Muonekano wa Chumba cha Upasuaji katika kituo cha
Afya Upuge Wilayani Uyui baada ya kuboreshwa kwa gharama ya shilingi milioni 500
zilizotumika kujenga majengo mapya yaliyowezesha huduma kuboreshwa ikiwemo kuanza kwa huduma za upasuaji.
Muonekano wa Jengo la
utawala katika Hospitali ya Wilaya ya Uyui Mkoani Tabora baada ya ujenzi wa Hospitali hiyo kukamilika tayari kwa kuanza kutoa huduma,
ujenzi wa Hospitali hiyo umegharimu shilingi Bilioni 1.5 hadi kukamilika.
Sehemu ya majengo mapya ya Kituo cha Afya Upuge Wilayani Uyui Mkoani Tabora kama yanavyoonekana baada kuboreshwa kwa gharama ya shilingi milioni
500 zilizotumika kujenga majengo mapya yaliyowezesha huduma kuboreshwa ikiwemo kuanza kwa huduma za upasuaji.
Sehemu ya majengo mapya ya Kituo cha Afya Upuge Wilayani Uyui Mkoani Tabora kama yanavyoonekana baada kuboreshwa kwa gharama ya shilingi milioni 500 zilizotumika kujenga majengo mapya yaliyowezesha huduma kuboreshwa ikiwemo kuanza kwa huduma za upasuaji.
(Picha zote na Aboubakari Kafumba)
Na
Frank Mvungi- MAELEZO
Serikali ya Awamu ya
Tano imetimiza ndoto ya wananchi wa Wilaya ya Uyui, mkoani Tabora kufikiwa na
huduma bora za afya katika maeneo yao.
Akizungumza katika
mahojiano maalum wilayani humo, Mkuu wa Wilaya, Gift Msuya amesema kuwa kwa sasa
wananchi wa wilaya hiyo wanafikiwa na huduma za afya kupitia vituo vya afya
vilivyojengwa na vile vilivyoboreshwa katika kipindi cha miaka mine iliyopita.
“ Tumekamilisha
ujenzi wa Hospitali ya Wilaya iliyogharimu Shilingi bilioni 1.5 na iko tayari
kuanza kutoa huduma baada ya kuwasili kwa vifaa, hili linaenda sambamba na
utoaji wa huduma katika vituo vyetu vya afya ambavyo vinatoa huduma
zinazoendana na mahitaji ya wananchi,” alisisitiza Msuya
Aidha, Msuya amesema
kuwa Serikali ilitoa milioni 500 zilizowezesha kuboreshwa kwa Kituo cha Afya
Upuge na pia shilingi milioni 400 zimetumika katika ujenzi wa Kituo cha Afya
Igalula.
Kuwepo kwa huduma
bora na vifaa vya kisasa kumewezesha Wilaya ya Uyui kutokuwa na vifo vya
akinamama wanaopatwa na uchungu pingamizi kwa kuwa sasa huduma ya upasuaji
inapatikana karibu na walipo wananchi tofauti na ilivyokuwa awali.
Naye Kaimu Mganga
Mfawidhi wa Kituo cha Afya Upuge, Sr. Dkt. Yustina Raphael amesema kuwa tangu kuanza kwa huduma ya upasuaji
kwa akinamama zaidi ya akinamama 100 wamefanyiwa upasuaji kwa ufanisi.
“Jukumu letu ni
kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi kupitia kituo hiki cha Upuge kwa kuwa
kimeboreshwa na kina vifaa vya kisasa vya kutolea huduma ikiwemo vya maabara na
vya kufanyia upasuaji,” alisisitiza Sr. Dkt. Yustina
Awali, kabla ya
maboresho ya kituo hiki kilichoanza
mwaka 1977 kilikuwa na huduma chache na kwa sasa kimeongeza huduma kama za
maabara, upasuaji, mama na mtoto na pia watumishi wameongezwa ili kuendana na
mahitaji.
Akizungumzia kuhusu
rufaa katika Kituo hicho, Sr. Dkt. Yustina amesema kuwa baada ya maboresho
rufaa za wagonjwa zimepungua kwa kiwango kikubwa na hivyo kuwapunguzia wananchi
adha ya kutembea umbali mrefu au kusafiri kufuata huduma za afya.
Kwa upande wake mmoja
wa wagonjwa waliofika kupata huduma katika kituo hicho, Bi. Salma Ramadhani
aliwapongeza watoa huduma wa kituo cha afya Upuge kwa utendaji bora na wenye
tija kwa wananchi wote wanaofika kupata huduma
kituoni hapo.
“Tunamshukuru Mhe.
Rais Magufuli kwa kuboresha sekta ya afya hasa vituo vyetu vya afya kama hiki cha Upuge kwa sasa tunapata huduma
za upasuaji hapa na wahudumu wa hapa wakiwemo madaktari wanatuhudumia vizuri na
mazingira yameboreshwa kupitia majengo mapya na vifaa vya kisasa kabisa”, alisisitiza
Salma.
Akifafanua amesema
kuwa amefanikiwa kujifungua salama
kutokana na huduma bora zilizopo katika kituo hicho hali inayowafanya akinamama
kuondokana na adha ya kusafiri umbali mrefu kufuata huduma hizo.
Serikali ya Awamu ya
Tano imefanikiwa katika kuimarisha huduma za afya ikiwemo ujenzi wa vituo vya
afya, hospitali za wilaya, zahanati, ujenzi wa hosptali za rufaa za Mikoa na
Kanda na pia upatikanaji wa dawa na vifaa tiba imekuwa chachu ya kuboreshwa kwa
huduma katika wilaya na mikoa yote hapa nchini.
No comments:
Post a Comment