala hayachaguwi aina ya mtu wa kuamuathiri, hivyo ni vyema wananchi wakaondokana na ushindani na kuzingatia maelekezo ya Serikali.

Alieleza kuwa Serikali imeingia katika vita dhidi ya adui asieonekana na hivyo ikalazimika kuchukuwa hatua mbali mbali za dharura ikiwemo kuzuia Kongamano la dini pamoja na kuzifunga skuli zote na wanafunzi kukosa taaluma.

 Shein alisema Serikali haiwezi kuainisha ukubwa wa gharama  inazopoteza kutokana na hatua ilizochukuwa katika kukabiliana na virusi vya ugonjwa wa Corona, sambamba na athari za kiuchumi zitokanazo na kuvurugika kwa sekta ya utalii, ambayo huchangia asilimia themanini ya fedha za kigeni.

Rais Dk. Shein aliwataka wananchi kuondokana na upotoshaji kupitia mitandao ya kijamii.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa wananchi kuondokana na mikusanyiko, hususan katika eneo la Hospitali kuu ya Mnazi mmoja pamoja na maeneo ya masoko, kwa kigezo kuwa hatua hiyo inaweza kuwa chanzo cha kusambaa kwa viusi hivyo, pale itakapotokezea mtu mmoja kuwa navyo.

Katika hatua nyengine, Dk. Shein alilisistiza azma ya Serikali ya kujikita katika kufanya uchunguzi wa maradhi mbali mbali kwa kigezo kuwa hakuna tiba muafaka bila ya kuwepo uchunguzi, hivyo akabainisha dhamira ya Serikali katika kukamilisha ujenzi wa jengo la kisasa la Maabara katika eneo hilo la Binguni.

Alisema Serikali imefikia uamuzi wa kukamilisha jengo hilo mahala hapo kwa kuzingatia mazingira bora yaliopo, ambayo yamejitenga na pia ni mazuri kwa shughuli hizo.

Aliwahakikishia wananchi kuwa jengo hilo litakamilika ndani ya kipindi cha miezi mitatu ijayo pamoja na  kuwekewa vifaa vyote muhimu ili kukidhi mahitaji na malengo yaliokusudiwa.

Aidha, alisema Serikali itakamilisha miradi yote ya Maendeleo iliyokwisha anzishwa, ikiwemo ya ujenzi wa Nyumba  Kwahani, Michenzani Mall, Barabara, Mahakama Kuu na mingineyo pamoja na kuanzisha miradi mipya, huku akibainisha kuwa endapo kutatokezea upungufu wa fedha itaangalia namna ya  kukamilisha miradi hiyo.       
 
Mapema, Waziri wa Afya Hamad Rashid Mohamed, amesema Wizara hiyo imejiandaa kikamilifu kushirikiana na Serikali ya Watu wa China  katika dhana ya kukuza utalaamu ili  kuleta ufanisi wa maabara itakayojengwa.


 Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 
 E-mail: abdya062@gmail.com

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.