Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Wasanii mbalimba Zanzibar katika ukumbi wa Sheikh Idrisa Abdulwakil Kikwajuni Jijini Zanzibar.
SERIKALI ya
Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuchukua hatua za kuimarisha sanaa na
kuendeleza utamaduni kwa kuwaendeleza wasanii kwa kuwaongezea taaluma ya
kuzifanikisha shughuli zao.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein aliyasema hayo leo katika hotuba yake aliyoitoa
kwenye Mkutano alioufanya kati yake na
Wasani wa Zanzibar, huko katika ukumbi wa
Sheikh Idris Abdul Wakil, Kikwajuni Jijini Zanzibar.
Katika hotuba yake hiyo, Rais Dk. Shein alisema
kuwa jitihada maalumu zitachukuliwa kuhakikisha kuwa kazi za sanaa zinatoa
fursa kubwa zaidi ya ajira kwa vijana kwa kufanya shughuli zao kisasa na bora
zaidi ambazo zitatumia fursa ya soko la utalii.
Rais Dk. Shein aliongeza kuwa katika kuyafikia
malengo hayo, Serikali inaendelea na jitihada za kuimarisha nyumba ya sanaa
iliyopo Mwanakwerekwe kwa kuijenga upya na kuwa na jengo la kisasa lenye
taswira nzuri.
Alieleza kuwa nyumba hiyo itawekwa vifaa vya
kisasa pamoja na kuongeza walimu wa fani mbali mbali za sanaa ambapo kukamilika
kwa hatua hio kutatoa nafasi muhimu kwa vijana wa Zanzibar kupata sehemu nzuri
ya kujifunza ujuzi wa fani mbali mbali.
Aidha, Rais Dk. Shein alisema kuwa sanaa na
utamaduni ni nyenzo muhimu za kuitambulisha jamii na ni hazina muhimu ya
kurithishwa kutoka kizazi kimoja hadi chengine kwani jamii isiyokuwa na
utamaduni, mila, silka, desturi pamoja na sanaa yake inakuwa kama vile haipo.
Rais Dk. Shein alieleza furaha yake kwa kukutana
na wasanii hao kutoka Unguja na Pemba na kueleza kuwa jamii ya watu wa Zanzibar
kama zilivyo jamii nyengine duniani nayo pia, ina sanaa, tamaduni, mila, silka,
desturi zake tangu enzi na dahari zilizoachwa na wazee hivyo, ni lazima zitunzwe,
zidumishwe na ziendelezwe.
Alisema kuwa sanaa imeiletea sifa Zanzibar na
kuifanya ijulikane miaka mingi iliyopita ambapo historia inaeleza kuwa wasanii
wa zamani akiwemo Marehemu Bibi Siti bint Saad tangu miaka ya 1930 aliweza
kuitangaza Zanzibar kwa muziki wa taarabu kiasi cha kufika India na Mataifa
mengine duniani.
“Sanaa ni uhai wetu, kwa hakika maisha bila ya
sanaa yangekuwa chapwa na kama yanauzwa
yangekuwa bure ghali…….kwa mnasaba huo kazi za wasanii ni muhimu na nakuhakikishieni
kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inathamini sana na inatambua umuhimu wa
wasanii”, alisema Dk. Shein.
Rais Dk. Shein alisema kuwa kwa kutambua na
kuthamini umuhimu wa kuienzi, kuidumisha na kuiendeleza sanaa na utamaduni wa
Kizanzibari ikiwa ni utambulisho na urithi wa jamii, Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar Awamu ya Saba imekuwa ikichukua hatua mbali mbali katika kuiimarisha
sekta hio.
Alieleza kuwa yapo mengi yaliyofanywa na Serikali
kwa ajili ya kuziendeleza sanaa na utamaduni wa Zanzibar kwa vipindi tofauti
kwa muda wa miaka 56 ya Mapinduzi ambapo katika kipindi chote hicho kila awamu
ya uongozi wa Serikali iliunda Wizara maalum inayoshughulikia mambo ya sanaa na
utamaduni na kuteuliwa viongozi wenye sifa wa kuiongoza Wizara hio.
Rais Dk. Shein alisema kuwa tayari zoezi la
ugawaji wa mirahaba limefanywa kwa awamu 6 tangu lilipoanza mwaka 2013 ambapo
katika mwaka huo TZS milioni 37.0 ziligawiwa na katika mwaka 2019 jumla ya TZS
milioni 120.1 ziligawiwa kwa wasanii mbali mbali wakiwemo waliokwishatangulia
mbele ya haki.
Hivyo, Rais Dk. Shein aliwahimiza wasanii na
wabunifu kujisajili ili waweze kunufaika zaidi kwa kazi zao kupitia utaratibu
huo ulioanizishwa na kusimamiwa na Serikali yao ambayo haina ubaguzi na
inasimamia suala hilo kwa mujibu wa sheria na haki kwa kila msanii na mbunifu
aliyesajiliwa rasmi.
Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein aliitaka Wizara ya
Vijana, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali
kushirikiana ili kuhakikisha kuwa malengo ya Serikali ya kufufua vuguvugu la
michezo katika maskuli linasaidia pia, kukuza masuala ya sanaa na utamaduni.
Aidha, aliitaka Wizara ya Elimu kuviendeleza
vipaji kwa kuwapa fursa watoto kucheza katika vipindi maalum vinavyotengwa kwa
michezo ndani ya wiki ya masomo.
Pia, alitoa wito kwa wafanyabiashara kutumia fursa
ya kuwepo kwa watumiaji wa vifaa vya muziki na filamu ili waweze kukuza
biashara zao na wasiogope kuleta biashara hizo kwani hazitooza na badala yake
zitapamba maduka.
Aliitaka Wizara hiyo kufanya mpango wa
kuwaendeleza wasanii kwa azma ya kuonesha kuwa wanawathamini na wako pamoja nao
kwa uzima na maradhi huku akiitaka Wizara hiyo kuzifanyia kazi changamoto zote
20 zilitotolewa na wasanii hao ndani ya mwezi mmoja na baadae kumueleza Rais
walipofikia.
Rais Dk. Shein pia, alitumia fursa hiyo
kulipongeza Shirika la Utangazaji la Zanzibar (ZBC), kwa kubuni kipindi maalum
cha “Vuna Vipaji” ambacho kimesaidia vijana kujitokeza na kuonesha uwezo wao wa
kuigiza.
Kadhalika, aliwataka wasanii kuendelea bila ya
kuchoka kuendeleza sanaa na utamaduni wa Kizanzibari pamoja na kuonesha katika
sanaa zao athari za kuiga na wasikubali kuziacha kwa namna yoyote ile sanaa,
utamaduni, mila na desturi zao na ni vyema wakazitetea wakati wote.
Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alitoa wito kwa
wasanii kutokana na kuwa mwaka huu wa 2020 Tanzania inakabiliwa na uchaguzi
mkuu wakaandaa kazi za sanaa zenye kuhamasisha wananchi kuitumia haki yao ya
kuwachagua viongozi kwa amani na utulivu kwani hakuna mbadala wa amani.
Nae Waziri wa Vijana, Utamaduni, Sanaa na Michezo
Balozi Ali Karume alitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa kukutana na wasanii hao
wa Zanzibar jambo ambalo limeonesha namna anavyowajali pamoja na kuzithamini
kazi zao.
Alieleza jinsi Wizara inavyochukua juhudi za
kuwaendeleza wasanii wa Unguja na Pemba ikiwa ni pamoja na kuiendeleza lugha ya
Kiswahili ili kiendelee kuwa lugha ya Taifa huku akisisitiza kuwa Wizara hiyo
itahakikisha inafanya juhudi za kutekeleza haki za wasanii kupitia Mirabaha
inayotokana na kazi zao.
Nao wasanii katika risala yao iliyosomwa na
Mwanakombo Mwadini ilimpongeza Rais Dk. Shein kwa uongozi wake kwa kuimarisha
miundombinu, utawala bora, kudumisha amani, kuinua hali za wananchi, kuinua
sekta za elimu, kilimo, afya, mawasiliano, ajira na nyenginezo bila ya kuisahau
sekta ya utamaduni, ubunifu na sanaa.
“Wasanii kwa pamoja tunakushukuru na kukupongeza
kwa kuinua hali za wasanii na sanaa kwa ujumla hakika Mheshimiwa Rais wewe ni
miongoni mwa wasanii nguli na ni mwenye kuipenda Sanaa, Pia tunakupongeza kwa
kutengeneza ukumbi wa kufanyia mikutano yetu pamoja na studio ya kisasa ya
kurikodia kazi zetu” walisema wasanii.
Wasanii hao walitumia fursa hiyo kutoa shukurani
kwa uongozi wa Wizara ya Vijana, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kuonesha
dhahiri kwa vitendo kwamba inathamini shughuli za sanaa na kuwa bega kwa bega
huku Wasanii hao wakitumia fursa hiyo kueleza changamoto mbali mbali
zinazowakabili.
Rais Dk. Shein pia, alipata fursa ya kuwasikiliza
wasanii mbali mbali katika mkutano huo ambao walieleza mafanikio na changamoto
wanazozikabili huku wakipongeza hatua yake ya kwenda kukutana nao.
Katika mkutano huo pia, wasanii kutoka vikundi
mbali mbali vya Unguja na Pemba walitumia fursa hiyo kuonesha kazi zao ikiwemo
michezo ya kuigiza pamoja na ngoma ya Kibati yenye asili ya kisiwa cha Pemba,
mkutano huo ambao pia, uliwajumuisha wasaanii wakongwe wa fani zote kutoka Unguja
na Pemba.
Rais Dk. Shein kwa kuonesha jinsi anavyowajali na
kuwathamani wasanii hao pamoja na wabunifu mbali mbali waliohudhuria katika
mkutano huo pia, aliwaandalia chakula maalum cha mchana hapo katika viwanja vya
Wizara ya Habari, Utalii na Mambo ya Kale, Kikwajuni Jijiji Zanzibar.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment