HOTUBA YA MAONI YA KAMATI YA SHERIA, UTAWALA BORA
NA IDARA MAALUM KUHUSIANA NA MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA WIZARA YA
KATIBA NA SHERIA,
KWA MWAKA WA FEDHA 2020/2021
Mheshimiwa Spika, kwanza
kabisa, ninachukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu, Mwingi wa
Rehema, Mwenye Kurehemu kwa kutujaalia uzima na afya njema ambavyo
vimetuwezesha kukutana tena katika Baraza hili Tukufu, kwa ajili ya kuendelea
na shughuli zetu za kuwatumikia wananchi wetu. Aidha, ninakushukuru wewe
Mheshimiwa Spika pamoja na Mheshimiwa Naibu Spika na Wenyeviti wote kwa
kuliongoza Baraza hili kwa ufanisi na nina imani kwamba mtaendelea kuliongoza
Baraza hili kwa uadilifu wa hali ya juu.
Mheshimiwa Spika, aidha, napenda kuchukua fursa hii kumshukuru na
kumpongeza kwa dhati kabisa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein kwa kuiongoza nchi yetu kwa
uadilifu na kuhakikisha kuwa maendeleo makubwa yanapatikana pamoja na kuendelea
kudumu kwa amani na utulivu katika nchi yetu.
Mheshimiwa Spika, pia, sina budi kumshukuru Waziri wa Katiba na
Sheria mheshimiwa Khamis Juma Mwalim pamoja na watendaji wote wakiongozwa na
Katibu Mkuu ndugu George Joseph Kazi. Aidha, Kamati inatoa shukurani zake za
dhati kwa Afisi ya Mwanasheria Mkuu Zanzibar inayoongozwa na Mwanasheria Mkuu
wa Serikali, mheshimiwa Said Hassan Said, Naibu Mwanasheria Mkuu, ndugu Mzee
Ali Haji pamoja na watendaji wao kwa mashirikiano mazuri waliyoyatoa kwa Kamati
katika kipindi chote bila ya kuwasahau watendaji wa Wizara ya Fedha na Mipango
kwa mashirikiano waliyotupatia wakati wa kupitia makadirio ya Bajeti ya Wizara
hii.
Mheshimiwa Spika, aidha, ninachukua fursa hii kuwashukuru Waheshimiwa
Wajumbe wa Kamati yetu kwa mashirikiano makubwa wanayonipatia katika kutekeleza
majukumu ya Kamati yetu na kuhakikisha kuwa thamani halisi ya fedha inapatikana
katika utekelezaji wa majukumu ya Wizara hii.
Mheshimiwa Spika, kwa heshima, naomba kuwatambua Wajumbe hao kwa
majina kama ifuatavyo:
1.
|
Mhe. Machano Othman Said
|
Mwenyekiti
|
2.
|
Mhe. Zulfa Mmaka Omara
|
Makamu Mwenyekiti
|
3.
|
Mhe. Ali Khamis Bakar
|
Mjumbe
|
4.
|
Mhe. Salma Mussa Bilal
|
Mjumbe
|
5.
|
Mhe. Dkt. Khalid Salum Mohamed
|
Mjumbe
|
6.
|
Mhe. Suleiman Makame Ali
|
Mjumbe
|
7.
|
Mhe. Maryam Thani Juma
|
Mjumbe
|
8.
|
Ndg. Ali Alawy Ali
|
Katibu, na
|
9.
|
Ndg. Haji Jecha Salim
|
Katibu
|
Mheshimiwa Spika, baada ya utangulizi huo sasa naomba nichukue fursa
hii adhimu kutekeleza jukumu langu la msingi lililonileta mbele ya Baraza lako
Tukufu.
FUNGU G 01: WIZARA YA KATIBA NA SHERIA
Mheshimiwa Spika, Wizara ya Katiba na Sheria, katika mwaka wa fedha 2020/2021 inategemea kutekeleza Programu
kuu tatu (3) na Programu ndogo tano (5) pamoja na mafungu manne (4) yanayojitegemea, licha ya kukabiliwa na changamoto
mbali mbali inazozikabili zikiwemo uhaba na ubovu wa baadhi ya ofisi zake kama
vile majengo ya Mahakama mbali mbali Unguja na Pemba, uhaba wa vyombo vya
usafiri na uhaba wa vitendea kazi katika sehemu mbali mbali katika nchi yetu.
Mheshimiwa Spika, Kamati yetu imeridhishwa sana na utekelezaji wa
programu za Wizara ya Katiba na Sheria baada ya kuona kuwa taasisi zinazohusika
na utetekelezaji na usimamizi wa masuala ya haki zimepiga hatua kubwa ya
kundeleza usimamizi wa haki katika jamii. Aidha, Kamati imeridhishwa sana na
utendaji wa Ofisi ya Mufti pamoja na kutoa elimu ya masuala ya dini ya Kiislamu
ikiwemo ndoa na talaka katika jamii.
Mheshimiwa Spika, kwa mara nyengine tena, Kamati yangu inatoa
masikitiko yake juu ya ukosefu wa gari kwa ajili ya mheshimiwa Mufti Mkuu wa
Zanzibar jambo ambalo limekuwa likipigiwa kelele na Baraza lako hili tukufu
kila inapowasilishwa Bajeti ya Wizara hii katika kila mwaka wa fedha. Kamati
inaishauri Serikali kwa kupitia Wizara ya Fedha na Mipango kulipa uzito suala
hili kwani muda umekuwa mrefu na changamoto hii bado haijapatiwa ufumbuzi.
FUNGU G 02: MAHAKAMA KUU
Mheshimiwa Spika, Mahakama ni miongoni mwa mihimili mikuu ya nchi
inayotarajiwa kuimarisha na kuongeza upatikanaji wa haki, kuheshimu utawala wa
sheria, kuzingatia haki za msingi za binadamu na ushirikishwaji wa shughuli za
kidemokrasia nchini pamoja na kujenga misingi imara ya Utawala Bora.
Mheshimiwa Spika, Kamati inaishauri Serikali kufanya juhudi za
kukamilisha jengo la Mahakama kuu Tunguu katika muda uliopangwa. Hata hivyo,
bado kuna haja ya kuangalia uwezekano wa kutafuta fedha kwa ajili ya kujenga au
kuyafanyia matengenezo baadhi ya majengo ya mahakama ambayo kwa kiasi kikubwa
hayalingani na hadhi yake, Mahakama nyingi za Mikoa na Wilaya ziko katika hali
mbaya kimiundombinu ikiwemo Mahakama ya Wete na Mkokotoni.
Mheshimiwa Spika, Kamati yetu inashauri uongozi wa Mahakama kwa
kushirikiana na Afisi ya Mwanasheria Mkuu kufanya tathmini kwa wahitimu
wanaotoka katika Chuo cha Skuli ya Sheria Zanzibar katika kila mwaka ili kuona
kama lengo lililokusudiwa linafikiwa au kuna marekebisho yanapaswa kufanywa
baada ya kuona uwezo wa wahitimu hao.
FUNGU G 03: AFISI YA MWANASHERIA MKUU
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, Afisi ya Mwanasheria Mkuu miongoni mwa
majukumu yake ya msingi ni kutoa ushauri wa kisheria kwa Serikali na Taasisi
zake, kuandaa Miswada, Kanuni na matangazo ya kisheria pamoja na kuiwakilisha
Serikali Mahakamani kwenye kesi zote za madai dhidi ya Serikali.
Mheshimiwa Spika, Afisi ya Mwanasheria Mkuu imeweka programu ndogo ya
Kutoa Ushauri wa Kisheria, Kutayarisha na Kusimamia Mikataba ya
Serikali;programu ambayo kimsingi utekelezaji wake unatimiza lengo kuu la
kuanzishwa kwa Afisi hii katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Aidha,
Kamati inatoa shukrani na pongezi za dhati kabisa kwa Afisi ya Mwanasheria Mkuu
pamoja na Tume ya Kurekebisha Sheria kwa kazi nzuri waliyoifanya ya kuipitia na
kurekebisha sheria mbali mbali nchini ambapo mchango wake ni mkubwa katika
kujenga misingi ya demokrasia.
Mheshimiwa Spika, sambamba na hayo, Kamati imeridhishwa na
uanzishwaji wa Afisi ya Mwanasheria Mkuu, Gombani, Pemba jambo ambalo
litawarahisishia wananchi na wakaazi wa Pemba kupata huduma za kisheria kwa
wakati na bila ya usumbufu wowote. Vile vile, Kamati yetu imeridhika na utendaji
wa Afisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali katika kusimamia majukumu yake na
hivyo tunaomba wazidi kutekeleza majukumu yao ya kuisaidia Serikali ili kuzidi
kuimarisha utawala wa haki na sheria.
FUNGU G 04: OFISI YA
MKURUGENZI WA MASHTAKA
Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka, miongoni mwa
majukumu yake ni kuendesha mashtaka Mahakamani, kutoa ushauri wa kisheria na
maelekezo juu ya haki za jinai. Ofisi hii inatarajia kuongeza upatikanaji wa
haki, kuheshimu utawala wa sheria, kukuza haki za binadamu na kukuza ushiriki
wa kidemokrasia nchini.
Mheshimiwa Spika, vile vile, Kamati inaipongeza kwa dhati Ofisi ya
Mkurugenzi wa Mashtaka kwa juhudi zake za kuiwakilisha Serikali katika kesi za
jinai na kupelekea kupungua kwa mrundikano wa kesi Mahakamani hususani kesi za
udhalilishaji wa wanawake na watoto ambazo katika kipindi cha hivi karibuni
matendo hayo yameongezeka mara dufu.
FUNGU
G 05: TUME YA KUREKEBISHA SHERIA
Mheshimiwa Spika, Tume
ya Kurekebisha Sheria Zanzibar ina jukumu kuu la kuzifanyia mapitio ya sheria
nchini ambapo imedhamiria kuzifanyia sheria mbali mbali mabadiliko ili ziende
sambamba na mabadiliko ya mazingira na wakati.
Kamati
imeridhishwa na utendaji wa Tume ya Kurekebisha Sheria kwa kazi nzuri
wanazozitekeleza katika kipindi hiki ambapo baadhi ya sheria amabazo ni za muda
mrefu na hazikuwahi kufanyiwa mapitio wamezipitia na kuweza kuwasilishwa katika
Baraza la Wawakilishi Zanzibar kwa ajili ya kupitishwa na kufanywa sheria bora
zinazoendana na wakati.
HITIMISHO
Mheshimiwa Spika, mwisho, napenda kuchukua fursa hii kukushukuru tena
kwa kunipa nafasi ya kuwasilisha maoni machache ya Kamati yangu kwa niaba ya
Kamati pamoja na kuwashukuru Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza lako tukufu kwa
kunisikiliza kwa umakini wakati wote wa uwasilishaji wa maoni yetu.
Mheshimiwa Spika, mwisho
kabisa,ili kufikiwa malengo yaliyopangwa katika utekelezaji wa majukumu yake,
Kamati inawaomba Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza lako Tukufu waichangie na
wairidhie Bajeti hii na hatimae waiidhinishie Wizara ya Katiba na Sheria
makadirio na makisio ya fedha zote zilizopangwa kutumiwa katika mwaka wa fedha 2020/2021 kama ilivyokusudiwa.
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Kamati yangu Naomba Kuunga Mkono Hoja.
Ahsante,
(Mhe. Suleiman Makame Ali )
Mjumbe,
Kamati
ya Sheria, Utawala Bora na Idara Maalum,
Baraza
la Wawakilishi,
Zanzibar
No comments:
Post a Comment