Habari za Punde

Mgonjwa Wa Tatu Apona Ugonjwa Wa Corona Na Kuruhusiwa.• Mwingine mmoja kusubiri kipimo cha mwisho

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto,Mhe. Ummy Mwalimu

Na. WAMJW-Dar es Salaam.                                                                                                                                       
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe.Ummy Mwalimu amesema kuwa mgonjwa wa tatu aliyeambukizwa ugonjwa wa corona nchini amepona na kuruhusiwa kurudi nyumbani, huku mgonjwa  mwingine mmoja kipimo cha pili ameonyesha negative hivyo anasubiri kipimo cha mwisho kuthibitishwa kupona.

Waziri Ummy  ameyasemahaya leo jijini hapa kuwa mmoja wa wagonjwa hao ni yule aliyekuwa amelazwa kwenye kituo maalumu ya tiba cha  Mkoa wa Kagera na ametangaza kwamba mkoa huo hivi sasa hauna mgonjwa.

“Arusha tulikuwa na wagonjwa wawili, mmoja aliruhusiwa na mgonjwa mwingine majibu ya leo asubuhi yameonyesha kuwa ni ‘negative’ hivyo tunasubiri kipimo kingine kimoja ili aweze kuruhusiwa,” amesema Ummy Mwalimu.

Pia, Waziri wa Afya amewashukuru wananchi kwa kuzingatia maelekezo ya wataalamu wa afya ya kujikinga dhidi ya maambukizi ya ugonjwa wa Corona hususani kunawa mikono kwa sabuni na maji tiririka.

Amewataka wananchi waendelee kuepuka mikusanyiko na misongamano isiyo ya lazima ili kukabiliana na
 maambukizi.

“ Nawaomba kukaa mita moja au zaidi kati ya mtu mmoja na mtu mmoja ili kuweza kuzuia maambukizi zaidi.
Katika hatua nyingine, Waziri wa Afya amekabidhi vifaa kinga kwa Jeshi la Polisi na Magereza kwa ajili ya kujikinga wakati wa kutoa huduma kwa  jamii ikiwa ni msaada kutoka Taasisi ya Jack Maa ya nchini China.

Amesema licha ya asilimia 90 ya vifaa kinga kuelekezwa kwa watumishi wa afya katika vituo vya huduma ya afya nchini, kipaumbele cha Serikali ni kuwakinga watumishi wa afya.

 “Juzi tulimsikia Rais wa Chama cha Madaktari Tanzania, na mimi nataka kutumia fursa hii ni kuendelea kuhakikisha sisi Serikali tunawalinda watumishi wa afya hawapati maambukizi wakati wanapotoa huduma kwa wagonjwa,”

Amevitaja vifaa kinga hivyo ni pamoja na Barakoa 16,000 kwa Jeshi la Polisi na Magereza, gloves 8,000, nguo za kijikinga (PPE) 50 na jiki ya vidonge kopo (chlorine) 100.

Amesema kuwa wizara yake imetoa vifaa hivyo ikiwa ni msaada kutoka kwa Jack Maa kwa sababu  Jeshi la Polisi na Magereza wamekuwa wakikutana mara kwa mara na wananchi na pia wamekuwa wakisaidia kazi mbalimbali za kuhudumia jamii ikiwemo kutoa huduma za afya jwenye vituo vyao.
Waziri Ummy Mwalimu amesema kuwa vifaa hivyo vitatumika kwa ajili ya vituo vya afya vya Jeshi na kwa ajili yao wenyewe wakati wa kutoa huduma kwa wananchi.  

“Lengo letu ni kuhakikisha pia kwamba vituo vyote vinatoa huduma kwa jamii hususani jeshi la Polisi na Magereza tunawapatia vifaa tiba ili kujikinga na maambukizi ya virusi vya Corona,” amesema.

Baada ya kukabidhiwa vifaa kinga kutoka kwa Waziri wa Afya, Naibu Kamishina wa Jeshi la Polisi na Mkuu wa Utawala wa Jeshi hilo, Anthon Ruta ameshukuru kwa kubabidhiwa vifaa kinga kwa ajili ya kuendeleza mapambano dhidi ya ugonjwa vya Corona na kuvitumia kutokana na maelekezo yenu.

Naye Mkaguzi Msaidizi na Ofisa Tabibu wa Jehi la Magereza, Kenazi William amesema kuwa ameshukuru kwa kupatiwa msaada ambao umekua ni chachu  kwao kwa kuwa wamekuwa wakipokea wageni wengi wakiwamo mahabusu, wafungwa na kuchanganyikana na pia vifaa hivyo vinawapa nguvu zaidi ya katika kukabiliana na ugonjwa corona.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.