Habari za Punde

Zanzibar Inathamini Sana Ushirikiano Uliopo Katika Sekta Mbalimbali za Maendeleo Ikiwemo Elimu, Afya, Biashara, Miundombinu, Kilimo na Huduma za Kijamii.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Ali Mohamed Shein, akizungumza na Balozi Mdogo Mpya wa India anayefanyia Kazi zake Zanzibar.Mhe. Bhagwant Singh, alipofika Ikulu Jijini Zanzibar kwa mazungumzo na kujitambulisha leo.16/3/2020. 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa hatua za India za kuendelea kuiunga mkono Zanzibar zina imarisha uhusiano na ushirikiano wa kihistoria na udugu uliopo kati ya pande mbili hizo.

Hayo yamesemwa leo na Rais Dk. Shein wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Balozi Mdogo Mpya wa  India katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Bhagwant Singh, aliefika Ikulu Jijini Zanzibar kwa ajili ya kujitambulisha.

Katika maelezo yake Dk. Shein alisema kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwemo Zanzibar ina uhusiano na ushirikiano wa kihistoria na India ambao umeanzishwa na  waasisi wa Mataifa hayo akiwemo Hayati Julius  Kambarage Nyerere  kwa mashirikiano na waasisi wa India akiwemo Hayati Jawaharlal Nehru na baadae Hayati Indira Gandhi.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa waasisi hao walishirikiana kwenye nyanja za kimataifa ikiwa ni pamoja na kupiga vita ukoloni pamoja na ubaguzi wa rangi.

Akielezea juu ya ushirikiano na uhusiano kati ya India na Zanzibar, Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa Zanzibar inathamini sana ushirikiano uliopo hatua ambayo imesaidia sana  kuongeza ushirikiano katika sekta mbali mbali za maendeleo ikiwemo elimu, afya, biashara, miundombinu, kilimo, huduma za kijamii na nyenginezo.

Kwa upande wa ushirikiano uliopo katika sekta ya elimu, Dk. Shein alitoa pongezi kwa India kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika sekta ya elimu ikiwa ni pamoja na kutoa nafasi kadhaa za masomo kwa Zanzibar nchini humo katika fani mbali mbali.

Akiongezea mazungumzo hayo katika sekta hiyo ya Elimu, Rais Dk. Shein alieleza haja ya India kuweza kushirikiana na Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) kwa ajili ya kuleta wakufunzi kwa ajili ya masomo ya Tiba na Kinga ya Meno yanayoendeshwa na Chuo Kikuu hicho.

Dk. Shein alisema kuwa India ni nchi ambayo inatambulika duniani kote kutokana na kupiga hatua katika mafunzo ya masomo ya Sheria na Tiba hivyo, hatua hiyo ya kuleta wakufunzi kuja kusomesha Chuo Kikuu cha (SUZA) kutasaidia kuimarisha sekta ya afya hapa nchini.

Aidha, alieleza kuwa hatua hiyo pia, itapunguza idadi ya wagonjwa kwenda nchini India kwa ajili ya kufuata matibabu yanayotolewa na Hospitali zake kuu za nchi hiyo na badala yake huduma hizo zitatolewa na madaktari wazalendo watakao pata mafunzo hayo hapa hapa nchini katika chuo hicho Kikuu hicho cha (SUZA).

Pia, alipongeza hatua za mashirikiano zilizofanyika Kati ya Zanzibar na India kwa nchi hiyo kuikopesha Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia benki yake ya Exim kiasi cha Dola za Kimarekani milioni 92 kwa ajili ya kutekeleza mradi mkubwa wa maji safi na salama katika Mkoa wa Mjini Magharibi.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alieleza hatua zinazoendelea kutokana na makubaliano ya mashirikiano yaliyofikiwa wakati wa ziara yake nchini humo mnamo Februari mwaka 2014.

Dk. Shein alimuahidi Balozi huyo kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana nae katika kuhakikisha anaendelea kufanya kazi zake vyema hapa nchini ikiwa ni miongoni mwa kukuza na kuimarisha uhusiano na ushirikiano kati ya India na Zanzibar.

Nae Balozi Mdogo Mpya wa India anaefanya kiazi zake hapa Zanzibar Bhagwant Singh  alipongeza uhusiano na ushirikiano wa muda mrefu uliopo kati ya India na Zanzibar na kuahidi kuwa nchi yake utauendeleza kwa manufaa ya pande zote mbili.

Balozi Singh alimpongeza Rais Dk. Shein kwa kasi kubwa ya maendeleo yaliyofikiwa hapa Zanzibar na kuahidi kuwa nchi yake itaendelea kuunga mkono juhudi hizo ili zizidi kuimarika.

Aliongeza kuwa India itahakikisha inakamilisha miradi yote ya maendeleo ilioanzishwa kwa mashirikiano kati yake na Zanzibar sambamba na kuendelea  kutoa nafasi za masomo kwa Zanzibar zikiwemo zile za muda mfupi kwa watendaji wa Serrikali kupitia mpango wa “Indian Technical and Economic Cooperation Program” (ITEC) na “International Forestic Science” (IFS).

Aidha, alieleza hatua za nchi hiyo za kuendelea kusaidia upatikanaji wa vitendelea kazi na kuleta wakufunzi katika  Chuo cha Amali Vitongoji Pemba ambapo Mpango huo upo katika hatua za mwisho za ujenzi wa majengo ya chuo hicho.

Sambamba na hayo, Serikali ya India imeweza kuisaidia Zanzibar katika kuimarisha elimu ya amali kwa kufadhili ujenzi wa Chuo cha Amali Kibokwa, Unguja kwa lengo la kutoa ujuzi kwa akina mama na vijana mradi ambao tayari umeshakamilia na kukabidhiwa kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar mnamo mwaka 2019.

Pamoja na hayo, Balozi Singh, alieleza azma ya nchi hiyo ya kuendelea kushirikiana na nchi za Bara la Afrika ikiwa ni pamoja na kuendelea kuziunga mkono juhudi za nchi hizo katika sekta zake za maendeleo ili zizidi kupiga hatua za maendeleo.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.