Habari za Punde

Kufuata Maelekezo Kupambana na Maradhi ya Corona na Kutoa Elimu Kwa Waliokuwa Hawajaelewa Juu ya Jangaa Hilo. Dk. Shein


WITO umetolewa kwa wananchi kupewa moyo kutokana na wengi wao kufuata maelekezo ya kupambana na maradhi yanayosababishwa na virusi vya Corona na kwa wale waliokuwa hawajaelewa wametakiwa kuelimishwa juu ya kupambana na janga hilo.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein alitoa wito huo hivi karibuni huko katika Ikulu ndogo, Chake Chake, Mkoa wa Kusini Pemba, wakati alipofanya mazungumzo na Viongozi wa Mikoa miwili ya  Pemba katika ziara yake ya siku tatu aliyoifanya kisiwani humo.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein alieleza kuwa wananchi walio wengi wameonesha muitikio katika kupambana na maradhi hayo kutokana na kufuata maelekezo yanatotolewa na wataalamu wa afya pamoja na viongozi wao.

Rais Dk. Shein alisema kuwa wananchi wengi hivi sasa wamekuwa wakifaa barkoa, wakitumia maji ya kutiririka na sababu pamoja na vitakasa mikono na maelekezo mengine ya kupambana na janga hilo, hivyo ni vyema wakapewa moyo kwa juhudi zao hizo.

Aliongeza kuwa kwa wale ambao bado hawajaelewa, Rais Dk. Shein aliwataka viongozi wote hapa nchini kuendelea na juhudi na mikakati yao ya kuwapa elimu ya kupambana na maradhi hayo kwa njia mbali mbali ili ujumbe huo uweze kuwafikia.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa licha ya juhudi na miongozo inayotolewa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupiti wataalamu wake wa afya pamoja na viongozi wake bado wapo wananchi ambao wanakaidi maelekezo hayo hivyo, ni vyema wakaendelea kuepwa elimu, miongozo na maelekezo juu ya janga hilo.

Hivyo, Rais Dk. Shein aliwataka viongozi wote hapa nchini kuendelea kuwapa elimu wananchi katika maeneo mbali mbali hasa vijijini na ikiwa bado elimu haijafika vyema watumiwe hata wataalamu wa sekta ya afya ili waende kutoa elimu hiyo kwa azma ya kupambana na maradhi hayo thakili.

Aidha, Rais Dk. Shein alipongeza mikakati iliyowekwa na viongozi wa serikali pamoja na wataalamu wa sekta ya afya hapa nchini na kusisitiza haja ya kupewa msukumo kwa wananchi kwani wapo walioanza kuelewa na wapo ambao bado elimu hiyo haijawafikia ama imewafikia lakini bado hawajaanza kuifuata.

Mnamo Machi 25, mwaka huu wakati akitembelea eneo linalotarajiwa kujengwa jengo la Uchunguzi wa Virusi vya maradhi makuu lililopo ndani ya Taasisi ya Afya huko Binguni Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja Rais Dk. Shein aliwataka wananchi kuacha ukaidi na kufuata kikamilifu maelekezo ya Serikali, ikiwa ni hatua za kuunga mkono juhudi za kukabiliana na Virusi vinavyosababisha maradhi ya Corona.

Katika maelezo yake siku hiyo, Rais Dk. Shein alieleza kuwa katika kukabiliana na virusi vya ugonjwa huo, Serikali tayari imetowa malekezo kadhaa, ikiwa njia ya kujikinga na virusi vya ugonjwa huo, hivyo akawataka wananchi kuacha ukaidi na kutekeleza maelekezo katika kupambana na janga hilo.

Aliongeza kuwa uwepo wa Virusi vinavyosababisha ugonjwa wa Corona ni janga na Kimataifa na ni maradhi yasiotaka mzaha wala hayachaguwi aina ya mtu wa kuamuathiri, hivyo ni vyema wananchi wakaondokana na ukaidi na badala yake wafuate maelekezo ya Serikali pamoja na wataalamu wa afya.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.